Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata hii nafasi ya kucahngia hii Wizara muhimu ya miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Eng. Kamwelwe, Manaibu Waziri, Engineer Nditiye na Naibu wake, CPA Kwandikwa kwa kazi nzuri walioyoifanya pamoja na Makatibu wao Wakuu. Kwa kweli wanafanya kazi nzuri, hata ukiangalia hii bajeti waliyopewa nafikiri wanastahili, nasi wachukue maoni yetu waweze kuboresha zaidi sekta hii ambayo ni mtambuka ambayo kwa kiasi kikubwa itatusaidia hata kuboresha kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru vilevile kwa ziara aliyoifanya Mheshimiwa Rais katika Mkoa wetu wa Mbeya na mengi aliyoyazungumzia ni pamoja na miundombinu ya barabara. Napenda kumkumbusha Mheshimiwa Waziri kuwa katika ahadi aliyoifanya siku ile, siku ya mwisho ilikuwa ni ujenzi wa barabara ya Mbalizi - Shigamba mpaka Isongole. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ni muhimu sana kwa vile inapitia kwenye maeneo ambayo ni ya kilimo cha mazao yanayotuletea pesa za kigeni; kahawa, pareto, viazi na pia kwenye mazao ya mbao. Vile vile hii barabara inatuunganisha na wenzetu wa Malawi na vilevile inapita kwenye bonde la Mto Songwe ambao ni ubia wa Serikali yetu ya Tanzania na Serikali ya Malawi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aangalie kwani wananchi wanasubiri sana hii ahadi yake ikiwa ni pamoja na barabara ya Isyonje - Kikondo na barabara ya Mbalizi - Chang’ombe kwenda Makongorosi. Hizi ni barabara muhimu sana. Kwa hiyo, nilipenda niliweke hili mwanzoni ili wasije wakajisahau kwa vile hizi ni ahadi za Marais waliotangulia na Rais wetu kasisitiza kwamba hii barabara ijengwe kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vilevile nichangie reli yetu ya TAZARA. Tunapoangalia ujenzi wa kuimarisha miundombinu ya reli ya nchi hii, naomba Wizara isije ikasahau miundombinu ya TAZARA. Reli ya TAZARA uwezo wake ni wa kubeba mizigo isiyopungua metric tonnes milioni tano, lakini mpaka leo hii nilikuwa naangalia report ya Mheshimiwa Waziri hapa, kwa mwaka 2018 na mwaka 2017 ni wastani wa metric tonnes 150,000 tu. Sasa hii ni chini ya asilimia tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia uwezo wa TAZARA; na hii reli ni ya kimkakati, bila hii reli, mizigo mingi ambayo inakwenda kwenye nchi za Zambia, DRC, Malawi na kwa kiasi fulani nchi ya Zimbabwe, hatutakuwa katika ushindani mzuri. Sasa hivi ushindani mkubwa wa Bandari yetu ya Dar es Salaam ni Bandari za Msumbiji, Bandari za Angola na Bandari za South Africa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia Bandari moja tu ya Msumbiji inaitwa Nakal ambayo wakilinganisha na gharama yake na Bandari yetu ya Dar es Salaam wao wako chini kwa asilimia 40. Sasa bila kuiboresha TAZARA na tukategemea hii mizigo iendelee kupitia kwenye barabara, sisi tutaondoka kwenye hiyo biashata na tutajikuta badala ya ku-create value ya bandari yetu lakini kwa kupitia TAZARA, tutakuwa tunafanya value evaporation. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Hongera sana.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile kwa sababu hii reli ni ya ubia kati ya Zambia na Tanzania, inaelekea wenzetu wa Zambia hawana tena umuhimu na hii reli. Nguvu wamezipeleka kwenye hizo nchi nyingine nilizozitaja na wanaona kuna manufaa zaidi ya kutumia hizo bandari nyingine kuliko hii reli yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri Wizara na Serikali iangalie ni namna gani kuangalia upya huo mkataba tulionao kwa sababu hadi leo tunashindwa hata kuchukua pesa ambazo Serikali ya China iko tayari kutukopesha. Kwenye Itifaki Na. 16 nimeona kwenye report hapa bado tunaendelea, tunaangalia namna ya kuharakisha lakini miaka inaenda, hata kukopa tu hizi pesa nayo bado imekuwa kwenye mkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimeona kwenye report ya Kamati, deni la wafanyakazi ni shilingi bilioni 434, hizo ni pesa nyingi sana. Siamini kama kweli hili deni kubwa namna hii kama ni la wafanyakazi tu na zimehakikiwa na hazijalipwa. Je, hii TAZARA itakuwa hai au imefilisika? Kwa sababu kama deni halijalipwa shilingi bilioni 434 ni la wafanyakazi, limehakikiwa toka 2016, leo 2019 hazijalipwa na ninaamini kwamba wafanyakazi wengi wa TAZARA wako katika umri wa kustaafu. Je, mkakati gani ambao unachukuliwa kuhakikisha kuwa tunaajiri wafanyakazi wapya wa reli hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na reli hii, ili ifanye kazi vizuri tunahitaji tuwe na Bandari Kavu pale Mbeya na vilevile tuwe na reli ya kutoka Mbeya -Inyala kwenda Kyela ili iwe kiungo cha Nchi ya Malawi, Msumbiji pamoja Zimbabwe na tuweze kutumia vizuri zile meli zetu tatu ambazo ziko kwenye Ziwa Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni muhimu sana. Hata ukiangalia katika maandiko ya nchi majirani na maandiko ya Kimataifa, zinaonyesha ni kiasi gani tutapoteza biashara ya TAZARA kwa nchi majirani kwa sababu reli ya TAZARA ilikuwa muhimu wakati ule wa ukombozi. Leo nchi zile zimeshakombolewa, nazo ndiyo zinafanya mikakati ya kuhakikisha kuwa watatunyang’anya biashara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na TAZARA, lakini vilevile napenda kuongelea kwa kifupi sana barabara zetu nyingine za Mkoa wa Mbeya ikiwemo barabara ya bypass na upanuzi wa barabara ya kutoka Tunduma kuja mpaka Igawa. Hizi barabara ni muhimu sana kwa ajili ya uchumi wetu. Gharama kubwa za kilimo zinachukuliwa na gharama za usafirishaji ikiwemo usafirishaji wa mbolea na usafirishaji wa mazao yetu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda umekwisha Mheshimiwa. Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)