Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia machache katika Wizara hii muhimu kwa afya ya Watanzania. Nianze kwa kuunga mkono hotuba ya Kambi ya Upinzani ambayo imesheheni ushauri na mambo mazuri kwa sekta yetu ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete chini ya uongozi mzuri wa Profesa Janabi na pongezi hizi ziende kwa madaktari wote, wauguzi na watumishi wote wa taasisi hiyo. Taasisi hii imekuwa ikifanya kazi nzuri na imesaidia sana kupunguza gharama za matibabu nje ya nchi, lakini bado kuna mtatizo ya vitendea kazi ambavyo vitarahisisha matibabu kwa wagonjwa na hata kwa watoa huduma. Mfano, kuwa na mashine zote kwa ajili ya vipimo hapo hapo hospitali kuzuia kwenda kufanya vipimo nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi hii imekuwa inakusanya fedha nyingi, lakini pale inapoomba tena fedha ambazo walikusanya wao hawapati. Mfano, mwaka jana waliomba bilioni nne, hawakupata wakati waliweza ku-save zaidi ya shilingi bilioni 12 za kwenda kutibu wagonjwa nje ya nchi. Nashauri Serikali itenge 30% ya mapato hayo ili kuwawezesha kuboresha huduma kwa wagonjwa na kurahisisha kazi kwa madaktari wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, udhaifu wa vipimo vya tiba katika hospitali zetu, kumekuwa na tatizo hili kwa wagonjwa kupewa majibu tofauti na maradhi waliyonayo na hii husababisha wagonjwa kutopona maradhi waliyonayo pamoja na kupewa dawa ambazo si sahihi kwa magonjwa hayo na kufanya dawa hizo kuwa sumu mwilini, badala ya kuwa tiba na hata kusababisha vifo kwa wagonjwa wetu. Wanaopona ni wale wenye uwezo wa kwenda hospitali nyingi kwa ajili ya kupima upya au kwenda nje ya nchi. Je, ni wangapi ambao hawana uwezo huo wanapoteza maisha. Nashauri Serikali kuchukua hatua kwenye suala hili ili kunusuru maisha ya Watanzania na kuhakikisha umakini unakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwajibikaji wa watumishi wa Sekta ya Afya; zipo taratibu na sheria zilizowekwa kwa ajili ya uwajibishaji wa watumishi wa afya, yapo Mabaraza ya Madaktari na Baraza la Wauguzi; haya ndiyo yenye jukumu la kuwawajibisha na si vinginevyo. Toka Awamu hii ya Tano imeanza tumeona viongozi wa kisiasa na wasiokuwa na mamlaka wala taaluma hiyo kuingilia kuwawajibisha Madaktari na Wauguzi pasipo kufuata taratibu. Tunajua upo upungufu unaofanwa na watumishi hao, lakini ni muhimu kufuata taratibu zilizopo. Tusipofanya hivyo tunapunguza morali wa kufanya kazi kwa watumishi hao muhimu wa sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha mchango wangu huo mdogo wa sekta hii ya afya.