Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kuchangia bajeti hii. Nampongeza Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa maono yake makubwa ya kuwasogezea wananchi wa Tanzania huduma muhimu za jamii, hususan katika sekta hii ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto; Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile na Makatibu Wakuu wote kwa kazi kubwa na ya kutukuka wanayoifanya kwa uadilifu, upendo, bidii na weledi mkubwa. Tunapongeza huduma kubwa za kisasa na utaalam mkubwa katika hospitali zetu za rufaa. Nipongeze utolewaji wa miundombinu ya vifaatiba na madawa. Tunapongeza sana juhudi za kukuza uwezo wa watumishi wa sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, naomba nitoe rai kwa Wizara hii kuzingatia umuhimu na haja ya kuajiri watumishi wengi katika zahanati na vituo vya afya, hasa katika kada ya Medical Officers ambao wanahitajika kwa wingi sana. Naomba kutoa rai pia kwa Wizara kuhakikisha kuwa zahanati zilizojengwa katika vijiji vyetu kwa nguvu za wananchi zinamalizika na zilizomaliziwa zipatiwe vifaa na watumishi ili zifanye kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Jimbo langu la Wilaya ya Ileje, Kituo cha Afya Mbebe bado hakijamaliziwa na kwa sasa kwa miundombinu ya Wilaya ya Ileje wananchi wanalazimika kupeleka wagonjwa Malawi ambako ni karibu zaidi kuliko kwenda Itumba kwenye Hospitali ya Wilaya. Zahanati ya Mapogoro hukohuko Mbebe haijamaliziwa na hivyo kuifanya Mbebe ikose huduma za afya kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi walijitoa kujenga Kituo cha Afya Itale, tunaomba Serikali itusaidie fedha za kumalizia kituo hiki cha afya. Tunashukuru Serikali kwa kutoa ambulance ndogo, tunaomba basi Kituo cha Afya cha Itale kikamilishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba Serikali itusaidie kuwezesha Vituo viwili vya Ibaba na Lubanda vilivyomaliziwa kwa fedha ya Serikali basi vizinduliwe ili vianze kazi. Mheshimiwa Ummy aliahidi ambulance Kata ya Lubanda, tunaomba sasa ipatikane.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Ikinga, Zahanati ya Kikota imemaliziwa ujenzi bado kufunguliwa. Tunaomba ifunguliwe ili wananchi wa Ikinga wapate huduma hii muhimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Isongole ni kubwa na ipo kwenye Mji Mdogo wa Wilaya ya Ileje. Kata hii ina watu wengi sana lakini inakosa kituo cha afya na kuifanya Zahanati ya Isongole kuzidiwa na wagonjwa na kushindwa kumudu mahitaji ya huduma za afya kwa wananchi. Sasa hivi barabara kuu inajengwa na imepita Isongole kwa hiyo kutakuwa na ongezeko kubwa zaidi la wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ileje ina miundombinu migumu sana na Mheshimiwa Waziri alishatembelea, anafahamu. Kata ya Ndola inahitaji kituo cha afya kupunguza adha kwa wananchi wa Ndola. Kata ina hosteli ya wasichana na changamoto zikitokea wanakosa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Itumba ndiyo Makao Makuu ya Wilaya na ndipo ilipo hospitali ya wilaya. Tunaendelea kuishukuru Serikali kwa kutupatia fedha za kujenga hospitali ya wilaya shilingi bilioni 1.5 pamoja na zilizotolewa siku za nyuma. Hospitali itakuwa na majengo muhimu saba na itajitosheleza lakini kwa sasa tunahitaji X- ray mashine ya kisasa ya radiologist na friji ya kuhifadhia damu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Isoko ni hospitali ya mission lakini imekuwa ikitoa huduma kubwa sana kwa Wanaileje na kuunga mkono juhudi za Serikali. Tunaomba Wizara iwafanyie secondment Medical Officers kwenda Isoko kuziba pengo. Hospitali ya Isoko haina uwezo wa kuajiri Medical Officers kuziba pengo lakini kwa kuwa wanahudumia wananchi wa Ileje na Watanzania na kwa kuwa wanashirikiana na Serikali, tunaomba sana Serikali iridhie kutoa secondment kwa watumishi wawili au watatu kwenye ngazi ya Medical Officer ili kukidhi ufanisi wa huduma zinazotolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.