Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hotuba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda sana niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna ambavyo imewekeza kwenye Wizara hii na inavyojitahidi kutatua matatizo yaliyopo katika subsectors hizo tatu ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na Manaibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wanafanya na kwa namna ambavyo wanajitahidi sana katika kujibu hoja zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi kubwa ambazo zinafanyika ningependa nichangie katika maeneo machache katika changamoto ambazo tunaziona kutokana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambayo ameitoa hivi leo asubuhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi kubwa ambayo imeshafanyika, katika hotuba ya Waziri ameainisha baadhi ya maeneo ambayo yamefanyiwa kazi, yakiwemo ujenzi wa barabara kuu, lami lakini barabara za Mikoa kwa ujenzi wa lami na vilevile kwa ujenzi kwa kiwango cha changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia vizuri, katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri kazi kweli imefanyika, lakini kwa kweli nimuombe Mheshimiwa Waziri tunahitaji kuongeza kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kuongeza kasi kubwa kwa sababu kiwango cha barabara ambacho kimekwisha kutengenezwa mpaka kufikia mwezi wa tatu mwaka huu, kwa barabara kuu ni asilimia 31.9 peke yake ambazo zimekwisha kukamilika kwa mujibu wa takwimu ambazo tumezipata kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ukienda kwenye barabara za Mikoa, hali bado iko vilevile, kwa upande wa barabara za lami, tumefikia asilimia 20 na upande wa barabara za changarawe tumefikia asilimia 12. Kwa hiyo, kasi hii hairidhishi sana, pamoja na kwamba tunafanya mambo makubwa, juhudi kubwa zinafanyika lakini kasi hii ni ndogo na maana yake ni kwamba maeneo mengi ambayo yalikuwa yamepangwa kwenye bajeti iliyopita mpaka sasa bado hayajafanyiwa kazi na ukizingatia kati ya mwezi wa nne na mwezi wa sita tumebakiwa na sehemu chache sana, au katika miezi mitatu hii hatuna uwezo wa kukamilisha kwa ukamilifu wake maeneo ambayo yamesalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pia hata katika ukarabati, hata katika ukarabati utaona tumeweza tu kukarabati barabara zenye urefu wa km 10,000, 968,000 kati ya 34 ambazo zilikuwa zimekusudiwa. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali kutoa fedha kwa ukamilifu ili kusudi miradi ambayo tulikuwa tumeshaipanga katika bajeti iliyopita ya mwaka 2018/2019 iweze kukamilika na tunapokuwa tunapanga kwenye bajeti mpya tuwe na uhakika kwamba zile ambazo tutapitisha kwenye bajeti hii ya mwaka huu wa 2019/2020 tunaweza basi tukapata hizo fedha na zikafanya kazi ambayo imekusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu tunakuwa na mashaka mara nyingi kwamba tunapitisha bajeti hapa lakini baadaye fedha zisipotoka miradi ile haikamilik. Nikitolea mfano wa barabara inayotoka Singida, inayokwenda Hydom mpaka Karatu, barabara hii imekuwa kwa muda mrefu kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa zaidi ya miaka saba, imekuwa ikiahidiwa. Na niseme tu mpaka sasa tunashukuru kwamba tumeona kwamba kuna fedha zimetengwa kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambayo inaanzia pale Singida kwenda mpaka Haydom, na zingine kutoka hydom kwenda karatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe sana Serikali, mara, mwaka wa fedha utakapoanza ni vyema sana shughuli hii ikaanza mara moja ili katika mwaka unaofuata tuweze kutengewa fedha za kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kuwa barabara hii ni muhimu sana, hasa kwa wananchi wa Mkoa wa Singida na Mkoa wa Manyara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wote ambao wanategemea kusafirisha mazao yao, lakini barabara hii pia ina huduma nyingi hasa huduma za afya kwa sasa tunajenga Hospitali ya Ilongero pale, ambayo wananchi wengi wataitegemea kupata rufaa kutoka kwenye vituo vya afya, lakini tunayo Hospitali ya Haydom, tunayo Hospitali ya Nkungi na maeneo mengi ambayo sasa ya uzalishaji ambayo yanategemea sana uwepo wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba na hilo, ipo ahadi ya Rais aliyoitoa pale Mkoani Singida mwaka jana mwezi wa tatu alipotembelea Mkoa wa Singida katika barabara inayotoka Singida mjini, Kinyeto, Merwa inakwenda mpaka Msange inakwenda kuunganisha na barabara kuu inayokwenda Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Wizara hii ikishirikiana na TARURA kutoka TAMISEMI watafuta fedha, watenge fedha ili kusudi upembuzi yakinifu na usanifu wa kina uanze mara moja kwa barabara hii ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais ili wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini waweze kunufaika na uwepo wa barabara ya lami, waweze kusafirisha mazao pamoja na wao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda katika suala la mawasiliano, kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wenzangu mwaka jana hapa tulitoa orodha ndefu sana, kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge ya maeneo ambayo bado hayana mawasiliano ya kutosha na mimi Jimboni kwangu yako maeneo mengi. Ziko Kata tano zina matatizo makubwa kabisa ya usikivu wa mawasiliano, na wawekezaji hawa wa Makampuni haya hawajaweza kuwekeza kule kwa sababu hawawezi kupata faida kutokana na uchache wa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe sana Serikali iweze sasa kutumia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote kuhakikisha maeneo haya ambayo hayana mawasiliano yaweze kupata mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la mizani, nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wameeleza, lakini niisemee mizani ambayo iko katika barabara ya kutoka Singida kwenda Arusha, tunayo mizani pale Mughamo lakini uko mwingine uko Mkoa wa Manyara, mizani hii inafanya kazi masaa kumi na mbili ya mchana peke yake. Mizani hii haina umeme, mizani hii hazina maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hatuna uwezo wa kulinda barabara zetu kwa masaa ishirini na nne, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kujaribu kuwekeza katika maeneo haya, kwa sababu wako watu ambao sasa wanakuwa wanasubiri Watumishi wakishaondoka ile saa kumi na mbili. Wanaanza kupitisha magari yenye uzito mkubwa na matokeo yake barabara zinaharibika na pia Serikali inashindwa kudhibiti hali hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo sio kupata fedha za tozo, lakini lengo ni kulinda barabara zetu ili tusiendelee kujirudia na mtaona barabara ile bado ni mpya lakini tayari imekwisha kuanza kupata maeneo ambayo kwa kweli yana upungufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niiombe sana Wizara, kwa unyenyekevu mkubwa, iko pia barabara inayotoka Singida kwenda Ilongero, kwenda Ngamu hii ni barabara ya Mkoa, na inaenda kuunganisha tena kwenye Mkoa wa Manyara. Barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wa Mkoa Singida na Manyara, niombe sasa ilikuwa imetangazwa km 12.6 za ujenzi kutoka Singida kuelekea Ilongero. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka jana ilipotangazwa mwezi wa kumi na moja mpaka sasa, bado hatua za manunuzi hazijakamilika. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, aweze kufatilia jambo hili, ili ujenzi wa kiwango cha lami katika barabara hiyo uweze kuanza mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja ya Waziri tuweze kupata fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi yote ambayo imepangwa kwa bajeti hii ya mwaka 2019/2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante sana. (Makofi)