Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Nina mambo machache ambayo napenda nichangie kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, natoa shukrani zangu za dhati kwa fedha iliyotolewa na Serikali kwa ajili ya kukarabati Kituo cha Afya cha Bonazi, nashukuru sana. Mara nyingi huwa nasema mafanikio ni baba wa matatizo kwa sababu unapokarabati kituo cha afya kikawa bora maana yake kitavutia wagonjwa wengi zaidi kukitumia na maana yake ni kwamba kituo kikishakuwa bora zaidi kukitumia na ni kwamba kituo kikishakuwa bora zaidi kikavutia wagonjwa wengi zaidi maana yake unahitaji kuongeza bajeti ya madawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nasema mafanikio ni baba wa matatizo na huwezi ukaliepuka hilo kwa sababu ukiliepuka hatutaendelea. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Afya na TAMISEMI wafanye kila kinachowezekana kuongeza bajeti ya Kituo cha Afya cha Bunazi na hasa upande wa madawa ili tuweze kukabiliana na ongezeko la wagonjwa ambao sasa watatumia kituo hicho na wameanza kukitumia kwa sababu sasa operesheni pale zinaweza kufanyika na mambo mengine ambayo hapo kabla yalikuwa hayafikiriwi kufanyika pale sasa yanafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri iliyofanya kwa kujenga Kituo cha Afya cha kisasa Kabyire. Mheshimiwa Waziri niliwasilisha maombi maalum kwa ajili ya kituo hicho cha kisasa ambacho ni bora kuliko vituo vyote katika Mkoa wa Kagera, naweza nikasema, lakini changamoto kubwa ni bajeti, inabidi tutoe bajeti maalumu kwa ajili kuhakikisha kituo hicho kinafanya kazi kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyofahamu Wilaya yetu ni mpya, hatuna Hospitali ya Wilaya, tunatumia Hospitali Teule. Tulishatenga eneo la kujenga Hospitali ya Wilaya, tunaomba sana Serikali ituweke katika awamu itakayofuata ili na sisi tuweze kujenga hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kitabu cha hotuba Mheshimiwa Waziri ameonyesha fursa mbalimbali za Tanzania katika ununuaji wa madawa na sasa tunawakilisha nchi 15. Pia nampongeza amefuta tozo mbalimbali na ameeleza kwamba wameandaa mwongozo wa uwekezaji katika viwanda vya dawa. Nimejaribu kutafuta mwongozo huo sijauona lakini uzoefu wangu unanituma kwamba mwongozo kama unaeleza tu fursa zilizopo bila kueleza incentive za kisheria zitakazotolewa kwa wale watakaowekeza, bila kutoa ardhi, mimi niseme Halmashauri ya Misenyi tuko tayari kutoa heka 400 kwa ajili ya kujenga viwanda vya madawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Mbunge wa eneo hilo nikizungumza na Halmashauri ya Misenyi imezungumza, mje niwakabidhi eneo hilo ili muweke hiyo center ya madawa. Ukijenga center ya madawa Misenyi maana yake umejenga Afrika Mashariki kwa sababu utaenda Uganda, South Sudan, Rwanda, utaenda kokote kule. Kwa hiyo, nachukua nafasi hii kuwakaribisha ili tufanye ujenzi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, naomba Mheshimiwa Waziri katika bajeti yake atenge fedha za kutosha za madawa, tunaita noncommunicable disease kwa sababu katika ngazi ya zahanati na vituo vya afya mara nyingi bajeti zao ni ndogo, madawa ya presha na kadhalika wanakuwa hawana. Mara nyingi nimekutana na watu wengi wako Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wakifuatilia dawa hizo nikawa najiuliza kama ikishajulikana fulani anaumwa na yuko sehemu fulani na dawa anazotumia ni aina fulani na katika Hospitali ya Rufaa zipo, utaratibu ufanywe kuhakikisha dawa hizi zinapelekwa mpaka ngazi ya vijiji na vitongoji ili kuwasaidia wagonjwa hawa kupata dawa ambazo vituo vyetu au zahanati haviwezi kuwa nazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilima mia moja. (Makofi)