Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii. Awali ya yote nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha mchana huu wa leo kusimama hapa na kutoa mchango wangu. Vilevile kabla sijasema chochote naomba nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Wenyeviti wa Bodi zote zilizopo kwenye Wizara hii. Vilevile pongezi zangu ziende kwa Katibu Mkuu na Makatibu wote wa kisekta ambao wanahudumu kwenye Wizara hii na bila kuwasahau Wakurugenzi wanaoendesha taasisi mbalimbali zilizopo ndani ya Wizara hii, wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kuonyesha kwamba ni namna gani sasa wafanyakazi au wateule hawa wa Mheshimiwa Rais wanaanza kumfahamu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli anataka kuipeleka nchi sehemu gani, tunataka kwenda wapi. Kwa hiyo, nawapa pongezi, Mwenyezi Mungu awajaalie, awape umri mrefu, waendelee kuhudumu kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nimeingia kwenye Bunge hili nilitoa hotuba ambayo nilipewa mwongozo na Mheshimiwa Jenista pale. Niliomba kuitoa Liwale kwenye nchi hii kwa sababu ilikuwa kama vile haihitajiki na nikapewa mwongozo kwamba huo ni uhaini. Nilisema Liwale tuitoe kisiwani na leo nasimama hapa napenda kusema rasmi kwamba Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imesikia kilio change, sasa mwelekeo wa kuitoa Liwale kisiwani unakwenda kutoka. Nilisema tuitoe Liwale kisiwani kwa mawasiliano, leo asilimia 70 ya Liwale tunawasiliana, nasema hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa pongezi zangu kubwa sana kwa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, kwa kweli kwa Wilaya ya Liwale umetutendea haki. Napenda kutoa pongezi kwa CEO wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, najua leo hii wanasherehekea miaka 10 ya mafanikio na nawaunga mkono kwa mafanikio waliyoyafikia na kuitoa Liwale kisiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, nilisema tuitoe Liwale kwa mawasiliano ya barabara na mara nyingi nimesimama hapa nilikuwa naiongelea barabara ya Nangurukulu - Liwale, Liwale – Nachingwea. Namwambia Mheshimiwa Waziri ahsante sana, kwa sababu barabara hizi nimekwenda nimeziona kwenye maandishi yake tayari ametutengea fedha kwa ajili ya kwenda kufanya upembuzi yakinifu na hatimaye iweze kujengwa kwa kiwango cha lami na naomba Mwenyezi Mungu ajalie hili na tupate fedha hizo ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijikite kwenye upande wa TAZARA. TAZARA kama ambavyo Mheshimiwa Mwambalaswa amesema, wenzetu wa Zambia wameshapoteza interest na reli hii kwa sababu tayari wana reli mbadala kwa ajili ya uchumi wao, sisi ndiyo tumebakiwa na umuhimu wa kubakia kwenye hii reli. Kwa hiyo, naiomba Serikali hebu wajaribuni kufanya mapitio ya mikataba ya hii reli. Kwanza reli hii kwa kiasi kikubwa kwa upande wa uongozi ipo upande wa Zambia zaidi, ndiyo wenye maamuzi, lakini Wazambia hawa pamoja na kwamba ndiyo wenye maamuzi kwa kiasi kikubwa lakini bado hawahitaji tena hii reli. Kwa hiyo, naiomba Serikali ifanye mapitio ili tuone ni namna gani tunaweza kuihodhi hii reli, ikiwezekana basi kila upande wa- operate kipande chao ili na sisi tuweze kujikwamua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ndiyo maana sasa hivi TAZARA wanakwenda kwa kusuasua hata mishahara yao ni ya kusuasua kwa sababu bado hawajapewa ile full mandate ya kuendesha hii barabara ya TAZARA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi zote nilizozisema kwa ajili ya upembuzi yakinifu wa barabara ya Nachingwea - Liwale na Nangurukuru - Liwale, sasa naomba nirejee Mheshimiwa Waziri barabara inayotoka Masasi kwenda Nachingwea. Barabara hii imefanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2015, leo hii kila unapofungua kwenye bajeti unaikuta barabara hii bado inatafutiwa fedha. Barabara hii ni muhimu sana na kwa nini naiongelea barabara hii, naiongelea barabara hii kwa sababu najua hata hiyo barabara ya Nachingwea – Liwale inayokwenda kufanyiwa upembuzi yakinifu, kama barabara ya Nachingwea –Masasi haitojengwa kwa kiwango cha lami, haiwezi kujengwa barabara ya Nachingwea – Liwale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali waiangalie sana hii barabara ya Masasi – Nachingwea, iende sasa ijengwe, huu ni mwaka wa tatu upembuzi yakinifu umekamilika, naomba Mheshimiwa Waziri aitengee fedha ili barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami. Barabara hii inakwenda sambamba na barabara ya Nachingwea – Nanganga. Barabara hizi mbili zikijengwa kwa kiwango cha lami, napata ahuweni kwamba sasa Liwale – Nachingwea inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana na napenda kuisistiza Serikali iendelee kuangalia hii barabara, iweze kujengwa kwa kiwango cha lami ili nami kule barabara ya Nangurukuru –Liwale iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee hii taasisi ya MSL. Mheshimiwa Rais ameonesha nia ya kufufua hii taasisi kwa maana tayari tunaweza kujenga meli kama vile tunavyojenga meli zile pale Mwanza - Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa na Ziwa Tanganyika, tumeona miradi inakwenda kujenga vivuko na meli. Hata hivyo, hii kampuni bado haijaimarika, kampuni hii bado ina madeni makubwa sana, hata wale watumishi bado wanaidai kampuni kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali basi ikiwezekana basi madeni haya Hazina wayachukue ili kampuni hii iweze kujiendesha kwa faida. Kwa inavyoonekana na kwa jinsi CEO wa kampuni hii alivyo- committed ni kwamba Serikali watakapowapa full mandate, kampuni hii inaweza ikafanya vizuri na ikatuinua kiuchumi na vilevile ikatusaidia kwenye usafirishaji wa mazao mbalimbali ya bahari na maziwa makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee hii kampuni ya TTCL, kampuni hii ni kampuni ya Serikali au Umma, tulitaraji sana kampuni hii iweze kwenda mbali kwa maana kwamba iweze kupeleka mawasiliano vijijini huko mahali ambapo hakuna mvuto wa kibiashara. Tatizo la kampuni hii ni mtaji, kampuni hii ina tatizo kubwa sana la mtaji na kwa nini ina tatizo la mtaji? Ina tatizo la mtaji kwa sababu kampuni hii vilevile ina madeni makubwa inazidai taasisi mbalimbali za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi naiomba Serikali sikivu ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, wawape fedha/mtaji TTCL ili waweze kufika mbali kwa sababu sasa hivi TTCL wapo kwenye mashindano na makampuni mbalimbali, lakini kama hawatakuwa wanapata mtaji wa kutosha, kampuni hii hawawezi kwenda mbele na hawawezi kuingia kwenye ushindani wakashinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali iendelee kuifutia madeni au ikiwezekana Hazina waifutie madeni basi hii TTCL nayo ili iweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu hapa wanabeza ununuzi wa ndege, wanayo haki ya kubeza kwa sababu ili waendelee kubaki kule…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: …ili waweze kuendelea kubaki kule ni lazima waseme hayo wanayoyasema, lakini kwa kweli ununuzi wa ndege una tija kubwa kwa nchi yetu kwa ajili ya kukuza utalii… (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja mia kwa mia. Ahsante. (Makofi)