Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii muhimu ya kuchangia Wizara ya Maji. Naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, zipo hoja nyingi ambazo zinaendelea kutolewa, lakini leo ntajikita kwenye hoja mbili, hoja ya kwanza ntatoa sababu za kuwaondolea wasiwasi wale wanaofikiri kwamba tukiongeza shilingi 50 kwenye mafuta petroli na dizeli kwamba inaweza ikasababisha mfumuko wa bei kuongezeka. Na jambo la pili ntakalozungumzia kwa ufupi, ntazungumzia hoja inayohusiana na Stiegler’s Gorge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na hoja ya kwanza; wale ambao wanafikiri tukiongeza shilingi 50 kwenye lita ya mafuta ya dezeli au ya petroli itaongeza mfumuko wa bei, nataka nitoe sababu zifuatazo kuwaondolea wasiwasi kwamba hilo halitatokea. Sababu ya kwanza hii shilingi 100 au shilingi 50 ambayo tunataka iwe shilingi 100 sasa, hii kodi kitaalam tunaita specific sio Ad valorem, na mchumi yeyote duniani ukimuuliza atakwambia kama ni specific maana yake haibadilikibadiliki, kama thamani ya kitu fulani inapanda au kushuka kodi yenyewe haibadiliki.

Mheshimiwa Spika, sasa hii tunasema shilingi 100, hii shilingi 100 bei ya dunia huko ya mafuta ipande ishuke, bei ya mafuta hapa Tanzania ipande ishuke, hiyo haibadilishi hiyo shilingi mia. Kwa hiyo, ntapenda yule atakayekuja kusema itabadilika anieleze yeye uchumi anaousema alisomea wapi na anatumia reference ya wataalam gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili, mfumuko wetu tunaouzungumza saa hizi ni wastani wa asilimia 3.1 mpaka Machi kwa takwimu za BOT, lakini BOT lengo lake ambalo wameliweka ni kwamba mfumuko wa bei usizidi asilimia tano, hilo ndilo lengo la BOT. Sasa kama lengo la BOT ambalo ndiyo lengo la Serikali pia ni asilimia tano tusivuke lakini saa hizi mfumuko wa bei ni asilimia 3.1, huu wasiwasi unatoka wapi wa kusema huu mfumuko wa bei utapanda. Ukipanda acha upande tu, sana sana ukipanda utaenda mpaka asilimia 3.5, itakwenda nne, hata ukifika tano uache tu ufike tano, kwani tatizo ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu ya tatu ni kwamba ndani ya Afrika Mashariki tumekubaliana kitu kinaitwa convergence rate, tumlichokubaliana ndani ya Afrika Mashariki ni kwamba nchi zote za Afrika Mashariki zihakikishe mifumuko yao ya bei haizidi asilimia nane. Sasa kama hiyo ndiyo ya Afrika Mashariki tuliyokubaliana tusizidi asilimia nane, sisi tuko asilimia 3.1, huu wasiwasi unatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo sababu nyingi kwa nini mfumuko wa bei unaweza ukapanda, unaweza ukapanda ama kwa sababu ya kuongezeka sana kwa aggregate demand au unaweza ukapanda kwa sababu ya cost push, gharama zinaongezeka, lakini hivi kama unasema unaweza ukapanda kwa aggregate demand ikapanda maana yake ni nini; maana yake ni kwamba watu wanakuwa na disposable income kubwa, watu wakiwa na disposable income kubwa kipato kikipanda sana wanaweza wakawa na nia ya kutumia sana.

Sasa unapoongeza kodi kwenye mafuta hauongezi disposable income bali unalenga kupunguza disposable income, sasa wasiwasi huu unatoa wapi kama uchumi hivyo ndivyo unavyotueleza na ndivyo ulivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine, EWURA ni chombo ambacho kinafanya kazi nzuri. Mara kwa mara wamekuwa wakitoa takwimu na wanachapisha kwenye magazeti yote, na tunasoma tunaona, na mara nyingi saa nyingine kulingana na mwenendo wa bei duniani wanasema sasa cape itapanda wanaweka cape inapanda kidogo; saa nyingine shilingi 50, saa nyingine 100 saa nyingine inashuka, lakini siku zote EWURA walipopandisha hiyo mfumuko wa bei haukupanda kwa sababu mafuta yamepanda kwa shilingi 50 au shilingi 100. Hata waliposhusha mfumuko wa bei haukushuka kwa sababu wameshusha, kwa maana hiyo kuna vitu vingine vya kuangalia vinavyoweza kusababisha mfumuko wa bei upande au usishuke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine kwa nini nina uhakika haitatokea kama tunavyofikiri; mfumuko wetu wa bei takwimu zinaonesha unachangiwa zaidi na chakula. Sehemu kubwa tunayoangalia ni chakula, sasa kama takwimu tulizonazo kila siku tunaambiwa tuna surplus ya uzalishaji wa chakula ndani ya nchi, wasiwasi huo unatoka wapi tena ya kwamba gharama hizi zitapanda tukiongeza? Kwa sababu sehemu ya kuangalia kwa makini na kwa wasiwasi ni sehemu tu ya ule mfumuko wa chakula usije ukapanda.

Mheshimiwa Spika, wachumi huwa wanaangalia mambo kwa macho mengi, lakini naomba niwaambie sio siku zote kwamba mfumuko wa bei ni jambo baya, hata mfumuko wa bei ukipanda kidogo si jambo baya, na mfumuko wa bei kupanda kwenye uchumi unatakiwa. Tatizo ni watu waliosoma vitabu vile vinavyowafundisha tu kwamba mfumuko wa bei ni mbaya, si kweli, mfumuko wa bei na wenyewe unatakiwa kwenye uchumi kwa sababu ukiporomoka zaidi, ukiwa negative, ni tatizo pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niliseme la mwisho; mfumuko wa bei pia unaangalia na interest rates. Kinachotakiwa siku zote mfumuko wa bei usiwe juu ya interest rates. Average ya interest Tanzania ni asilimia 8.3; sasa huu wasiwasi wa mfumuko wa bei unatoka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie tu kwa ufupi kuhusu Stiegler’s Gorge; ni mradi mzuri sana, lakini mnakumbuka tulikuwa tuna Sheria Na. 5 ya mwaka 1975 ambayo tuliifuta nadhani humu Bungeni kwa sababu tulifuta ile Sheria ya RUBADA, sasa Stiegler’s Gorge ni mradi mzuri na pale tutaweka trilioni 6.3.

Mheshimiwa Spika, ningeomba itungwe sheria ya kulinda mradi ule kwa sababu bila kuwa na sheria maalum ya kulinda ile Stiegler’s Gorge kwa maana ya kulinda chanzo cha maji, tusipokuwa makini tutawekeza hela nyingi halafu baada ya muda maji hayatakuwepo. Kuna sababu ya kuja na sheria maalum ya kulinda ule mradi, ya kulinda vyanzo vya maji. Hili jambo tunaweza tukafikiri si muhimu lakini nadhani lazima tuanze kufikiria sasa na lazima tuchunge sheria hiyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)