Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya kuchangia leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Serikali kwa kazi nzuri inayofanya, vile vile niwapongeze Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yake ya wataalam wote kwa kazi nzuri wanayofanya. Pia niishukuru Serikali kwa kukubali kuanzishwa kwa Wakala wa Maji RUWASA yaani chombo ambacho kitakuja kusaidia na kuondoa kero zote ya maji, tunaamini hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu kwenye RUWASA ni kuwa na chanzo cha uhakika cha mapato ambapo itakuwa inatekeleza miradi. Huku kote tulikuwa tunalalamika kwamba miradi inasimamiwa vibaya, miradi imesanifiwa vibaya naamini RUWASA wakianza, wataanza na wataalam waliobobea wataalam wazuri na kutakuwa na usimamizi mzuri. Kwa hiyo RUWASA tunaamini itakuwa sawa na REA kwa upande wa maji. REA imepata mafanikio makubwa kutokana na usimamizi mzuri, lakini pia upatikanaji wa fedha wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, leo hii tumepata Sh.50 ambayo tulitenga kama Bunge kwa ajili ya kwenda kwenye Mfuko wa Maji. Kwa sehemu kubwa bilioni 106 ambayo ni sawa na asilimia 67 ya fedha iliyotakiwa kwenda ya bilioni 158 ndiyo fedha ya Mfuko wa Maji. Fedha ya bajeti ya kawaida ni bilioni 333, bilioni 443 ni asilimia 17 tu iliyoenda yaani bilioni 43 ndiyo zimeenda. Sasa ukizijumlisha zile zote mbili ya Mfuko wa Maji iliyoenda na bajeti ya kawaida iliyoenda, bado haijafikia fedha zote ingekuwa imepatikana asilimia 100 ya Mfuko wa Maji ambayo ni ring fenced. Sasa tunapoomba iongezwe shilingi 50 iwe shilingi 100 au tutafute na vyanzo vingine iwe ni kwa kutokana na mitandao yaani kutokana na DART au EWURA au vyanzo vingine zikipatikana bilioni 150 nyingine ya ziada itakuwa tunapata karibu bilioni 300 na ndiyo fedha zote zilizoenda leo kwenye miradi yote ya maji ya fedha ya ndani, ya nje yote jumla imeenda bilioni 343 ambayo ni asilimia 51 tu ya fedha iliyotengwa kwa ujumla wake. Kwa hiyo sehemu kubwa ya hii fedha ni huu Mfuko wa Maji lakini pia Mfuko wa Maji unapeleka maji mijini pamoja na vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni vizuri tukaboresha Mfuko huu ukapatiwa, tusiogope kuweka hata hiyo ya mafuta watu ambao wanasema italeta inflation. Kipindi hicho bei ya mafuta imeshuka mpaka Sh.1,400, hakuna nauli iliyoshuka, hakuna bidhaa iliyoshuka wala hakuna kodi ya ziada, walikusanya kutoka kwa wafanyabiashara waliopata super profit kutokana na hiyo bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mfuko huu wa Maji unapeleka maji mjini na pamoja na vijijini. Ni vizuri tukaboresha mfuko huu, tusiogope kuweka tozo kwenye mafuta ambapo watu wanasema italeta inflation. Kipindi bei ya mafuta yameshuka mpaka 1,400 hakuna nauli au bidhaa iliyoshuka bei wala hakuna kodi ya ziada mlikusanya kutoka kwa wafanyabiashara waliopata super profit kutokana na bei hiyo. Sisi kama Wabunge tutawaelimisha Watanzania kwamba tumefanya hivyo ili wapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni muhimu sana ni suala la uvunaji wa maji ya mvua na mito ili tuweze kuyatumia vizuri. Kwenye hilo la uvunaji wa maji tulishapitisha sheria kwamba majengo yote yanayojengwa mjini na sehemu nyingine kama huna mfumo wa kuvuna maji basi usipewe kibali cha kujenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia huko tunapopoteza maji mengi kwenye mito na maji ya mvua, Serikali iondoe kodi kwenye mitambo ya kuchimba maji na kutengeza mabwawa. Siyo lazima kila kitu kifanywe na Serikali mitambo ikiwa ya bei nafuu wananchi wa kawaida (private sector) itawasaidia kujenga mabwawa kwa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaposema tumtue mwanamke ndoo kichwani ni vizuri Serikali ikaondoa pia kodi kwenye solar pumps. Leo hii miradi mingi ya maji ambayo inatumia diesel au umeme, wananchi vijijini wanashindwa kulipa bili tungetumia solar pumps. Solar pumps ukileta leo ina kodi lakini solar pump hiyo hiyo ukiileta kwa njia ya irrigation haina kodi, ni controversial. Anayetaka kuleta pumps kwa ajili ya umwagiliaji haina kodi ila ukileta kwa ajili ya matumizi ya kawaida ina kodi. Ni vizuri Serikali ikaweka msimamo ikaondoa kodi jumla ili hata yule mwananchi wa kijijini pump hiyo imsukumie maji mita 400 sawa na yule wa mjini inawezekana ikidhamiria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hizi mashine za kuchuja maji (water purifiers? Mkiondoa kodi kwenye water purifiers bajeti ina maana tunayotumia zaidi ya shilingi bilioni 45 ya kutibu magonjwa ambayo yanatokana na maji hiyo pesa tungeweza kuitumia kupata maji safi na salama, ni bora kukinga kuliko kutibu. Kwa hiyo, tungeweza huku kuondoa kodi ndiyo utapoteza kidogo lakini ile shilingi bilioni 45 unayopeleka kwenye afya utaweza kuiokoa na wengi wanaopata shida hiyo ni watu wanoishi vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye mitambo ya kuchimba maji, nchi zote za Afrika Mashariki hazina kodi isipokuwa Tanzania. Kwa wale wakandarasi wakubwa ambao wanaleta vifaa vya kuchimba maji pamoja na Drilling and Dam Construction Agency wote wanapata msamaha wa kodi lakini mwananchi wa kawaida akitaka kuleta mashine yake moja hata kama ni mtumba bado anatozwa kodi ndiyo maana gharama za uchimbaji maji zimekuwa kubwa na uvunaji wa maji umekuwa mgumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo Wakala wa Maji katika maeneo mbalimbali katika wilaya ambazo zina Bodi ni vema tungeziunganisha. Kwa mfano, Bodi moja inaweza kuhudumia wilaya tatu, nne hata mkoa mmoja kwa sababu ndiyo tutapata ufanisi kuliko kila kata na tarafa kuwa na Bodi yake ili kupunguza gharama za uendeshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri tukajipanga na naamini tukijipanga vizuri haya yote ambayo tunayazungumza tutafanikiwa. Maeneo mengi ambapo mashine zinatumia diesel au umeme tufunge solar na hasa katika taasisi mbalimbali za Serikali. Tukiweza mifumo hiyo gharama ya uendeshaji itakuwa ndogo na pia upatikanaji wa maji ni mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haya maji tusipoyavuna ndiyo yanakwenda kuharibu miundombinu ya barabara na reli. Tukiweza kuvuna maji hayo na tukayatumia vizuri tutapata maji ya kunywa, ya umwagiliaji na mabwawa ya kufugia samaki na pia tutaweza kuzalisha zaidi hata maji ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa tunalopata uzalishaji wetu unakuwa mdogo hata upande wa umwagiliaji kutokana na kwamba hatuna vifaa vya kuchimbia mabwawa haya. Ondoeni hiyo kodi kidogo wenye kustahili kupata msamaha tayari wanapata ni hao wachache wachache ndiyo hawapati. Kwa hiyo, mngeruhusu hata kwa private sector pia maana itaweza kusaidiana na Serikali katika suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna tozo mbalimbali ambazo zinachajiwa na Mabonde kwa watu ambao wanatumia maji. Ni vizuri tukaangalia zile chaji katika Mabonde yote bei zifanane. Ni vizuri tukawezesha haya Mabonde zikasaidia upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine ambao naomba Serikali izingatie, leo hii kwa sehemu kubwa tumeanza kutumia maji ya ardhini lakini hatujawekeza hata shilingi moja wala hatuna asilimia hata moja ambayo inaenda kwenye kutunza vyanzo vya maji na maeneo ya catchment (vidaka maji) ambavyo vita-recharge aquifer za kule chini. Tusipo-recharge zile aquifer baada ya muda hata hivi visima ambavyo leo tunapata maji kwa mita 80 mpaka 100 tutakuja kujikuta tunatafuta maji kwa mita 200 au 300 ambapo hatutakuwa na uwezo wa kutoa hayo maji huko chini. Kwa hiyo, suala la mazingira nashauri Serikali kwenye kila mradi ambao tunaanzisha angalau asilimia moja ya fedha yote mradi iende kwenye kutunza mazingira, kuboresha vyanzo vya maji na vidaka maji (catchment area) ili tuweze ku-recharge aquifer za huko chini ili tuweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Serikali ni moja ingeangalia bajeti tunayotumia upande wa afya kutibu magonjwa yatokanayo na ukosefu wa maji lakini vifo vinavyotokea kwa kutumia maji machafu na ambayo siyo salama, hayo tungeweza kuepuka kama tutaondoa baadhi ya kodi. Najua Serikali inasita kuondoa hizi kodi kwenye water purifier kwa sababu tutakosa kodi kwenye viwanda zinavyouza maji ya chupa lakini ni vizuri tukose kodi hiyo afya ya Watanzania iwe salama haswa huko vijijini ambapo sehemu kubwa tunakosa maji. Tukiboresha huduma za maji, umeme kama inavyoenda sasa hivi na miundombinu huko vijijini hakuna mtu yuko tayari kukaa mjini kwani maisha ya vijijini ni mazuri. Tukiboresha huko vijijini watu hawatarundikana mijini na kukosa ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiendelea kuboresha huduma mbalimbali huko vijijini na maji ni uhai na maji ndiyo maisha, kwa hiyo, kilimo mifugo, uvuvi haya yote tunaweza tukafanikiwa kama Wizara hii ya maji itashirikiana na kuratibu masuala mbalimbali ya namna ya kuboresha miundombinu ya maji kwa njia zote, iwe ni uvunaji wa maji na kusimamia. Pia Kamati ya Bajeti na Wizara ya Fedha zikae pamoja ili kuangalia na kuondoa baadhi ya hizi kodi ambazo zitakuwa ni chache sana. Mimi naamini kwa data ambazo tunazo ni kodi kidogo sana ambazo tutapoteza kutokana na msamaha tutakaotoa ambapo multiply effect yake hii mitambo yote ikiletwa kwa bei nafuu watu wengi sana watachimba maji wenyewe na itaisaidia Serikali maana siyo lazima kila kitu kifanywe na Serikali. Kwa hiyo, dhana nzima ya PPP (Public Private Partnership) tutakuwa tumeifikia kama private sector na Serikali watashirikiana kufanya jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la maji kama ilivyo Babati Mjini ndiyo hivyo hivyo ilivyo katika wilaya zote Tanzania. Hakuna sehemu yenye nafuu, iwe mjini au vijijini kote kuna tatizo la kubwa la maji. Hakuna mahali hata huko mijini unaweza kufungua bomba la maji ukanywa yale maji bila uhakika kama ni safi au salama kwa sababu upatikanaji wa maji ni jambo moja lakini maji safi na salama ni jambo lingine. Kwa hiyo, ni muhimu tupunguze bajeti ya kwenye matibabu turudishe huku kwenye maji hata namna ya kutibu maji ili Watanzania wapate maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika Serikali hii ni sikivu huu ushauri ambao tumeutoa kwa muda wote huu mtauzingatia vizuri na haswa hii ya kuongeza bajeti ya Mfuko wa Maji ili iweze kufika agalau shilingi bilioni 350 maana pesa yote iliyoenda kwa ujumla wake ni shilingi bilioni 343. Kwa hiyo, ingekuwa tumeongeza mwaka jana au mwaka juzi badala ya shilingi 50 iwe 100 ungekuta pesa yote asilimia mia moja ingetokana na huo Mfuko wa Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tujue hii miradi mingine, iwe ni mradi wa zile fedha za Exim Bank ya India au fedha nyingine tunayopata kutoka kwa wafadhili mbalimbali hailengi Watanzania wote bali inaenda kwenye specific project. Kama ni miradi ya miji 28, kama ni ule Mradi wa Ziwa Victoria yaani ni miradi ambayo imetengwa na imechaguliwa, je, sisi ambao hatuko kwenye hiyo miradi tunapata wapi hiyo bajeti na ukiangalia ni shilingi bilioni 41 tu ndiyo imeenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni lazima muweke utofauti kati maji mjini na maji vijijini. Percent kubwa ya Watanzania wanakaa vijijini, kwa hiyo, asilimia kubwa ya fedha inatakiwa kwenda vijijini. Ni sawa na hii ya TANROADS na TARURA ilivyowekwa kwamba asilimia 70 ni ya TANROADS na asilimia 30 ni TARURA, hapa pia kwenye huu Mfuko wa Maji asilimia 20 ndiyo iende mjini na asilimia 80 iende kuwasaidia Watanzania wanaoishi vijijini kwa sababu huko ndiko kwenye shida kubwa ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho tutumie E-water. Mfumo wa E-water itasaidia maji kupotea na ni eneo ambapo Serikali itaweza kukusanya mapato yake kabla. Hata kama ni zile Kamati za Maji zinazosimamia gharama ya usimamizi wa maji inakuwa ndogo, Serikali itaendelea kupata unafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuendelee kuboresha vyuo vyetu ambavyo vinafundisha hawa wataalam wa maji na naamini kabisa RUWASA ndiyo itakuja kuwa mkombozi wa sekta ya maji Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)