Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii kuchangia pia kwenye Wizara hii, asubuhi nilipata fursa ya kuuliza swali la nyongeza juu ya mpango wa ujenzi wa reli ya Standard Gauge Kaskazini mwa nchi hii na Mheshimiwa Waziri majibu yake yalikuwa ni kwamba tusiwahishe mambo tusubiri wasilisho lake mambo mazito yanakuja. Sasa na mimi kama alivyoongea

Mheshimiwa Mzee Nsanzugwanko nimecheki kwenye kitabu hiki nimekuta hadithi ni ile ile upembezi yakinifu, usanifu wa kina muhandishi mshauri, mhandisi muelekezi. Hizi hadithi zinatakiwa zifike mahali sasa zikome. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka kuona ni vitu vinajengwa miundombinu ijengwe hadithi ya kujenga reli hii ya Kaskazini ya kuanzia Tanga Musoma imekuwepo tangu nikiwa mtoto mdogo wa shule leo kichwa kimekuwa cheupe bado kipande cha Arusha Musoma hata haijawahi kufanyiwa kazi. Kwa hiyo, nilikuwa nafikiri kama haiwezekani kujenga ni bora tukae kimya tusihamasishe hivi vitu wananchi wapate moyo kwamba kuna kitu kinakuja. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, wenzetu wakoloni waliotutawala miaka hiyo ya 1890 walikuwa na maono wakajenga reli ya mwazo Tanga kwenda Usambara sisi leo miaka 100 baadaye bado tuna mipango ambayo bado haieleweki. Niishauri Serikali tufike mahali tuwe wa kweli kama hatuwezi tuseme hatuwezi. Imeongelewa sana hii reli ya standard gauge sasa hivi tunajenga vipande viwili lakini kwa uhakika kama ambavyo Wabunge wengi wameshauri na makundi mbalimbali yameshauri kipande cha kutoka Tabora kwenda Kigoma ni kipande ambapo hakiepukiki kama kweli tunataka kujenga reli hii iwe na faida ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli inabeba abiria na mizigo tutamaliza kujenga reli hii huko tunakotaka kujenga lakini mwisho wa siku tutakosa mizigo ya kubeba kama hatutakuwa na mikakati ya kutafuta mizigo iko wapi, nadhani ni muda muafaka sasa Serikali ijielekezi hivi hi mizigo ya kubeba iko wapi? Imesemwa sana tuna soko DRC , tuna soko Burundi lakini tufahamu kwamba kuna wenzetu wa Kenya na wenyewe wana reli ya aina hii na wenyewe wanaelekea huku huku na hivi majuzi tumesikia Marais wa nchi hizo mbili wameingia mkataba wa mashirikiano, sasa kama hiyo mizigo tunayoilenga DRC itakwenda kwa wenzetu wa Kenya hivi hii ya kwetu mizigo ya kubeba itatosheleza? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tuwe na mpango wa nini tunakwenda kubeba hata kama tunakwenda kuijenga reli hii. Nafikiri sasa pia ni vizuri reli hii ya sasa ya kati tumeijenga kwa kutumia vyuma kutoka nje ya nchi, lakini sisi tunaambiwa tuna-deposite ya vyuma huko Mchuchuma miaka mingi, hivi hata hatuoni fahari tunaona fahari kutumia ndege kwa sababu tuna Twiga pale nyuma hivi kwa nini tusione fahari kujenga reli hizi kwa kutumia chuma ambacho tunacho ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tuna nia njema ya kukuza uchumi wa nchi hii hebu hizo reli mbili ambazo tunaambiwa ziko kwenye upembuzi yakinifu, usanifu wa kina kwa maana ya reli ya Mtwara na kuendelea na hii ya Tanga tuijenge kwa kutumia chuma ambacho kinapatikana ndani ya nchi yetu. Kwa namna hiyo nadhani huo uzalendo ambao tunausema kila siku tutakuwa tumeuona vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihame kwenye eneo la pili, Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL). Shirika hili ni kati ya mashirika machovu nchi hii. Sote tunafahamu historia ya Shirika la TTCL, shirika hili lina shida kubwa ya upungufu wa mtaji, halina mtaji na ndio maana mambo yake hayaendi. Shirika hili limeshindwa kuingia kwenye soko la ushidani na mashirika mengine ya mawasiliano ambayo tunayo nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo ambalo linasikitisha Taarifa ya CAG imebaini kwamba, mmoja wa wadaiwa sugu wa shirika hili, yaani watu wanaodaiwa na shirika hili ni Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambayo Mheshimiwa Eng. Kamwelwe wewe ndiye Waziri wake. Unadaiwa shilingi bilioni 20.6 fedha ambazo TTCL wametumia kulipa shughuli na kazi za mkongo wa Taifa, wakati huohuo Wizara yako imeshikilia akaunti ya mapato ya mkongo wa Taifa. Sasa TTCL kwa sura hiyo itawezaje kujiendesha kama wewe mwenyewe baba hutaki kulipa fedha ambazo wao wenyewe wamezizalisha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tunaomba kama TTCL kweli tunataka liwe shirika ambalo litaingia kwenye soko la ushindani tuwape fedha zao. Walipeni bilioni zao 20 halafu washindane na hao wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye eneo la tatu, Uwanja wa Ndege wa Lake Manyara. Uwanja wa ndege wa Lake Manyara umekuwepo katika vitabu vyetu tangu mwaka juzi, mwaka jana hata mwaka huu, lakini sioni dalili ya uwanja ule kujengwa. Wananchi wamekubali kutoa maeneo yao, wananchi wamekubali kupisha ujenzi wa uwanja ule, lakini mpaka leo hawajalipwa fidia na uwanja haujengwi. Sasa kama Serikali haina fedha muwaambie wananchi waendelee na shughuli zao za kimaendeleo kuliko maeneo ya wananchi mmeyachukua halafu bado hakuna kitu kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom, tumeiongea mara nyingi sana. Mheshimiwa Waziri imetengwa shilingi bilioni 1.4 na imeegeshwa tu kwenye Barabara ya Mto wa Mbu, Loliondo na Nata, shilingi bilioni 1.4, barabara ya kilometa 389 zinakwenda kufanya nini? Nadhani wakati mwingine mnaturidhisha tuone vitu vimeandikwa, lakini kwa uhakika hakuna kitu unaweza kwenda kufanya kwenye barabara ile kwa hiyo, utuambie hii barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom inakwenda kujengwa lini? Na hii bilioni 1.4 ni za kujenga lami au ni kwa ajili ya kuendelea na upigaji uleule wa upembuzi yakinifu, usanifu wa kina nambo mengine kama hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimeona kwenye barabara ile fedha hizi umezielekeza kwenye kipande cha Mbulu – Haydom, yaani unakwenda kujenga katikati fulani, mwanzo umeacha na mwisho umeacha. Mheshimiwa Waziri hata ukiingia saluni hata kichwa hakianziwi huku katikati unaanzia huku pembeni; sasa wewe kwa nini umeenda kuanza hii barabara pale katikati? Kama kweli tunataka kujenga barabara hii na tuone ina manufaa ya kibiashara na kiuchumi kipande cha Karatu – Mbulu nashauri uanzenacho ndio kipande ambacho kina magari mengi, lakini ndiyo kipande ambacho udongo wake wakati wa mvua unateleza sana; hata muwa Mheshimiwa Engineer Kamwelwe unaanza kule mwisho au huku mbele, lakini wewe unapiga muwa katikati, una lako jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwamba, kwa kweli, barabara hiyo kama mna nia ya kuijenga muanze kuijenga kuanzia Karatu kwenda Mbulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Barabara ya kuunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu ilikuwa Barabara ya Oldian Junction – Matala – Mto Sibiti na kwenda Mkoa wa Simiyu, lakini sasa ni kama barabara hii imehamishwa ndio hii ya Karatu – Mbulu – Haydom. Hebu Serikali itoe kauli na Wananchi wajue, Waziri Mkuu alikuwa Mang’ola aliulizwa swali hilo akasema barabara imeshafanyiwa usanifu na baada ya usanifu tutapata fedha na kujenga barabara hiyo. Sasa barabara ya kuunganisha Arusha na Simiyu ni barabara ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali muwaambie wananchi, wananchi wasisubiri kitu ambacho hamuwezi kujenga. Nakushukuru. (Makofi)