Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyoko mezani. La kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai, lakini la pili nawashukuru sana wananchi wa Urambo kwa kunipa ushirikiano wakati wote, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kuishukuru Wizara ya Maji ikiongozwa na Profesa Mbarawa, Mheshimiwa Aweso, Katibu Mkuu Profesa Mkumbo, Naibu wake na watendaji wote kwa kweli kazi wanachapa, nawatakia kila la heri waendelee kuchapa kazi, kazi wanaiweza, kitu kikubwa ni kuwezeshwa kifedha tu. Ni uhakika usiopingika kwamba chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kazi inafanyika katika Wizara ya Maji, hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa niaba ya wananchi wa Urambo nichukue nafasi hii kushukuru sana Wizara kwa kutuwezesha sisi watu wa Urambo kuingizwa katika Mradi wa Maji kutoka Lake Victoria. Nawashukuru sana sana kwa sababu tulikwenda sisi kwenye Mto Malagarasi tukaona umbali ulioko kutoka Malagarasi mpaka Urambo halafu pia na mwinuko wa nchi, kwa kweli tunashukuru kwamba tunapata maji kutoka Lake Victoria kwa sababu ni kilomita 90 tu kutoka Tabora, tunashukuru sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali moja tu ambalo ningeomba wanijibu kwa niaba ya wananchi wa Urambo wakati wa kuhitimisha ni kwamba, sasa huu mradi wa maji kutoka Lake Victoria ni wa mwaka gani wa fedha ili na sisi tuishi kwa matumaini. Kwa hiyo tutashukuru sana kujua ni lini tunapata maji kutoka Lake Victoria, mwaka gani wa fedha. Kwa kuwa Urambo kuna shida kubwa sana ya maji kwa kweli nikiulizwa wakati wowote kipaumbele au shida kubwa inayowakabili wananchi wa Urambo; la kwanza nitasema maji kwa sababu sisi water table imeshuka, yaani maji yameshuka chini sana kwa hiyo ni vigumu kupata maji na hakuna njia nyingine ambayo inaweza kutuwezesha kupata maji kipindi hiki ambako tunasubiri Mradi wa kutoka Lake Victoria isipokuwa visima. Kwa hiyo naomba sana Wizara ya Fedha izingatie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa fedha 2018/ 2019 tulitengewa fedha kama shilingi milioni 620 kwa ajili ya kujenga visima 30 katika vijiji, tunaomba Wizara mtuwezeshe hilo kwa sababu naanza kutetemeka kidogo kwa kuwa sasa hivi tayari tuko mwezi Mei na bado fedha hazijatoka. Uzuri wetu sisi watu wa Urambo, tuliipa Wakala wa Serikali (DDCA) kazi hii ya kuchimba visima. Kwa hiyo, tutashukuru tukipata hiyo shilingi milioni 620 ili DCCA iweze kuchimba visima 30 kwenye vijiji wananchi waweze kupata maji wakati tunasubiri mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo mjini Urambo kuna shida ya maji sana na mtandao mzima wa maji una changamoto. Katika mwaka huu wa fedha 2018/2019, tuliomba na tukaahidiwa kupata shilingi milioni 429 ili tuchimbe visima Mjini Urambo lakini pia tuweze kurekebisha miundombinu. Tutashukuru sana Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla mkitupa fedha hizo ili tuweze kupata maji kwa njia ya visima wakati tukisubiri mradi mkubwa kutoka Ziwa Viktoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mmojawapo kati ya watu waliopata bahati kwenda Bermuda ambacho ni Kisiwa America Kusini. Jambo ambalo nilijifunza, naomba niliseme hapa, wao wamegundua kwamba nchi yao hawawezi kupata maji mazuri, wakajiwekea wenyewe katika sheria yao kwamba yeyote anayeomba kibali cha kujenga, kwanza wanakagua kama ameweka miundombinu wa kuvuna maji. Mimi niliona ni jambo zuri sana lakini kwetu sisi kwa sababu bado halijawekwa katika sheria na utaratibu wa ujenzi kwamba lazima mtu anapojenga nyumba aweke miundombinu ya kuvuna maji, mimi ningeomba ianzie na shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule zetu nyingi sehemu wanazojengwa maji huwa ni haba, kwa hiyo, utakuta watoto barabarani wanatembea na chupa na vidumu vya maji. Niiombe Serikali kwa sababu ni moja wakashirikiana Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI kuona waweke sharti gani kwa watu wanaojenga shule ili miundombinu ya kukusanya maji iwepo. Mimi nasema inawezekana, kwa sababu bila maji ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Waheshimiwa Wabunge kwa kushirikiana na Mheshimiwa Spika tumeendesha zoezi zuri sana la uchangiaji wa vyoo ili watoto wa kike wapate vyoo vya kuwahifadhi. Pia katika ramani ile ambayo tulipendekeza, inaonesha lazima kuwe na maji na njia pekee ambayo inaweza kutuhakikishia upatikanaji wa maji ni kuweka miundombinu ya ukusanyaji wa maji ya mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono Kamati ya Kilimo, Uvuvi na Maji ambayo kwenye kitabu chake ukurasa 20, wamependekeza kwamba Serikali itilie mkazo suala la uvunaji wa maji ya mvua. Kwa hiyo, ni suala tu la kuongea na sekta husika ili tuone kama wanaweza kuweka kiwe ni kipengele kimojawapo kwamba kabla shule haijafunguliwa au haijajengwa lazima kuwe na ramani ya utaratibu wa ukusanyaji wa maji shuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo, naomba nichomekee hapo hapo, kama wataweka sharti mojawapo la ujenzi wa shule kwamba kuwe na miundombinu ya kuvuna maji, pia naomba nipendekeze kwamba kuwe na utaratibu kwamba kabla shule haijakaguliwa au inapokaguliwa la kwanza kuangaliwa ni suala la vyoo ambapo Waheshimiwa Wabunge wamependekeza ramani nzuri ambayo inawahifadhi watoto wa kike, watoto wenye ulemavu na watoto wote kwa ujumla. Kwa kweli vyoo na maji iwe kama ni sharti mojawapo la kwanza la kuzingatiwa kabla shule haijajegwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji halina ubishi, sisi wanawake ndiyo tunahitaji sana maji kwa sababu baba anapokuja nyumbani anategemea akute maji. Kwa hiyo, nashukuru sana kwamba Wabunge wote tumeungana kuiomba Serikali ione utaratibu ambao unaweza kuiwezesha kupata fedha kutuwezesha sisi Wabunge na wananchi kwa ujumla kupata maji katika maeneo yetu jambo ambalo litakuwa ni ukombozi. Sisi wote tunasema mtu ni afya lakini huwezi kuwa na afya bila kuwa na maji kwa sababu maji hayana mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapo kwa kuishukuru tena Serikali kwa kutuwezesha sisi watu wa Urambo kuingizwa katika Mradi wa Maji kutoka Lake Victoria kama inavyooneshwa kwenye ukurasa wa 88 wa kitabu hiki halafu pia imerudiwa kwenye ukurasa wa 148 kwamba tutapata maji kutoka Lake Victoria. Tunawashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Urambo na tunaomba tu Mheshimiwa Waziri mtakapokuja kujibu hapa basi mtupe matumaini lini tunapata maji kutoka Lake Victoria kama ukombozi wa kudumu au suluhisho la kudumu la upatikanaji wa maji katika Wilaya yetu ya Urambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)