Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo. Nimpongeze Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa kazi nzuri na kubwa anayofanya katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Wakurugenzi wote na wataalam mbalimbali waliopo Wizarani na katika taasisi zetu chini ya Wizara hii. Mheshimiwa Waziri ni msikivu sana na anapokea ushauri kutoka kwa kila mdau. Naibu Waziri pia amekuwa mstari wa mbele kutoa ushauri wa kitaalam na kuweka mfumo bora katika utekelezaji wa shughuli za Wizara. Wataalam wote hutupa ushirikiano wa karibu na pia elimu tunapohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ushauri katika maeneo machache ili kuboresha huduma. Kwanza, nishauri kuendelea kupunguza gharama zisizo za lazima ili kuongeza ufanisi kama mlivyopokea ushauri wangu wa ujenzi wa vituo vya afya na hospitali kutoka shilingi bilioni 4.5 kituo cha afya hadi milioni 500 au milioni 400 na Hospitali za Wilaya kutoka shilingi bilioni 705 hadi shilingi bilioni 1.5, hali ambayo ilifanya tujenge vituo vingi zaidi na pia hospitali nyingi za Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Kitengo cha Manunuzi (procurement) cha MSD kiboreshwe na tuwe na team ndogo nyingine ambayo itafanya kazi ya kuhakiki manunuzi. Naamini bado tunaweza kupunguza gharama za manunuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze kwa kuendelea kutumia force account. Muhimu pia ni kutumia mfumo wa PPP katika kuboresha huduma za afya. Mfano eneo la huduma za maabara, nchi nyingi huwa na wataalam na vifaa vya maabara ambazo wanashirikiana na hospitali, vituo vya afya na zahanati kutoa huduma. Siyo lazima tuwekeze sisi katika kila hospitali au kituo cha afya. Pia huduma za Radiology za X-Ray, Utrasound, CT-Scan, MRI, tushirikiane na watoa huduma private. Naamini kwa kufanya hivyo bei za huduma hizo zitateremka.

Mheshimiwa Naibu, nishauri pia suala la telemedicine lipewe kipaumbele. Hii itasaidia kusogeza huduma ya mabingwa katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kitengo cha kutengeneza viungo bandia kiboreshwe. Watanzania wengi wenye uhitaji wa viungo bandia hushindwa kuvinunua kutokana na kuwa na gharama kubwa. Tuangalie namna ya kuboresha na kutoa huduma hii katika maeneo mbalimbali nchini badala ya maeneo machache kwa bei kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri Serikali iangalie namna ya kuwa na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote itakayokuwa ni lazima (universal health care insurance). Leteni sheria mapema Bungeni ili Watanzania wengi wapate bima ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nishauri tuendeleze sera yetu ya kinga bora kuliko tiba. Katika magonjwa mengi tunaweza kutoa elimu ya kinga badala ya kuingia gharama ya tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la usalama wa chakula na lishe, nashauri Serikali tujikite katika kinga kupunguza tatizo la lishe bora ili kuepuka tatizo la kudumaa na utapiamlo. Nashauri Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto ishirikiane na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Maliasili na Utalii na Viwanda na Biashara ili kwa pamoja tuweke mpango na mkakati wa kutokomeza utapiamlo na suala la kudumaa (malnutrition stunting). Pia elimu zaidi juu ya namna ya kupata lishe na mazoezi kwa ajili ya magonjwa yasiyoambukiza (non-communicable diseases) itolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri TFDA iweke vifaa vya kupima mazao hasa ya mboga mboga na matunda katika masoko yetu yote makubwa. Leo hii tunakula vyakula hasa mbogamboga na matunda vilivyopigwa dawa (sumu) kabla ya kumaliza muda maalum wa tahadhari kumalizika (chemical residuals from insecticides). Pia katika mifugo tunalishwa nyama na maziwa ya mifugo kutoka kwa mifugo iliyopigwa chanjo na dawa za matibabu kabla ya muda maalum kuisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri pia Serikali iangalie uwezekano wa kuondoa kodi katika vifaa tiba na vifaa wanaotumia wenye matatizo mbalimbali ya afya. Mfano baiskeli za walemavu na viti maalaum vya wagonjwa (wheel chairs) pamoja na magongo na vifaa mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe pia Serikali isaidie kuboresha huduma katika Kituo cha Wazee Sarame-Magugu. Pia kutupatia X-Ray katika Kituo cha Afya Magugu. Niwashukuru kwa kupata vituo viwili Jimbo la Babati Vijijini, Magugu na Haiti. Naomba sana kupata vifaa vyote katika vituo hivyo ili kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri Serikali iangalie namna ya kuboresha na kuweka utaratibu wa kuboresha sekta ya dawa za asili. Katika nchi mbalimbali hasa Bara la Asia na Mashariki ya Mbali (South East Asia), wameweza kuratibu, kuweka rekodi na kufanya utafiti wa mimea na dawa za asili kwa manufaa ya raia wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Tanzania katika kila eneo kuna dawa za asili na zote hazina rekodi wala kufanyiwa utafiti katika maabara ili kuwa na uhakika wa hizo dawa na nini kipo ndani yake (herbal medicine). Nashauri tungeanzisha mafunzo ya dawa za asili katika vyuo vyetu. Tuna rasilimali nyingi sana ambazo zinaweza kutumika kuleta tiba mbadala (homeopathy na allopathy).

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, nashauri wataalam wa jadi au wa asili wapatiwe mafunzo ya kitaalam. Mfano tunao wataalam wa asili wenye uwezo wa kufunga mifupa, kurudisha mifupa iliyosogea katika sehemu zake (dislocation), wakipatiwa mafunzo zaidi wanaweza kutoa huduma vizuri zaidi. Hospitali ya Daseda Haydom wanawashirikisha na kuwasaidia kusoma X-ray ili wafunge mifupa vizuri. Nashauri Serikali iweke maabara maalum kwa ajili ya kupima mimea mbalimbali na dawa hapa nchini pamoja na kuweka rekodi za dawa hizo ili kupata dawa za uhakika na bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiboresha sekta hii na pia katika vipodozi (cosmetics) tunaweza kukuza ajira na kuongeza mapato na ikawa ni kivutio cha utalii. Mfano Morocco, Jordan, India, Indonesia, Thailand na nchi zingine zinapata mapato makubwa kutokana na dawa za asili na vipodozi (cosmetics). Ni sekta kubwa sana, nashauri vyuo vyetu vya tiba na maendeleo ya jamii viboreshwe sana. Mitaala yake iboreshwe na vifaa vya kufundishia na kujifunza ili wanaohitimu wawe na viwango vya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nirudie, tuboreshe vyuo vyetu vya uuguzi pamoja na vya afya (nursing and medicine) nchini ili Watanzania wengi wasome na hata kama hakuna ajira nchini waweze kwenda nchi za nje. Tukiwa na wataalam wetu nje ya nchi, watatangaza nchi yetu na kuleta mapato ya fedha za nje. Nchi nyingi za Asia hufanya hivyo. Huduma pia ya mazoezi ya viungo ni muhimu na wataalam ni wachache (physiotherapists).

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.