Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu. Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na tunaweza kusimama katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri wa Wizara hii, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile kwa kazi kubwa wanazozifanya. Hakika wanaitendea haki Wizara hii. Mheshimiwa Ummy, kwa kweli umetupa heshima wanawake wenzio, Mwenyezi Mungu aendelee kukupigania na kukuinua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia Katibu Wakuu, Naibu Katibu Mkuu na Madaktari wote Tanzania nzima kuanzia Taifa na wale wa wilayani na mikoani. Kwa kweli madaktari wanafanya kazi nzuri na kubwa. Mwenyezi Mungu aendelee kuwatia nguvu na kuwabariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee, nampongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa na nzuri anazozifanya. Ndani ya kipindi kifupi ameweza kufanya mambo makubwa; nikianza la kwanza, ameweza kuboresha upatikanaji wa madawa hospitalini; pia ameweza kukarabati vituo vya afya takribani 325; na amefanikiwa kutoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za mikoa mipya. Kazi nyingi sana amezifanya Mheshimiwa Rais, nikianza kuziorodhesha hapa nina dakika saba zitaisha. Kwa kweli anastahili pongezi. Mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siwezi nikaitendea haki roho yangu bila kumwombea Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli. Naanza kwa kusema Baba katika Jina la Yesu, mbariki sana Mheshimiwa Dkt. Magufuli, mbariki Mheshimiwa Waziri Mkuu, mbariki Mheshimiwa Ummy Mwalimu, wabariki Mawaziri wote akiwemo Mheshimiwa Jenista Mhagama, wabariki Mawaziri wote na Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania. Mwenyezi Mungu kibariki Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nasema wote tuseme Amen. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Amen! (Makofi/Kicheko)

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, niingie sasa kwenye hoja za msingi. Nianze kwa kuomba. Jimbo la Nkasi Kusini lipo umbali mrefu sana kutoka Makao Makuu ya Wilaya. Wanawake wanaotoka Kata za Kara, Ninde na Nkandase wanapata shida sana wanapopata ujauzito.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi juzi mwanamke mmoja amefia njiani wakati anakwenda hospitali kujifungua. Namwomba mdogo wangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu atufikirie sana Jimbo la Nkasi Kusini kutuletea ambulance. Wanawake wale wakipata ambulance tutakuwa tumeokoa maisha ya akina mama wengi katika Tanzania hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niipongeze Serikali kwa kutujengea Hospitali za Wilaya. Katika Mkoa wa Rukwa wilaya zote zimepata Hospitali za Wilaya, lakini bado Wilaya moja ya Sumbawanga Mjini haijapatiwa Hospitali ya Wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia bajeti iliyopita ilipanga kujenga Hospitali ya Rufaa katika Mkoa wa Rukwa ambapo ilipanga kujenga katika Kijiji cha Milanzi, lakini mpaka sasa hivi hatujaona ujenzi ukianza Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Rukwa. Pia hospitali iliyopo ya mkoa majengo yake yamechakaa, jengo la mortuary limechakaa, halina hadhi ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tulikuwa tunaomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili, ile hospitali ya rufaa ianze kujengwa, itasaidia sana kuepusha msongamano katika hospitali iliyopo ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee sasa Wilaya ya Nkasi, kuna vituo vya afya vimeanza kujengwa, wananchi wanajenga kwa nguvu zao.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata muda wako umeisha, lakini kwa maombi uliyopiga, nakuongeza dakika mbili. (Makofi)

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nakushukuru sana, Mungu akubariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Akasu, Kate, Ninde na King’ombe wameanza kujenga maboma ya vituo vya afya. Naomba Mheshimiwa Waziri atuongezee nguvu, awape moyo wale wananchi wanaojenga wapate support ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga Mjini, kaka yangu Jacob Ntalitinginya ameweza kuwakopesha wanawake vikundi karibia 99 ambapo walikuwa wanasubiri kwamba labda Benki ya Wanawake ingejengwa Mkoa wa Rukwa lakini haijajengwa. Yeye ameweza kuwakopesha wanawake, pia ameweza kukusanya mapato karibia asilimia 110. Kwa hiyo, nampongeza sana Jacob Ntalitinginya, Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dakika mbili zimeisha na nilikuwa na hoja nyingi lakini naomba kwa haya tu, niongelee sana suala la ambulance kwa wanawake katika Jimbo la Nkasi Kusini kwa Mheshimiwa Mipata.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)