Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema aliyetujalia uzima, aliyenipa uwezo kuwepo Bungeni leo na kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu wake, wanafanya kazi nzuri Mheshimiwa Waziri ni msikivu sana tunampongeza sana anafanya kazi kubwa na kazi nzuri. Pia tumpongeze Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, kwenye Wizara hii siyo kwa Waziri na Katibu peke yake hata wataalam wao wale watu wa Idara ya Maji Vijijini Mkurugenzi na Msaidizi wake wanafanya kazi nzuri, wanatoa ushirikiano wa kutosha huwa nawasumbua wakati mwingine mpaka usiku nikiwa na changamoto za maji kule kwetu Korogwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru sana Serikali, kwa muda mrefu watu wa Korogwe tumekuwa tukiangaika na vibali vya mradi wa Vuga, Mlembule, na mradi wa Lusanga, lakini mwezi wa pili hatimaye tumepata vibali vile na miradi ile tayari taratibu zimeanza manunuzi kwa ajili ya wakandarasi kuendelea na kazi zile, tumesubiri kwa muda mrefu kwa hiyo tunaishukuru sana na kuipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri nikushuku sana kwa ile kazi ya ujenzi wa tenki pale Mombo tulikuwa na changamoto ya mtambo kwa ajili ya kutibu maji, tumeshamaliza michoro, imeshaletwa Wizarani tunaomba mtusaidie ile kazi ifanyike kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana dada yangu Mheshimiwa Mboni, alizungumza kwa uchungu sana kuhusu kero ya maji kule Handeni; na ni kweli Handeni kuna shida kubwa sana ya maji, na miongoni mwa njia za kutatua kero ya maji Handeni ni mradi ule wa HTM, na Wizara ilishafanya mpaka usanifu wa kupanua na kuboresha ule mradi. Sasa ukienda kule Korogwe kuna Kata inaitwa Kata ya Mswaha, ina vijiji vitano, kijiji kimoja kinaitwa Kijiji cha Tabora, ndipo kwenye chanzo cha maji cha mradi huu wa HTM na kuna vijiji vingine vinne Kijiji cha Mswaha Darajani, Mswaha Majengo, Kijiji cha Mafuleta, na Kijiji cha Maulwi Rutuba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji hivi vilifanyia usanifu pia kwamba vitafaidika na mradi huu wa uboeshaji na upanuzi wa mradi huu wa HTM ni muda mrefu wananchi wale wanasubiri Mheshimiwa Waziri tunakuomba sana kazi hii ifanyike na itakapofanyika msiwasahau watu wa Korogwe kwenye Vijiji hivyo maana Kata hiyo ndiyo kilipo chanzo cha maji cha HTM.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule Korogwe kuna eneo linaitwa Bungu, tuliwahi kuwa na mradi wa maji tulipata ufadhili wa watu World Division, tukawa na mradi wa shilingi milioni 969, na ule mradi ulikamika na ulinufaisha vijiji tano, lakini maji yale ni mengi yana uwezo wa kunufaisha vijiji vingine vitatu, Kijiji cha Mlungui, Kijiji cha Kwemshai na Kijiji cha Ngulu. Tunaiomba sana Wizara tuko kwenye maandalizi ya mwisho ya kuleta maombi kwenu ili mtusaidie tuweze kupata fedha za kusambaza na kupeleka maji kwenye maeneo hayo ambayo nimeyataja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa maji wa Mwanga, Same, korogwe, mradi huu umesemwa muda mrefu ni mradi muhimu sana unanufaisha Wilaya za Same, Wilaya ya Mwanga na Wilaya ya Korogwe, nimeona kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri kwenye mwaka wa fedha unaokuja tunasema tumetenga bilioni 29 sijaona kama ndiyo tunakwenda kukamilisha ule mradi au bado tutaendelea kusubiri kwa miaka mingine na awamu nyingine zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa shida ambayo tunaipata watu wa Korogwe ambao na sisi tumesubiri kwa muda mrefu mradi huu sisi ndiyo tuko mwishoni, tuna Vijiji vitano kwenye Kata ya Mkomazi, Kijiji cha Manga Mikocheni, Kijiji cha Manga Mtindilo, Kijiji cha Mkomazi Kijiji cha Bwiko na Kijiji cha Nanyogie. Vinanufaka na mradi huu na sisi ndiyo tuko mwishoni na tunaambiwa kuna bilioni 29, je mradi huu unakwenda kukamilika? Maana sisi watu wa Korogwe ambao ndiyo tuko mwishoni tunanufaika na mradi huu ukiwa umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri ukumbuke kwamba tumeusubiri kwa muda mrefu, na changamoto ya maji kwenye vijiji hivyo ni kubwa sana tunakuomba sana utakapokuja kufanya majumuisho utuambie maana mwanzoni pia kwenye vikao vya maandilizi na utekelezaji wa mradi huu watu wa Korogwe tulikuwa tunahusishwa, lakini baadaye kumekuwa na kama sintofahamu hivi hatujui hata kinachoendelea ni nini. Utakapokuja utuambie ni kweli bado watu wa Korogwe ni wanufaika kwenye mradi huu? Na kama ndivyo matumaini yetu yale lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepeleka Wizarani taarifa ya usanifu wa mradi wa maji wa Kijiji cha Mgwashi na kwa Kibomi tangu mwezi wa tatu, hatujapata taarifa yoyote kwamba tutapa lini kibali. Nilikuwa namuomba sana Mheshimiwa Waziri najua watu ni wasikivu kule Wizarani tusaidie tuweze kupata kibali ili mradi huu angalau ukaanze tutekelezwa kwenye maeneo ya Mgwashi na Kwakibomi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hizi fedha za PBR, sisi ni miongoni ambao tulikuwa tunatumaini kwamba tutanufaika na fedha hizi, lakini kwa mwaka huu wa fedha tulikokuwa nao mpaka sasa hatujapata hizi fedha, na sisi tulikuwa tumelenga kwenda kutatua changamoto za maji kwenye baadhi ya maeneo ndani ya Jimbo letu kwa kwenda kufanya ukarabati mdogo wa vyanzo vya maji. Tulikuwa tunategemea kupata fedha hizi kwa ajili ya ukarabati vyanzo vya maji kule Magoma, tulikuwa tunategemea kupata kwa ajili ya kukarabati chanzo cha maji kule Mazinde, tulikuwa tunategemea kwenda kukarabati chanzo cha maji Kerenge na baadhi ya Vijiji vya Kata ya Mashewa. Lakini mpaka leo hatujapata hizi fedha nimejaribu kuuliza Wizarani sijapata majibu ambayo yamekaa vizuri, naomba sana Mheshimiwa Waziri utusaidie tupate hizi fedha twende tukatekeleze hayo mambo kwenye hayo maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ulikuja Korogwe tulikuomba fedha kwa ajili ya kupeleka maji kwenye eneo tunalojenga Hospitali ya Wilaya na tunashukuru kwamba ulikubali na tuliandika ikaja Wizarani baadaye mkaturudishia tulete mchanganuo tukaandaa, tukaleta mchanganuo Wizarani na ukatuhaidi kutupa shilingi milioni 95.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa bahati mbaya sana maji tuliyokuwa tunataka kuyatumia pale chanzo chake ilikuwa ni maji ya kisima, lakini tumegundua chanzo kikubwa na kizuri cha maji ambacho kitakuwa na maji ya mtiririko kwa ajili ya hospitali, pia kwa ajili ya maeneo na Makuyuni na maeneo ya kwa Sunga Mpirani. Kama utaridhia Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba ulikubali, na ukahaidi kutoa milioni 95 nakuomba sana kwa unyenyekevu najua wewe ni msikivu, wewe ni muungwana sana hebu ukubali tukuletee haya marekebisho ili badala ya kutumia chanzo kile cha kisima tutumie chanzo hiki kingine cha maji ya mtiririko na vijiji vingine vya karibu na maeneo yanayojengwa hospitali na vyenyewe viweze kunufaika na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu Bunge limeanza la bajeti tangu bajeti ya kwanza nilikuwa nataka kuchangia naenda uhamishoni, lakini leo sijaenda uhamishoni nachangia nikiwa kwenye kiti hiki, kwa sababu maji ni jambo muhimu ndiyo maana hata humu unaona kumetulia. Ukisoma vizuri hata kitabu hivi vitabu vya hotuba vya rangi hii nadhani mnanielewa nikisema vya rangi hii kwa mara ya kwanza nimeona hotuba ambayo imegusa vitu tofauti na nyingine utakuta Wizara tatu, Wizara nne hotuba ni hiyo hiyo, lakini leo nimeona hotuba nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tumesema hapa na nimesema Mheshimiwa Waziri kila mahali nasema tunaomba tunaomba niliposoma hutuba yako kwenye kitabu hichi ukurasa wa 106 changamoto ya kwanza unaionesha ni ukosefu wa fedha. Kwa hiyo, pamoja na maombi yote haya ambayo tunayaweka kama hatuna fedha bado changamoto ni kubwa ni miradi hii itakuwa na shida kwenye kutekeleza, yamekuwepo mawazo humu kwamba iongezwe shilingi 50 na wengine wamesema kwenye mafuta, pia iko hofu kwamba inaweza ikasababisha mfumuko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nishauri tunahitaji kweli ongezeko la fedha kwa ajili ya miradi ya maji kwenye nchi yetu. Ukiangalia lengo tulilokuwanalo la kufika upatikanaji wa maji mwaka 2020 na asilimia tuliyokuwa nayo sasa bila kuwa na mkakati madhubuti wa kupata fedha kwa ajili ya miradi ya maji tutapata shida kwenda kufikia lengo letu. Niombe tu kuishauri Serikali wametusikia Waheshimiwa Wabunge hebu ufanyieni kazi huu ushauri wa Wabunge uliotolewa, ungeniambia kwenye mafuta kunakuwa na mfumuko wa bei nikasema bado yako maeneo mengine, kuna maeneo kwenye mawasiliano kuna watumiaji wengi, tunaweza kuangalia namna ya kuongeza huko ili tupate fedha ajili ya kuweza kusaidia kugharamia miradi ya maji, baada ya kusema hayo nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake yote, hotuba yangu kwa ujumla imelenga kwenye maombi, naomba sana maombi yangu myapokee, naomba myafanye kazi naomba muwasaidie watu wa Korogwe ili tuondokane na changamoto hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, kwa asilimia 100. (Makofi)