Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuungana na Watanzania kwa msiba mzito uliotupata wa Dkt. Mengi. Sisi watu wa Kilwa tunamkumbuka sana Dkt. Mengi. Mwaka 1993 Mzee Kingunge Ngombale Mwiru aliitisha harambee ya kuchangisha ujenzi wa sekondari ambapo Mheshimiwa Dkt. Mengi alitoa milioni 20, tutakukumbuka daima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala zima la kuhitaji mtaalam wa mionzi katika Hospitali ya St. Marks Kipatimu. Hospitali hii tayari tumepata X-ray mpya lakini hatuna huyo mtaalamu. Naomba Serikali itupatie huyo mtaalamu ili wananchi waweze kupata uduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili naomba nizungumzie gharama za utoaji maiti katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kuna changamoto kubwa. Kama ambavyo tunafahamu Hospitali ya Muhimbili ndiyo hospitali kuu ya rufaa, kwa hivyo, wagonjwa wengi wakishindikana wanakwenda pale na upo uwezekano wakatibiwa kwa muda mrefu sana. Sasa ikitokea mgonjwa amepata umauti kuna mtihani mkubwa wa gharama na kinachofanyika pale ni kuzuia maiti isitoke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na tatizo kubwa sana hili na wauguzaji walio wengi wanashindwa kugharimia gharama hizo na matokeo yake ile maiti inazuiwa na hatimaye huenda kuzikwa na city. Naomba tuangalie upya utaratibu katika suala hili kwa sababu binadamu anastahili heshima na azikwe kwa mujibu wa mila na desturi zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiti chako kilishawahi kutoa ruling kikasema kwamba marehemu hadaiwi, sasa hii sijui inakuwaje? Kusudio siyo kukopa ni kupata tiba na ni haki yake, sasa hana uwezo na yeye ameshafariki kwa nini wauguzaji wasiruhusiwe kuchukua maiti wakamzike ndugu yao kwa heshima kubwa? Naomba Serikali iangalie suala hili ni tatizo kubwa, Wabunge tumekuwa tukipigiwa simu mara kwa mara kusaidia katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ningeona niliseme leo ni kuhusiana na suala nzima matibabu ya wazee na hii Sera ya Matibabu Bure kwa Wazee. Ni sera ambayo imeanza kutekelezwa lakini kwa kusuasua. Niishauri Serikali basi ilete Muswada wa sheria ili sasa iwe kwa mujibu wa sheria na siyo sera ili basi wazee wetu wa kuanzia miaka 60 waweze kupata matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la Kituo cha Afya Njinjo pale kwangu, tungeomba Serikali itupatie fedha kama ambavyo vituo vingine vimepata. Kituo kile kimekuwa chakavu sana, tunaomba nacho kipatiwe fedha hizo ili kiweze kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia wananchi wameanza kujenga Kituo cha Afya Chumo na Somanga. Tunaiomba Serikali nayo itusaidie ili vituo hivi vikamilike.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la UKIMWI. Wafadhili wameendelea kujiondoa katika kufadhili ugonjwa huu. Kwa mfano, hawa wenzetu PEPFAR wao wenyewe wamepunguza msaada wao katika suala nzima la UKIMWI kwa kiasi cha dola milioni 119. Hii ni kwa sababu kasi ya kupima bure kufikia asilimia 90 ni kama inaenda kwa kusuasua. Kwa hiyo, ni nini mkakati wa Serikali wa kuwaruhusu wananchi wajipime binafsi kwa kutumia kile kipimo cha mate. Naomba Serikali iharakishe ili wafadhili hawa waendelee kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la homa ya ini. Sisi Wabunge tumepata chanjo ya homa ya ini ni vizuri lakini Watanzania walio wengi bado hawajapata chanjo hii. Niiombe Serikali iangalie uwezekano wa kutoa chanjo hii kwa Watanzania wote kwa sababu ugonjwa huu ni hatari na unatishia amani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la bima ya afya kwa wote. Mimi ni miongoni mwa Wabunge tuliotembelea nchi ya Rwanda kuona namna gani wenzetu wanatoa hii bima ya afya kwa wote. Wenzetu wamefanikiwa sana na wanachokifanya ni kuhusisha wahudumu wale wa ngazi za chini, wanawapa majukumu na wao ndio wanafanya ushawishi kwa wananchi lakini wanawa-train kiasi kwamba wawe wanaweza kutoa huduma ya kuzalisha, kuchoma sindano na vitu vya namna hiyo. Niombe Serikali ije na huu Muswada wa Sheria ili basi huduma ya bima ya afya itolewe kwa watu wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)