Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Maji ni hitaji la msingi na ni haki kwa kila mtu, kwa hiyo tunapochachamaa na kudai huduma hii muhimu ya maji tunadai jambo ambalo ni la msingi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na miradi ya maji ambayo inajengwa chini ya kiwango. Mwaka jana wakati tupo kwenye hotuba kama hii, Wabunge wengi walitaka kuazimia Tume huru ya Bunge ili kwenda kuchunguza mingi ya maji iliyojengwa siku za nyuma hasa ile ambayo iko kwenye ule mpango wa WSDP, lakini baadaye Wizara ikasema tuwape nafasi ya mwisho wenyewe waende wakafanye kazi hiyo ili watuletee ripoti. Sijui na sidhani mpaka leo kama ripoti ile imeweza kupatikana. Kwa hiyo naomba Wizara hii itupe taarifa ya wataaam wao walipokwenda kukagua miradi ile, tatizo hasa ni nini ya ujenzi ule kuwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana mimi natokea Karatu, timu hiyo ilikuja Karatu, walipokuja Karatu badala ya kupelekwa kwenye miradi ambayo ina hali mbaya sana, walipelekwa kwenye miradi ambayo ina unafuu mkubwa. Ukipata Daktari Bingwa anakutembelea kwenye hospitali yako nadhani namna bora ni kumpeleka kule kwenye wagonjwa walioko ICU sio kwa wale wagonjwa wa nje wanaokuja na kurudi, lakini wale wataalam kwa baadhi ya maeneo walipelekwa kwenye miradi ambayo walau inafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Miradi ya Vijiji Kumi kila Wilaya, pale Karatu tuna miradi 10 lakini miradi mitano kati ya 10 haifanyi kazi hadi sasa. Ukijumlisha fedha zilizotumika ni zaidi ya shilingi bilioni nne, Mradi wa Matala, Kansay, Buger, Getamock na Mradi wa Endonyawet, miradi hiyo yote haifanyi kazi. Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja Karatu tukamweleza kwenye kikao cha wilaya na aliahidi kupita kwenye miradi hiyo, lakini tangu wakati ule mpaka leo hajaweza kurudi. Jambo hili sisi Viongozi wa Wilaya limetushinda, Viongozi wa Mkoa, Mkuu wa Mkoa ameshakwenda mara kadhaa imemshinda, sasa tunaomba huu mzigo hebu wakaubebe wao. Watu hawa wameiibia Serikali, wakandarasi na wataalam hawa wamewaibia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuombi fedha mpya, tunataka fedha zilizotumika, ziende zikafufuliwe ili wananchi wapate huduma ambayo ilikuwa imekusudiwa. Kwa kweli haipendezi mradi unakaa miaka saba, miaka kumi haufanyi kazi na huku wananchi bado wanahangaika na shida kubwa ya maji iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, niwaombe hili suala la miradi ya Benki ya Dunia ambayo imechakachuliwa kwa sehemu kubwa, tunaomba walivalie njuga, wafike kwenye maeneo hayo ili watusaidie kuwaleta site wale Wakandarasi waliofanya kazi hiyo, wale Wahandisi, Washauri waliosimamia lakini pia wale Wahandisi wa Halmashauri ambao na wenyewe walikuwa na nafasi kwenye kuhakikisha miradi hiyo inafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni suala la vyombo vya watumia maji. Naamini kujenga mradi wa maji kimiundombinu ni jambo moja, lakini jambo la pili ambalo nalo ni muhimu sana ni kuhakikisha miradi ya maji inakuwa endelevu. Kwa maeneo ya mjini tunazo Mamlaka za Maji Mijini, lakini kwa maeneo ya vijijini kwa sehemu kubwa vyombo hivi vya watumia maji ndivyo ambavyo vinasimamia na kuendeleza miradi hii ya maji. Vyombo hivi, vinatambuliwa katika nchi hii. Sera ya Maji ya Mwaka 2002 inavitaja, hata kwenye hotuba ya Waziri vinatajwa, lakini pia Sheria mpya ya Maji Na.5 ya Mwaka 2016 pia imevitaja. Ni vyombo ambavyo tukivisimamia vizuri vinaweza vikapunguza matatizo ya maji kwenye badhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwetu Karatu tuna vyombo vitatu vinavyotoa huduma. Tuna Mamlaka ya Maji ya Mji wa Karatu ambayo imeundwa ina karibu miaka mitano, ambayo inatoa huduma ya maji kwa asilimia 6.7, lakini tuna Bodi ya Wadhamini, chombo ambacho kimeundwa na wananchi, kilichosajiliwa kisheria ambacho kimekuwepo kwa muda wa miaka 20 na ambacho kinatoa huduma kwa zaidi ya asilimia 76 kinaitwa KAVIWASU. Pia tuna watoa huduma wachache, watu binafsi ambao wana visima vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa naomba nieleze kwamba hivi karibuni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, barua hii hapa, ameandika barua kusitisha zoezi la kisheria la kupata wawakilishi wa wananchi ili waweze kusimamia mradi huo wao nilioutaja wa Karatu Villages Waters Supply. Kama kweli tuna nia njema ya kuona miradi ya wananchi inayofanya kazi, mradi wa Karatu ni wa mfano. Ukitaka kuona mradi wa PPP ambao pia wananchi wameusimamia kwa ufanisi mkubwa ni huo mradi wa Karatu lakini Mkurugenzi ameandika barua kusimamisha uchaguzi kwa sababu Bodi iliyokuwepo muda wake umeisha, sasa wanataka kuchagua bodi nyingine lakini Mkurugenzi anasimamisha eti kwa maelekezo kutoka juu. Eti kwa sababu Wizara sasa hivi inatunga kanuni kwa ajili ya hizi sheria mpya, hivi vinahusiana wapi na wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Karatu tuna machungu, Karatu tuna makovu ya matatizo ya maji ya miaka iliyopita. Naomba msiturudishe huko. Inawezekana kwenye jambo hili kuna siasa, lakini siasa inaingia wapi kwenye huduma ya maji. Niseme tu wazi, Mheshimiwa Humphrey Polepole, Katibu Mwenezi wa CCM alikuja Karatu na ndiye aliyetoa maagizo ya kusimamisha uchaguzi huo, inaumiza sana. Inaumiza sana kwa sababu wananchi mradi huo wameuendesha peke yao miaka 20 bila hata kupata ruzuku ya senti moja kutoka Serikalini. Leo zoezi la kisheria ambalo wananchi wako tayari kuendesha mradi wao, linasimamishwa kwa hisia tu za kisiasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache niseme kwamba, mradi huo wakati wadau wa maendeleo pamoja na wananchi wameumaliza na Bodi ilipokabidhiwa miaka 20 iliyopita, walikuwa na mtandao wa bomba wa kilomita 57, leo wana kilomita 421. Wakati huo walipokabidhiwa wana vituo vya umma 37 leo wana 86. Walipokabidhiwa walikuwa na kisima kirefu kimoja leo wana visima saba. Walipokabidhiwa walikuwa na matenki 10 leo wana matenki 23. Walipokabidhiwa walikuwa na private connections sifuri (1) leo wana 2,661. Walipokabidhiwa walikuwa hawana mfumo wa kulipia kabla (prepaid) leo wana vituo karibu 15 vya prepaid na mambo mengine mengi. Ndiyo maana nilisema kama kuna mradi unaweza kuona jinsi wananchi wanavyosimamia miradi yao na kuiendesha ni mradi wa Karatu lakini leo mradi ule unataka kuzimika kwa sababu tu ya hisia ambazo siyo za kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu jambo hili inasemekana limetoka ofisini kwenu Mheshimiwa Waziri, hebu niwaombe mtuache Karatu tuendeshe mradi wetu kwa namna ambayo tunaweza. Wananchi wako tayari, fomu za kugombea wamechukua lakini sasa zoezi limesimama na matokeo yake hata mishahara ya watumishi hawawezi kulipa kwa sababu wale watendaji wamebaki wenyewe, wale wawakilishi wa wananchi kwa maana ya Wajumbe wa Bodi hawapo. Leo hata madeni ya maduka ya vifaa hawawezi kulipa kwa sababu ya kusimama kwa zoezi hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa vile inasemekana jambo hili limeanzia kwenu naomba mruhusu wananchi wa Karatu na vijiji vya jirani waweke viongozi wao. Kama kuna matatizo mengine, hata muende mkautembelee na mtaona, Naibu Waziri nashukuru ulikuja Karatu lakini hata ulivuyokuja, hata kuambiwa kwamba kuna mradi unahudumia asilimia 76 ya maji katika Mji wa Karatu na vijiji vya jirani haukuambiwa. Kwa hiyo, ujue katika sura hiyo jinsi ambavyo kuna tofauti na harufu ya kisiasa kwenye jambo hili. Kwa hiyo, naomba kadri itakavyowezekana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)