Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mungu kwa kutupa uhai na uzima na kwamba tunaendelea kuwatumikia Watanzania. Niendelee kuwashukuru ndugu zangu wa Mkinga kwa jinsi ambavyo wanaendelea kuniunga mkono ninapotimiza majukumu yangu ya kuwatumikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze vilevile kwa kuishukuru Serikali kwa jitihada inazofanya katika kuwezesha miundombinu ya nchi yetu, hususan Bandari ya Tanga tunaiona kazi inayofanyika ya kupanua na kuongeza kina cha bandari ile, tunawashukuru. Tunawashukuru vilevile kwa Barabara ya Tanga – Pangani – Bagamoyo ambayo tunaambiwa muda si mrefu itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, tunaishukuru Serikali kwa jitihada hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikitoa pongezi hizo, nieleze masikitiko yangu katika maeneo mawili. Kwa muda mrefu sasa tumekuwa tukipigia kelele barabara ya kutoka Mabokweni – Maramba – Bombo Mtoni – Umba Junction – Mkomazi – Same. Barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Tanga na ni muhimu sana kwa watu wa Maramba, Mkinga, Korogwe, Lushoto na Same. Ni barabara inayounganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Kilimanjaro lakini vilevile na nchi jirani ya Kenya. Ni barabara ya kiusalama kwa sababu ipo kwenye ukanda wa mpakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni barabara ya kiuchumi kwa sababu inaunganisha maeneo ya kiutalii. Unapozungumzia utalii unaofanyika Zanzibar fursa hiyo vilevile inakuja kwa upande wa Tanga, unaiunganisha na eneo lile la Bagamoyo lakini vilevile unaunganisha na Mbuga ya Mkomazi ambayo inaanzia upande huu wa Mkinga eneo la Mwakijembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa kiutalii lakini uchumi wa kusafirisha mazao, kama walivyosema wenzangu, bidhaa za mazao ya matunda, mbogamboga, karafuu kutoka kule Kigongoi na mazao ya viungo kutoka Muheza na kule Bosha. Kwa hiyo, ni barabara ambayo tukiona kunakuwa na kigugumizi cha kuishughulikia tunapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Serikali ihakikishe barabara hii sasa inawekewa fedha ili iweze kufanyiwa usanifu. Barabara hii kwa upande wa Kilimanjaro tayari usanifu umekwishafanyika, tunashangaa kwa nini upande huu wa pili barabara hii haifayiwi usanifu? Tunaomba suala hili liweze kushughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna matengenezo yanayoendelea katika barabara hiyo lakini kuna maeneo korofi. Eneo la kwa Mukamba, pale tunahitaji kifereji na kuweka kifusi cha changarawe ili barabara ile iweze kupitika wakati wote. Eneo la Majumba Matatu na lenyewe ni korofi, najua kuna mifereji inaanza kujengwa pale lakini ikamilishwe kwa wakati na iongozewe eneo refu zaidi ili barabara ile iweze kupitika kwa wakati wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni bandari. Mwaka 2014 Kampuni ya Kichina inayojulikana kama Hengia ilionesha nia ya kuja kuwekeza katika nchi yetu kiwanda cha kuzalisha tani milioni 7 kwa mwaka, uwekezaji wa dola bilioni 3, lakini vilevile walisema wataanza na uwekezaji wa bilioni 1, hapa unazungumzia trilioni 2.3 hivi zingeweza kuwekezwa katika kujenga kiwanda kikubwa katika Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara. Hata hivyo, pamoja na jitihada zao za kuomba vivutio mbalimbali vya uwekezaji bado tangu mwaka 2014 mpaka leo kiwanda hiki kimekwama kupata vibali kianze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu hawa walitaka sambamba na kujenga kiwanda cha kuzalisha simenti vilevile waweze kupata fursa ya kujenga jet. Tumekuwa na kigugumizi cha kuwapa ruksa ya kujenga jet kwa sababu za kiusalama. Ni jambo ambalo unaweza kulielewa ukielezwa lakini maswali tunayojiuliza hivi sisi tumeshindwa kuvi-engage vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vikasimamia jet ile hata kama wameijenga wao? Tukawaweka watu wetu wa TRA wakasimamia mapato yetu? Tukaweka vyombo vingine vya bandari vika-manage jet ile ili uwekezaji hu mkubwa tusiweze kuupoteza? Watu wa Mkinga tunahitaji kupata majibu ni lini kitendawili hiki kitateguliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapata hofu kwamba tunaenda kupoteza uwekezaji mkubwa huu wa trilioni 6.5 ambazo zingeingia kwenye uchumi wetu. Tunaiomba Serikali ifanye maamuzi ili watu hawa waweze kuanza ujenzi na kuzalisha simenti. Kama tunadhani hatuwezi kuwaruhusu wao kujenga basi twendeni tukajenge sisi jet ile ili uwekezaji huu usiweze kupotea. Naiomba Serikali ifanye maamuzi ya haraka ili jambo hili liweze kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)