Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunifikisha kwenye kipindi hiki cha Ramadhani ya mwaka huu, kwani wapo tuliofunga nao mwaka jana, 2018 leo wako mbele ya haki na wengine wameshindwa kushiriki Ramadhani hii kwa hali na maradhi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa leo naomba nianze mchango wangu kwanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Manaibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote kwenye wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhudumia jamii yetu kwenye sekta hii muhimu ya kulinda afya zetu. Namwomba Mungu awape umri mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa bajeti ya mwaka 2018 kwa kunipa watumishi 80 wa Sekta ya Afya, lakini kutokana na uhaba mkubwa tulionao watumishi wale wamekuwa kama tone la damu baharini. Bado Hospitali ya Wilaya ya Liwale yenye wodi nne zinahudumiwa na mhudumu mmoja tu kwa shift ya usiku kutokana na uhaba wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe shukrani kwenye bajeti hii kwani wilaya yetu imetengewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, maana ile iliyopo ilikuwa ni kituo cha afya, hivyo kushindwa kukidhi hadhi ya kuitwa Hospitali ya Wilaya. Ombi langu ni fedha kuja kwa wakati ili ujenzi huu uanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya na vituo viwili vya afya vya Mpengerewa, Kibutuka, bado Halmashauri ya Liwale inakabiliwa na uhaba mkubwa sana wa gari la wagonjwa (ambulance). Jiografia ya Liwale yenye vijiji 76 ni ngumu sana. Hivyo, namna ya kuwafikisha wamama hasa wajawazito ni ngumu sana, ukizingatia kuwa zahanati zetu hazina wataalamu na vifaa vya kutosha. Kwa hiyo, uhitaji wa gari la wagonjwa ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kupunguza mlundikano wa wagonjwa kwenye hospitali na zahanati zetu, wakati sasa umefika wa kuimarisha kada ya Mabwana na Mabibi Afya kwenye Kata na Vijiji vyetu. Watumishi hawa ni muhimu sana kwenye jamii zetu. Waswahili husema, “kinga ni bora kuliko tiba.” Elimu ya afya ikiwafikia wanajamii juu ya kutunza afya zetu na mazingira yetu kwa ujumla tutaepuka magonjwa ya mlipuko. Kada hii ya Mabwana/Mabibi Afya ni kama imesahauliwa kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ajira kwa watoto ni jambo linalotishia maisha ya watoto wetu kwani kila kukicha bado ongezeo la ajira kwa watoto mitaani linaongezeka siku hadi siku hasa kwa mijini. Wako watoto wanaosukuma baiskeli kuwatembeza watu wenye ulemavu wa viungo na wasioona kwenye shughuli zao za kuombaomba. Vilevile wako watoto wanaotumwa na wazazi wao kwenda mitaani kupita kuombaomba. Hivyo, naiomba Wizara kuja na mkakati maalum wa kukomesha ajira hizi za watoto na kuwaondoa watoto wanaoombaomba mitaani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Wananchi wa Tanzania kukosa kuwaingiza kwenye mpango wa Bima za Afya (NHIF) ni kutokuwatendea haki, kwani familia za Maaskari wetu zimekuwa zikihangaika sana hasa zile familia zinazoishi uraiani. Pamoja na kazi ngumu wanazofanya za kulinda nchi yetu, lakini bado hawana uhakika wa afya zao na familia zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Wazee nchini ni changamoto kubwa hapa nchini kwani hadi leo Serikali haitaki kuleta Sheria ya Wazee ili kuweza kutambua hao wazee. Pamoja na kuwa na matangazo sehemu mbalimbali kama vile “Pisha Mzee”, “Wazee Kwanza”, matangazo ambayo yanashindwa kuwatambua wazee hao, kwani hakuna sheria inayowatambua; kwa nini Serikali inakuwa na kigugumizi cha kuleta Sheria ya Wazee hapa Bungeni ili wazee hawa waweze kutambuliwa? Tukumbuke kuwa sisi sote ni wazee watarajiwa. Hivyo, hiki tunachokifanya ni kujikaanga kwa mafuta yetu.