Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia na kipekee nipongeze sana hotuba ya kamati pamoja na hotuba ya Kambi ya Upinzani ambapo ni mwanakamati. Ninaomba sana Wizara itekeleze yale yote hasa maoni hayo ambayo kwa kweli ni ya msingi na ninaamini mkiyachukua tutaboresha sana sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa suala zima la bajeti. Wizara hii kama ambavyo wote tunajua ni Wizara muhimu sana kwa afya ya Taifa letu na hata hivyo tunavyosema kwamba Tanzania ya viwanda haitawezekana kama rasilimali watu wetu watakuwa wagonjwa na hawapati huduma bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo la kusikitisha sana kuona kwamba Wizara hii pamoja na kutengewa bajeti kubwa tulipitisha takriban shilingi trilioni moja lakini kwenye fedha za maendeleo tulipeleka bilioni 561 mpaka leo tunapozungumza imeenda shilingi bilioni 91 tu sawa na asilimia 16, hivi kweli asilimia 84 ya fedha tulizozipitisha ndani ya Bunge hili bado hazijapatikana na tunafikia mwisho wa mwaka tunaomba kujua ni kwa kiasi gani tunategemea ubora wa huduma za afya kama fedha ambazo tumekaa hapa ndani kwa kipindi cha miezi mitatu haziendi tunaiuliza Serikali tuna sababu gani ya kukaa hapa Bungeni tunapitisha fedha nyingi kiasi hicho ambacho tunaamini zinaenda kufanyakazi lakini fedha hazitoki huku tukiambiwa kwamba Serikali inakusanya fedha fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri atapokuja ku-windup atuambie hivi hiyo asilimia 84 inategemewa kwenda lini na hizo huduma zote ambazo zimekwama kwa huu muda ni kwa kiasi gani wananchi wame-suffer ni kwa kiasi gani watu wamefariki kwa sababu ya kukosa hizi fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo kutokana na uchache huu wa fedha naamini ndiyo sababu tunakuwa na matatizo mengi kwenye Wizara hii. Kwa mfano kuna watu wengi sana wanaenda kwenye hospitali wanafanyiwa vipimo lakini vipimo vinakuwa tofauti na ugonjwa alionao. nitatoa mifano hata Waziri akiita baadhi ya Wabunge ambao wamepata matatizo hayo ni wengi sana. Kwa mfano majuzi hapa niliangalia kwenye TV kuna binti mmoja amepimwa Muhimbili, amekutwa na matatizo ameambiwa ana matatizo ya ini, ini limeungua amekaa karibu anakufa amepelekwa India only to find ana matatizo ya moyo sasa watu wa namna hii wako wengi kiasi gani. Nilikuwa naomba Waziri atuambie tatizo ni uelewa wa madaktari wetu au technician au tatizo ni vifaa tulivyonavyo haifanyi kazi nilikuwa naomba hilo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la magonjwa yasiyoambukiza limekuwa kubwa sana na tatizo kubwa sasa hivi pamoja na diabetes ni pamoja na tatizo kubwa la kansa. Leo tunavyozungumza ni hospitali mbili tu za Serikali zina mashine ya mionzi yaani radiograph sasa na hii iko hospitali ya Ocean Road na hospitali ya Bugando lakini tuna hospitali zaidi ya mbili za rufaa tuna hospitali ya Kanda ya Mbeya, tuna hospitali ya Kanda ya Kilimanjaro kwa maana ya KCMC Kanda ya Kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipo kwenye kamati ya maendeleo ya jamii kwa muda mrefu madaktari au wakuu wa hospitali hizi mbili kilio chao kikubwa kimekuwa ni fedha kwaajili ya kununua bunkers kwa ajili ya kuweka hizo bunkers ili waweze kuweka hizo mashine hospitali ya KCMC na hospitali ya Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna sababu ya kupandisha hadhi au kuwa na hospitali za Kanda kama hatuna vifaa. Kwa hiyo, tatizo la Ocean Road kuwa na mrundikano litakuwa palepale kwa sababu wagonjwa katika Kanda kwa mfano Nyanda za juu kusini, wagonjwa katika Kanda ya Kusini, wagonjwa katika Kanda ya Kaskazini, wanapopata matatizo ya kansa wameshakuwa wameshatambulika wana kansa wanatakiwa wapate mionzi hawapati mionzi wanatakiwa tena waende Ocean Road kwa hiyo tunarudisha tatizo palepale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukiangalia hata kitabu cha maendeleo cha mwaka huu hakuna fedha yeyote ya maendeleo iliyotolewa katika hospitali ya KCMC wala hospitali ya Mbeya. Kwa hiyo, wagonjwa wetu katika maeneo husika wataendelea kufariki kwa kukosa huduma za msingi kwa sababu tunaambiwa huduma kansa inaweza ikatibika kama imeweza kujulikana mapema lakini watu wamegundua lakini bado hawana access kwenye hizo hospitali, kwa hiyo. nilikuwa naomba hilo pia Waziri atusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye suala zima la watumishi ni wazi kwamba watumishi wa Wizara ya Afya, sekta ya afya kwa ujumla wake ni wachache sana na Waziri wanakiri ni karibu asilimia 50 lakini vijijini asilimia mpaka 74 hakuna wauguzi, hakuna wataalam wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa na tunaendelea pia kujenga vituo vya afya tunaendelea kujenga zahanati lakini suala la watumishi halijaonyeshwa. Inasikitishwa kuambiwa kwamba ni kwasababu ya kuondolewa kwa wale waliokuwa na vyeti feki, sijui waliokufa. Wewe unatambua kwamba kama ikama ipo tayari na fedha zao za mishahara zipo sasa kama hawa wameondolewa replacement ipo madaktari wapo kibao wana-graduate lakini vilevile wauguzi wanajaa sasa hoja ni nini hapa watuambie labda Serikali haina fedha lakini kutuambia wanaendelea na uhakiki na uhakiki wakati hawa watu walikuwa kwenye ikama na fedha zao zipo maana yake ukimuondoa, lazima umrudishe ambaye yupo na wapo mitaani ukipiga filimbi hapa madaktari ambao wako mitaani wapo kibao manesi wako kibao kwa sababu kila siku kila mwaka wana-graduate. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa kweli tunaendelea kuweka afya za watu wetu rehani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nielezee kwamba ni makamu mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa chama changu na kwa maana hiyo sina budi kuongelea suala la wazee, toka nimeingia kwenye Bunge hili tumekuwa tukiambiwa tuna Sera ya wazee toka 2001 lakini mpaka ninavyozungumza sheria haijaja na ndiyo sababu wazee wanaendelea kudhalilika katika nchi hii. Wazee wanaendeshwa kwa sera kwa miongozo kwa taratibu lakini hakuna sheria nilikuwa naomba kila siku tunapigwa danadana tuwambia kwanini wanasema wanaendelea kuboresha, wanaendelea kufanya hivi lakini kwa nini msilete sheria? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli hatuoni aibu kwamba wazee hawa ndiyo wametulea wazee hawa ndio wameleta uhuru katika nchi hii lakini wazee hawa leo mmesema mara mtawapa vitambulisho, mara sijui mtawapa nini lakini wazee hawa wananyanyasika kwelikweli na ninajua kwamba siyo wazee wote hawana uwezo lakini hata wale wasio na uwezo ikija sheria itawatambua kwa sababu hata leo nikimuuliza Waziri mwenye dhamana tuna wazee kiasi gani katika nchi hii sidhani kama wana-database. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana suala la wazee ni la muhimu lakini vilevile suala la pensheni ya wazee ni la muhimu siyo wazee tu waliokuwa wanafanyakazi, hata wasiokuwa na kazi walitakiwa walau wawe na posho ambayo itawasaidia kujikimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nije kwenye suala la ndoa za utotoni limeelezwa kwa kina lakini niseme ni jambo la aibu sana kuona kwamba sheria yetu ya mwaka 71 bado ndiyo tuliyonayo lakini kipekee niseme kwamba jambo hili lilipelekwa mahakamani na tayari limeshakuwa ruled out kwamba sheria hiyo ibadilike vile vifungu vilitakiwa vibadilishwe lakini kinachosikitisha Serikali kupitia AG wamekata rufaa. Sasa nashindwa kuelewa hivi ni kweli tunataka watoto wetu waolewe katika umri huo? Sheria ya mwaka 71 wakati tulikuwa hatuna shule leo tunasema kila mtoto aende shule yeye eti sheria bado ni ileile kwahiyo kuna confusion na ni lazima huo utata uweze kutatuliwa kwa sisi Wabunge kukaa pamoja na kuona umuhimu wa kubadili sheria hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo nilitaka kuzungumiza ni suala zima la huduma ya unasihi. Tuna matatizo makubwa sana Tanzania. Sasa hivi kuna suala stress na sonona (depression) na hii inatokana na changamoto za maisha ikiwa ni pamoja na kutopandishwa mishahara ikiwa ni pamoja na vyuma kukazwa na mambo mengi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo hili linahitaji ushauri nasaha. Tuna vyuo vyetu vya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii, hasa cha Ustawi wa Jamiiā€¦

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Susan kengele ya pili ilishagonga. Ahsante sana. Nilikuwa nasubiri umalizie hoja yako muhimu.

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwanza.

NAIBU SPIKA: Zimeshagonga mbili Mheshimiwa. Ahsante sana.