Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kutoa mchango wangu katika bajeti hii ya Afya. Kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya uhai, kwa kutuwezesha leo kuwepo katika Bunge lako hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nampongeza Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. Tunaiona na kila mmoja anaiona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza pia Mheshimiwa Waziri, pamoja na Naibu Waziri, Makatibu Wakuu wale wawili na timu nzima ya Wizara hii kwa kubwa ambayo wanaifanya kutuhudumia hasa katika eneo la Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza Serikali kwamba katika Bajeti ya dawa imeongezeka sana kutoka shilingi bilioni 31 ambayo tulikuwa tunaizungumzia mwaka 2015/2016 sasa tunazungumzia shilingi bilioni 270 hivi sasa ninavyozungumza. Naipongeze sana Serikali kwa kweli kupitia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza Wizara na Serikali kwa Mkoa wangu wa Singida. Mkoa wangu umekuwa wa pili kwa kupata upatikanaji wa dawa zile 30 muhimu kwa Mkoa wa Singida. Mpaka sasa hivi tunapata asilimia 96.6, ni wa pili kutoka Mbeya ambao wanapata asilimia 97.1. Kiambatanisho Na. 5 cha Rejea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilete maombi machache sasa baada ya pongezi hizo. Ombi langu la kwanza, Mheshimiwa aliyemaliza kuzungumza dada yangu Mheshimiwa Sakaya amezungumzia Kituo cha Makazi ya Wazee wasiojiweza pale Sukamahela. Mheshimiwa Naibu Waziri alifika tarehe 29 mwezi wa 10 mwaka 2018 pale akaongea na wale Wazee na pia alituahidi kwamba katika yale makazi 17, Mikoa 17 katika nchi nzima, akasema wana mpango sasa wa kuyapunguza na kuboresha yakawa machache kugawa katika Kanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walisema mojawapo ya Kanda nadhani Sukamahela itakuwa ni Kanda mojawapo. Nilisimama siku ile na kusema kwamba tunawakaribisha kwa sababu Sukamahela lile eneo ni kubwa, tunazo ekari 80 pale za kutosha kabisa, pia ni barabara kuu imepita pale, tunayo maji, tunao umeme, kwa hiyo, huduma zote zipo, tunawakaribisha sana; na wananchi wako tayari sana ili muweze kufanya eneo lile kwa kanda ya makazi kwa Kanda ya Kati. Tunaikaribisha sana Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu la pili, ulipofika Mheshimiwa Naibu Waziri tarehe 29 hiyo mwezi wa 10 mwaka 2018, tulikuomba pamoja na mambo mengine ambulance. Mpaka sasa hivi bado hali ni ngumu, catchment population ya Hospitali ya Wilaya ya Manyoni kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012 ni 250,000, lakini hivi ninavyozungumza nadhani sasa inakwenda kwenye 500,000 na zaidi kwa sababu maeneo mengi sana wanakuja; Sikonge wanakuja, maeneo ya jirani, Bahi huko wanakuja. Kwa hiyo, imesha-double ile catchment population.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kwa kweli pamoja na huduma nyingine, lakini ambulance tunaihitaji sana. Tulikuwa nayo lakini sasa imechakaa, iko kwenye mawe. Tufikirie sana kama Wizara, mgao utakaotokea wowote ule, Manyoni muifikirie sana kwa ile Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lingine la tatu, Wilaya ya Manyoni sasa ni kubwa imekuwa, kile kilikuwa Kituo tu cha Afya, tukakikuza na tukakipandisha hadhi lakini majengo yale Mheshimwia Naibu Waziri amefika hata Mheshimiwa Waziri ameshafika pale. Ile siyo hadhi ya Wilaya kwa yale majengo. Mnapofikiria kujenga Hospitali za Wilaya katika nchi hii kwa mgao unaofuata, naomba sana muifikirie Wilaya ya Manyoni. Tunalo eneo tumelitenga, tumelipima, pana zuri, nasi mtupe huo mgao wa kujenga sasa Hospitali ya Wilaya, maana sasa Wilaya ya Manyoni imekua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu lingine la mwisho ni Ikama. Kama nilivyosema Wilaya ya Manyoni imekua sana, tunapokea wagonjwa wengi sana sasa hivi; pamoja na Vituo vya Afya vile viwili tulivyojengewa, tunashukuru, lakini bado ile Wilaya tunapokea wagonjwa wengi sana. Tunao Madaktari wanne tu. Watatu wanafanya kazi, lakini mmoja pia ni DMO, sasa ni watatu tu ambapo ilitakiwa wawe 14 mpaka 20, lakini ni wanne tu. Hebu fikiria hiyo situation, ni ngumu sana. Mtufikirie sana ikama kwa maana ya Madaktari pamoja na Wahudumu wengine kama Manesi. Kwa kweli hali ni ngumu, wamezidiwa sana kihuduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nashukuru sana, niachie na wengine wazungumze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja Wizara hiyo. Ahsante sana. (Makofi)