Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi jioni hii kuchangia hoja ya Wizara ya Maji. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kuniwezesha kusimama, lakini nitakuwa sina fadhila niwashukuru wadau walionisaidia Jimbo la Tunduru Kusini kwa kuwataja kuchimba vya maji, nikianzia na Help for Under Reserved Community ambao wamechimba visima 74 vya maji virefu kwa gharama ya kila kisima shilingi 650,000 kitu ambacho ni kikubwa kwetu gharama ya visima vinaeleweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba niwashukuru Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Masasi, kwa kupitia Mradi wa CHIP wao wamechimba visima virefu vya maji 24 ambavyo vinawasaidia wananchi wangu kuweza kupata maji salama. Tatu, nawashukuru Taasisi za Kidini za Firdaus na Istiqama wao wamechimba visima 60 kwenye Jimbo langu bure bila hata senti tano. Kwa hiyo nawashukuru sana wamesaidia kuondoa kero ya maji kwa asilimia kubwa katika maeneo yangu. Kwa hiyo ukiangalia katika Jimbo langu, hawa wadau wamechimba visima zaidi ya 200 ambavyo vimesaidia kupunguza kero ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda moja kwa moja kwenye hoja, naomba nimshukuru sana Waziri. Waziri pekee aliyekanyaga kwenye Jimbo langu, kaenda kwenye Mradi wa Mtina na kwenye mradi wa Mbesa. Mradi wa Mtina alitoa maagizo, mradi ule unaendelea vizuri kidogo, lakini kuna matatizo mawili, matatu ambayo yametokana na kutokuelewana kati ya Mkandarasi na Mhandisi wa Maji. Katika mchoro wa ule mradi ulionesha kwamba watatumia solar panel 16 na kutumia battery 32. Ushauri wa Mkandarasi alishauri kwamba tutoe battery 32, wanunue panel 16 jumla ziwe 32 ambazo zitakuwa na uwezo sawa na kuwa na battery 32 ili waweze kusukuma maji. Matokeo yake Mhandisi alivyokataa imeonekana maji hayapandi ipasavyo kwa hiyo wakati wa kifuku kama sasa wananchi wale hawapati maji. Kwa hiyo tunaomba Wizara iingilie kati ili yule Mkandarasi aruhusiwe kununua panel zingine 16 ili maji yaweze kupatikana kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Waziri alivyokuja Mbesa alitoa ahadi ya kuchimba kisima kirefu kimoja, kile kisima mpaka leo hakijachimbwa. Naomba sana afuatilie ile ahadi yake iweze kutekelezeka wananchi wa Mbesa pamoja na kuwa watu wengi sana lakini wana shida kubwa ya maji. Maji Mbesa ni tatizo kubwa sana, Waziri mwenyewe amefika, Mradi ule wa Benki ya Dunia mpaka leo maji hayafiki kwenye lile tenki kubwa, limekuwa ni tatizo kubwa sana. Hata feasibility study iliyofanyika maji yanaishia kwenye tenki na pesa kwa ajili ya kugawanya maji kwenye vijiji bado haijaweza kupatikana. Kwa hiyo naomba Waziri afuatilie ile ahadi yake bado haijatekelezwa na wananchi wanaendelea kupata shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine amblo napenda nilizungumzie ni suala la wafanyakazi wa Idara ya Maji, kwa upande wa Tunduru ina shida kubwa sana. Mwaka jana mwaka wa fedha 2017/2018, tulipata fedha kwa ajili ya kukarabati visima vya DANIDA. Vile visima vya DANIDA vingi vimejengwa miaka ya 80 na 90 na ndivyo vinavyowasaidia karibu maeneo mengi ya Jimbo la Tunduru Kusini, lakini kutokana na ongezeko la watu vile visima vimeshindwa kutosheleza mahitaji ya watu na vimezeeka. Mwaka jana tulipata fedha kwa ajili ya kukarabati visima 25, kwa milioni tatu kila kisima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya tatizo la wataalam mpaka leo vile visima vyote, walinunua vifaa lakini havifanyi kazi. Vifaa vimenunuliwa, wamekwenda kuvifunga, naamini kutokana na ujuzi na namna fulani ilivyofanyika vile visima mpaka leo havitoi maji pesa imeondoka. Kwa hiyo tuna tatizo kubwa la watumishi katika idara yetu hasa Mhandisi nina mashaka naye kwa sababu miradi mingi ameshindwa kuisimamia. Hata hawa wahisani niliokuwa nawashukuru walikuwa na mkataba na halmashauri kwa ajili ya kusimamia, watoe gari, watoe mafuta, watoe mfanyakazi, lakini wameshindwa kufanya hivyo, tumekaa vikao mara chungu nzima, lakini imeshindikana. Mpaka leo bado anaendelea kufanya kazi halmashauri kwa upande wa Idara ya Maji wameshindwa kusimamia. Kwa hiyo naomba kwa kuwa Idara ya Maji sasa iko chini ya Mheshimiwa Waziri, awasiliane na huyu Mhandisi, kwa kweli ni kero, ni shida, ameshindwa kusimamia kutekeleza miradi ya maji katika Jimbo la Tunduru Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda sana kuliongelea ni suala la maji kwa vile vijiji vilivyopo kandokando ya Mto Ruvuma. Kuna vijiji takriban 10, kuna Vijiji vya Amani, Mkalachani, Misechela, Liwanga, Mkapunda na Makande, vyote hivi vipo pembezeni mwa Mto Ruvuma, lakini hawa watu wana shida kubwa sana ya maji, maji yako kilomita nne, tatu, tano. Kwa hiyo hawana visima vya maji, wanategemea kuchota maji mtoni, mara nyingi watu wanapata shida sana wanakumbana na mamba kule watoto wanakwenda na maji, wanakufa na maji kutokana na shida ya maji. Naomba kama Serikali yetu inajali watu wetu kama tunavyozungumza kila siku basi tuanzishe mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma kwa ajili ya hivi vijiji vilivyopo pembezoni mwa Mto Ruvuma ili hili kero ya maji iweze kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, sio kwa umuhimu, naomba kwenye vile vijiji vilivyokuwa kwenye miradi ya Benki ya Dunia kwa mfano Mchoteka na Namasakata. Vile vijiji vilionekana havina vyanzo vizuri vya maji kulingana na utafiti, lakini lakini ukweli vyanzo vipo. Tunaomba basi ule mradi urudi tena ili vile vijiji viweze kupata maji ya kutosha kwa sababu Mchoteka peke yake ina vijiji vine, umati ulioko pale ni zaidi ya watu 8,000, wanategemea visima vinne tu ambavyo kila kijiji ina kisima kimoja. Naomba sana Mheshimiwa Waziri kwa kuwa tulikuwa na nia nzuri ya kuweka Mradi pale wa Benki ya Dunia, lakini utafiti ulifanywa shaghalabaghala, haukuweza kutosheleza mahitaji yale, naamini kuna andiko lilipelekwa Ofisini kwa Mheshimiwa Waziri tangu 2017 kutokana na utafiti uliofanyika na Mhandisi wa Maji aliyekuwepo kipindi kile, lakini mpaka leo lile andiko halijafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na andiko hilo kuna andiko la Namasakata, nacho Namasakata ni kijiji kikubwa sana, nacho tulikuwa na andiko ambalo thamani yake ilikuwa ni milioni 180 tu ambavyo ingeweza kusaidia kupata maji ya uhakika kutokana na utafiti ambao ulifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa kuna mradi wa Amani. Naishukuru sana Serikali ule mradi umeweza kusaidia vijiji vitatu, lakini maji yale ni mengi, mabomba yanapasuka kila siku nilipeleka Ofisini kwa Mheshimiwa Waziri andiko la kuongezea vijiji vitatu ili kuweza kuondoa tatizo hili la kupasuka mabomba kila siku kutokana na presha kubwa ya chanzo cha maji ambayo yanakuwa supplied katika mradi ule. Lile andiko liko ofisini kwa Mheshimiwa Waziri, lina thamani ya milioni 300 tu ambalo lingeweza kusaidia kuondoa hilo tatizo la kupasuka mabomba yale kila siku ili kuweza kuwahudumia wananchi wengine wa Misechela, pamoja na Liwanga ambao wanateseka na wanashida kubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)