Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaac Aloyce Kamwelwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano imethibitisha kwamba ni Serikali ya watu iliyowekwa na watu kwa ajili ya watu na ndiyo maana utaiona tu hotuba ya Mheshimiwa Waziri Kamwelwe imesheheni miradi mbalimbali ya maendeleo yenye kulenga kuitengeneza Tanzania mpya katika sekta mbalimbali za Uchukizi, Ujenzi na Mawasiliano. Nimpongeze Mheshimiwa Rais, Makamu wake, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri, Makatibu Wakuu na Watendaji mbalimbali ambao wamehusika katika maandalizi ya hotuba nzuri hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ipo barabara ya kutoka Butengorumasa- Iparamasa-Mbogwe-Masumbwe inatakiwa sasa iendelezwe ili iweze kuiunganisha sasa Mkoa wa Geita, Mkoa wa Shinyanga, Mkoa wa Tabora, Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii itarahisisha sana mawasiliano baina ya Wananchi wa Mikoa hii niliyoitaja kwa sababu Wananchi wa Geita hawatakuwa na sababu sasa ya kupita Nzega ndiyo aende Tabora. Atatakiwa tu anatoka Geita anapita Mbogwe, anakwenda Ushetu, anakwenda Kaliua, Kaliua sasa hapa anachangua; kama anakwenda Kigoma atapita Urambo atakwenda Kigoma huko, akifika Kaliua anaweza akakata kuelekea Mpanda- Sumbawanga au anarudi kwenda Tabora, Tabora anakuja Singida mpaka hapa Dodoma na Dar es salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri nilikuwa naomba barabara hii kwasababu sehemu ya Butengorumasa-Iparamasa-Mbogwe mpaka Masumbwe imeshapandishwa kuwa barabara ya TANROADS, nilikuwa naomba na hiki kipande kilishosalia sasa cha kutoka Masumbwe-Mwabomba-Nyankende-Bomba A-Uroa-Uyoa- Sungwa-Mwamnange-Buhindi mpaka Kaliua na yenyewe ichukuliwe na Serikali ili iweze kupandishwa kwa kiwango cha TANROADS na ikibidi ufanyike usanifu wa kina ili hatimaye ije ijengwe kwa kiwango cha lami ili iweze kuwasaidia wananchi wa maeneo haya waweze kuwa na mawasiliano ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa kukubali ombi la kuipandisha hadhi barabara ya kutoka Bwelo, Makao Makuu ya Wilaya ya Mbogwe kwenda Karumwa katika Wilaya mpya ya Nyang’hwale, jambo hili na lenyewe litatufungua kwahiyo tutakuwa na urahisi wa kuwez kutoka Wilaya moja hadi nyingine bila ya kupata kikwazo cha aina yoyote katika usafiri wa watu na vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia kuipongeza Serikali kwa hatua yake ya kutenga fedha kwa ajili ya usanifu wa reli na kuanza kuijenga kwa kiwango cha Kimataifa (standard gauge) na mpaka sasa ujenzi unaendelea kutoka Dar es salaam mpaka Morogoro na hatua ni nzuri na hatimae tutaona kutoka Morogoro kuja Dodoma na baadaye Dodoma-Tabora-Isaka-Mwanza na kutoka Tabora hadi Kigoma baadaye Kaliua mpaka Mpanda na Kadema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa lolote na tunaamini kabisa kwamba uwepo wa miundombinu namna hii ambayo ni rafiki itachochea ukuaji wa uchumi katika Taifa letu hasa ikizingatiwa kwamba Nchi yetu imejaaliwa kuwa ni lango la Nchi mbalimbali ambazo ziko land locked ambazo hazina Bahari na bahati nzuri sisi tumekuwepo katika ukanda ambao tuna Bahari, tuna Maziwa Makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo uwepo wa Maziwa na Bahari unarahisisha uwepo pia wa Bandari na Serikali yetu imejipambanua katika kuhakikisha kwamba zinakuwepo Bandari ambazo zina uhakika na zinazoweza kutoa huduma kwa nchi zetu ambazo ziko jirani na sisi. Kwa mfano, Bandari ya Dar es salaam, Bandari ya Tanga, Bandari ya Mtwara na ile Bandari ya Bagamoyo ambayo inatarajiwa kujengwa hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naishauri Serikali iendelee kuziangalia pia zile Bandari za kwenye Maziwa kwa mfano, tunazo Bandari katika Ziwa Victoria, kwa Geita pekee tunayo Bandari ya Nyamirembe, Bandari ya Nkome, Bandari ya Nungwe, zote hizi zinahitaji kuwekewa miundombinu ili kusudi ziweze kutoa huduma kwa Wananchi wa Mkoa wa Geita na ili waweze kuwasiliana na wenzano wa Mikoa ya jirani, kwa mfano, Mkoa wa Kagera na Mkoa wa Mara na Nchi jirani kwa maana ya Uganda na Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mawasiliano ya anga, niipongeze Serikali kwa kununua ndege mpya na ambazo zinaendelea kufanya kazi. Vilevile niipongeze Serikali kwa kuendelea na upanuzi wa viwanja vya ndege ikiwemo kiwanja cha ndege cha Mwanza. Niungane na Wabunge wenzangu ambao wanatoa mapendekezo kwa Serikali kwa sababu nedge zimepatikana basi zianze kuwepo route za kutoka Mwanza kuja Dodoma ambapo ndiyo Makoa Makuu ya Serikali ili kusudi Wananchi wa Mwanza na Mikoa mingine ya Kanda ya Ziwa waweze kufika kwa urahisi katika Makoa Makuu ya Nchi pamoja na kwenda sehemu za Dar es salaam na Mikoa mingine kama kule Mbeya kwa uwanja wa Songwe na uwanja wa Nduli kule Iringa na sehemu zingine ambazo kama Kilimanjaro na sehemu zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa kwamba Serikali yetu imejipanga na ndiyo maana inatekeleza kwa kiwango kikubwa mambo mengi ambayo yanahitajika kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe tu kusema maneno haya kwa sababu kazi kubwa iliyofanywa na Wizara hii inatosha na niseme tu kwamba naiunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri asilimia 100 kwa 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.