Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza nitoe shukrani za dhati kwa Rais mpendwa Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais wa Awamu hii ya Tano, kupitia salamu zao kwangu mimi Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini. Kwa kweli ni Serikali iliyofanya kazi kubwa sana katika Tanzania hii na hasa nikizungumzia Jimbo la Mbulu Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipoingia Bunge hili nilikuwa mkorofi sana, nilikuwa nachangia vibaya pia, lakini nilikuwa nafikiri ni lini matatizo haya ya wananchi wa Mbulu yatatatuliwa. Yamefanyika kwa kasi kubwa sana. Nitoe salamu za shukrani pia kwa Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima, Naibu Mawaziri na watendaji wote Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa shukrani hizi kwa sababu kulikuwa na mambo magumu sana yalikuwa hayafanyiki, lakini sasa yanafanyika. Nashukru sana kwa timu hiyo kufanya kazi toka walivyoingia madarakani pamoja na TANROADS. Barabara za Halmashauri ya Mji wa Mbulu zilikuwa hazipitiki nyakati nyingi za mvua na akina mama walikuwa wanapata shida. Kwa sasa ni miaka mitatu barabara hizo zinapitika nyakati zote pamoja na mvua hizi ambazo zinanyesha za mwezi wa Nne hadi wa mwezi wa Sita; na ni historia kubwa kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa na daraja la Magara. Natoa shukrani za dhati kwa Katibu Mkuu ambaye sasa ni Katibu Mkuu wa Wizara ya TAMISEMI. Daraja la Magara ni daraja lenye upana wa mita 84, siyo rahisi ingejengwa kwa sababu mbele ya hilo daraja kuna mlima ambapo wewe Mheshimiwa Naibu Spika, ulipita, mlima wenye kona 130, haupo Tanzania nzima kwa maeneo ambayo nimetembea, lakini leo hilo daraja linajengwa liko katika hatua za mwisho. Naishukuru sana Serikali, nasema ahsanteni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ule mlima uliokuwa umepanda siku ile ulipokuja Mbulu, sasa karibu robo yake au asilimia 30 ya mlima una zege. Kwa hiyo, usiposhukuru wakati fulani utaonekana na wewe huna shukrani na hutambui jitihada za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile mnara uliojengwa katika Tarafa ya Nambis ambako wamehangaika sana Wabunge wenzangu waliotangulia, lakini Tarafa hiyo ambayo ndiyo asisi ya kabila letu kule Nambis, sasa hivi kuna Halotel wananchi wanawasiliana. Naishukuru kwa dhati sana Serikali ya Awamu ya Tano pamoja na maboresho yoyote yaliyofanyika katika Mji wa Mbulu hadi sasa yanayoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije sasa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Eng. Kamwelwe. Utakuwa Waziri wa kwanza kuweka historia katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu kwa kilometa hizo 50 unazofikiri za kutoka Mbulu kwenda Haydom.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna namna nyingine. Jimbo la Mbuli Mjini tunapakana na Jimbo la Karatu, tunapakana na Jimbo la Babati, tunapakana pia wakati fulani na Jimbo la Vijijini, lakini eneo hilo la kilometa kama 389 inayozungumzwa, eneo letu ndiyo tuko katikati tumezengukwa na ukanda wa Bonde la Ufa ambako hakuna njia nyingine zaidi kutokea Haydom kuja Mbulu ama kutokea Karatu - Mto wa Mbu kuja Mbulu. Kwa hiyo basi, hizo kilometa 50 ni muhimu sana, ni za thamani. Mheshimiwa Waziri tunakushukuru kwa mpango wako unavyofikiri wa hata hizo kilometa 50 ili baadaye tuunganishwe kutoka Karatu mpaka kule Shinyanga kutokana na umbali huu kupunguzwa kwa awamu kwa sababu ya uwezo wa Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ninaishukuru pia Serikali na ninaiomba isibadilishe mpango wake huu wa usanifu wa barabara ya Mbuyu wa Mjerumani – Magara – Mbulu ambapo barabara hiyo inaunganisha Mji maarufu wa Arusha, lakini pia inaunganisha Makao Makuu ya Mji wetu wa Babati. Kwa hiyo, ni shukrani pekee tunazitoa, lakini pia tunaomba mpango huu uzingatiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaomba sana Wizara hii pia iangalie utaratibu wa kuweka minara ile iliyopanga katika bajeti ya mwaka huu unaoisha Juni katika Tarafa ya Nambis ambako tulipagiwa minara. Basi tunamwomba Mheshimiwa Waziri na timu yake utekelezaji wa ile minara ufanyike.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaomba watutumie wataalam wa viwanja vya ndege kwani Mkoa wa Manyara hauna uwanja wa ndege, kwa sababu sisi tulio juu ya bonde la ufa kwa maaana ya Mji wa Mbulu huwa usafiri wetu wa dharura ni mgumu. Kwa hiyo, hata tukipata uwanja wa ndege kule Babati, Manyara utasaidia kuunganisha mkoa wetu na mikoa mingine ya nchi kwa kadri ambavyo itawezekakana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hii ni kubwa, ukisoma kitabu cha bajeti kwa kadri ambavyo fedha hizi kidogo kidogo ambazo zimewekwa ili kutatua changamoto zilizoko, zipo jitihada kubwa zimefanyika katika kila Wizara katika Jimbo la Mbulu Mjini ndiyo maana wakati fulani nanyamaza, nasema nitoe tu salama za shukrani lakini zaidi kuomba omba Serikali ihakikishe basi ni kwa namna gani hatua hii inayokusudiwa ya barabara hizi za Dongobeshi - Dareda kupata usanifu na Mbulu - Magara - Mbuyuni kupata usanifu, lakini na hizo kilomita 50 za kwenda Haydom, ambapo itakuwa imepunguza, tutakuwa na kipande cha Mbulu kwenda Karatu na kipande Haydom kwenda Shinyanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, eneo hilo ni muhimu sana, naona anasemeshwa, lakini hili ni ombi kwa niaba ya Serikali na nasema Waziri huyu ni msikivu atakuwa ameweka historia, barabara hiyo inaweza ikaitwa kwa jina lake, ikaitwa Kamwelwe Road kwa sababu ilikuwa haipo, haipatikani, sasa angalau kuna dalili, tunaishukuru Serikali na tunamshukuru na Rais. Naomba Mheshimiwa Waziri afanye ziara alikataa kupita Magara, alisema kona hizo ni nyingi anaogopa, akapita Karatu, safari hii akija apite Magara ili aone huo mlima tunaoulalamikia na hiyo barabara ya Magara ilivyo ngumu na Wanambulu wakiililia wakati wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)