Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ametujalia uzima na sisi wote leo tuko hapa tukiwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuru Wizara kwa kutupatia fedha za maji. Mwaka 2018 tulitengewa shilingi bilioni 1,400, tumepata shilingi milioni 960, tunazungumzia takribani asilimia 67. Nawashukuru sana. Wakati nikishukuru, nikumbushe tu kwamba kuna kiporo cha shilingi milioni 461, tunategemea fedha hizi zitapatikana ndani ya kipindi cha mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nikisema hayo vilevile natambua katika bajeti ya mwaka kesho tumepangiwa shilingi bilioni 1,139 kwa ajili ya miradi ya kule Mbuta, Mwakijembe, miradi miwili ile ambayo ili ikamilike tunahitaji shilingi bilioni 2,300. Hii maana yake nini? Maana yake tuna upungufu wa shilingi bilioni 1,160 ili miradi hiyo iweze kukamilika. Kwa hiyo, naiomba Serikali ifanye kazi kuhakikisha kwamba fedha hizi zinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nizungumzie tatizo la maji katika nchi yetu kwa ujumla. Nilikuwa nasoma taarifa ya World Bank, inaitwa Reaching for SDG The Untapped Potential of Tanzania Water Supply Sanitation and Hygine Sector ya mwaka 2018. Taarifa inatuambia kwamba takribani Watanzania milioni 20 hawapati maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposikia jambo hili, siyo jambo zuri hata kidogo. Kwa vigezo vyovyote vile, haiwezekani kama nchi tukaona Watanzania milioni 20 hawapati maji safi na salama halafu tukaona ni jambo la kawaida, lazima tuchukue hatua. Hapa ndipo linapokuja suala hili sasa kwamba lazima tutafute maarifa mapya ya kuhakikisha kwamba kama Taifa tunatoka hapa tulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili liliazimia, moja ya maarifa iliyotumia Bunge ni kuongeza fedha za Mfuko wa Maji. Najua wenzetu wapo wanaosema kwamba tukiongeza kule tunaweza ku-trigger inflation, lakini statistics zinatuonesha kwamba kwa kipindi cha miaka kumi iliyopita tumeweza ku- control inflation. Kwa mwaka huu ndiyo tumeweza kupata kiwango kikubwa sana cha inflation iliyochangiwa na Sekta ya Usafirishaji, maana yake mafuta yako humu. Wakati tumefikiwa kiwango hicho, bado inflation yetu ni asilimia 3.1. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake nini? Hii maana yake tusijifiche kwenye kichaka cha inflation, bado tuna room ambayo tunaweza kufanya tukatumia Sekta hii Mafuta kupata fedha za maji na hatimaye tukaondoa tatizo hili kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili la maji ni kubwa vilevile Mkinga; na hili nimekuwa nikilisema mara kwa mara. Mkinga imegawanyika katika maeneo mawili, kuna eneo la milima na ukanda wa Pwani. Maji yanayotumika katika Mji wa Tanga, chanzo chake ni Mkinga, katika Kata ya Bosha na katika Kata ya Mhinduru. Tangu kuumbwa kwa dunia watu wa Kata hizi mbili hawajawahi kuona maji ya bomba. Hii haiwezi kuwa sawa hata kidogo. Watu wale wamejitahidi kuhakikisha wanalinda vyanzo vya maji. Maji yale yananywewa Tanga Mjini, wao hawana huduma ya maji. Haiwezi kuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikileta maombi, Halmashauri tumekuwa tukileta maombi kwamba tujenge miradi ya maji kwenye maeneo yale, tumekuwa hatupati majibu. Mwaka huu tumeleta maombi, tunahitaji shilingi bilioni nane ili maeneo katika Kata ya Mhinduru, eneo la kwa Mtiri, Churwa, Muheza, Mhinduro, Bamba, Mazengero, Kichangani na Segoma na vile vile maeneo ya Bosha, Kuze, Kibago, Bosha, Kwamtindi na Buzi Kafishe yaweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wapeni maji watu hawa, ndiyo wanaotunza vyanzo vya maji vinapeleka maji Tanga, ndiyo wanaotunza vyanzo vya maji vinavyopeleka maji sasa Muheza wao hawana maji safi na salama, haiwezi kuwa sawa hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili ni ukanda wa Pwani. Ukanda wa Pwani hatuna Mito, tungetegemea tupate maji kwa kuchimba visima, lakini kila visima tunavyochimba, chumvi inakuwa ni nyingi mno, kwa hiyo, maji yale hayafai kwa matumizi ya binadamu. Sasa wakati ikiwa hivyo nataka mwelewe kwamba Watanzania wenzenu wanakunywa maji yasiyo safi na salama kwa sababu tu tumeshindwa kuwapelekea maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, alikuja Mheshimiwa Kamwelwe akawaahidi watu wale kwamba suluhisho la tatizo lile ni kutoa maji Mto Zigi kuyapeleka kule. Maji yale leo hayajapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule uliambiwa utengenezwe ili wananchi wa Mkinga wapate maji, nimeambiwa Wizara ilitoa tangazo la mradi ule, amepatikana Mhandisi mwelekezi, lakini mpaka leo hakuna kinachoendelea. Tangu mwezi wa Kumi nasikia Mhandisi amepatikana, lakini kuna majadiliano yasiyoisha juu ya mradi ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana, nimeangalia vitabu hivi vya bajeti, mradi ule haupo. Hivi mnataka watu wa Mkinga tukapate wapi maji? Mheshimiwa Waziri alikuja mpaka Horohoro akaiona kadhia ile, watu wetu wanaenda kuchota maji Kenya. Tuondoleeni aibu ile. Aliwaahidi watu wale kwamba tutapata mradi wa maji wa quick-win. Aliagiza watu wa Tanga, UWASA walete mapendekezo; nimeambiwa mapendekezo yako Wizarani kwake, tunaomba fedha hizo ili tatizo lile liweze kuondolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anajua, amefika Mkinga, Makao Makuu ya Wilaya hayana maji. Hivi tunakuwaje na Wilaya ambayo haina maji? Tuna mradi pale wa ubabaishaji tu, tunatoa maji kutoka kwenye Kijiji jirani ndiyo ki-save Makao Makuu ya Wilaya. Hii haiwezi kuwa sawa. Tusaidieni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisema jambo hili tangu Mzee Maghembe ni Waziri, ameondoka Mheshimiwa Prof. Maghembe wamekuja wengine, sasa uko wewe, imani ni yangu ni kwamba jambo hili litapatiwa ufumbuzi. Tusaidieni tuweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taarifa ya Mheshimiwa Waziri, Wilaya ya Mkinga ndiyo eneo lenye Ukanda mkubwa wa bahari kuliko Wilaya nyingine zote katika Mkoa wa Tanga. Kwa hiyo, tuna potential ya ujenzi wa mahoteli katika ukanda ule, lakini tunashindwa kujenga mahoteli kwa sababu hatuna maji. Mahoteli yanajengwa upande wa pili wa nchi ya Kenya, upande wa Mombasa, sisi tunaangalia. Nawasihi sana, tusaidieni tupate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakusudia kujenga kiwanda kikubwa kabisa cha uzalishaji wa cement katika nchi hii. Mapato yanayotegemewa pale ni shilingi bilioni 450 kwa mwezi. Kiwanda kile kitafanyaje kazi tusipokuwa na maji? Kiwanda kile kinategemewa kuvutia viwanda vingine 11 pale Mtimbwani, tunajengaje viwanda vile kama hatuna maji?

Mheshimiwa Waziri, tusaidieni, watu wa Mkinga wana shida ya maji, tupeni maji ili tuweze kupiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, ahsante sana. (Makofi)