Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa fursa ya kuchangia jioni hii juu ya jambo muhimu sana kuliko mambo mengine, maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijasema maneno yangu, Mheshimiwa Waziri, Profesa, pamoja na mdogo wagu Mheshimiwa Aweso, mimi sina matatizo na ninyi bali Serikali. Kwa sababu hapa ndani wakati mwingine Wabunge tunazungumza inaweza ikaonekana kama tuna matatizo na Mawaziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema maji ni uhai. Mawaziri mnisikilize vizuri, maji ni uhai. Waheshimiwa Wabunge, hebu tujaribu wiki yote moja hii tule bila kunywa maji tuone itakuwaje, hapo ndiyo tutakapojua maji ni uhai. Sasa ukishakuona ndugu na jamaa zako wanakutenga na maji, hawa wana mawasiliano na Mwenyezi Mungu afungue lango la mbinguni ili wewe uende kule maana yake hawataki upate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa Ulyankulu tumetengwa na nitaendelea kusema mpaka siku ya mwisho. Alikuja Makamu wa Rais, unajua wanasiasa unaweza ukaanza kusema lolote, mtu mmoja akasema Ulyankulu ni mbali kwa hiyo maji yasiende, ajabu kabisa hii. Sasa kutoka Tabora kwenda Ulyankulu yaani kuingia kwenye Kijiji cha Kadutu kilometa 60…

MBUNGE FULANI: Ni mbali sana.

MHE. JOHN P. KADUTU: Ni mbali hiyo? Kutoka Tabora kwenda Urambo kwa Mheshimiwa Mama Sitta ni kilometa 94; kutoka Tabora mpaka Kaliua ni kilometa 120, hapo ni karibu sana; kutoka Kahama kwa ndugu yangu Mheshimiwa Kishimba pamoja na Mheshimiwa Kwandikwa kuingia kwenye Jimbo langu la Ulyankulu ni kilometa 80, bado watu wanasema Ulyankulu ni mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna miradi miwili, mradi wa kwanza unatoa maji Ziwa Victoria, hawataki ufike Ulyankulu. Kwa sababu maji Kahama yapo yangeweza kuletwa Ulyankulu watu wakatulia, Tabora yatafika lakini hata maandishi tu ya kupeleka maji Ulyankulu hayapo. Tuna mradi wa maji Malagarasi, hapo sasa nadhani ndipo hatutaelewana, maji ya Malagarasi yanatoka Ulyankulu lakini mradi huu umeandikwa maji yatakwenda Kaliua na Urambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku tulikuwa tunakutana Kaliua na Profesa akija kwenye ujenzi. Kuna picha moja ya Chuck Norris walikuwa na kamanda mwingine hivi wakapotezana kwenye ile filamu. Siku ya mwisho kamanda yule anamwambia Chuck Norris we meet again, sasa Mheshimiwa Profesa tumekutana tena. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa alikuwa anakuja nakupokea Kaliua nikakwambia Ulyankulu mpaka uwe na dhamira ya kwenda Ulyankulu, sasa maji mimi sina. Sasa huu mradi wa Malagarasi maji yanatoka Mto Igombe Ulyankulu, sasa niwaambie tu, kama hamtatupatia maji watu wa Ulyankulu tunakwenda kuziba mto halafu mje mniweke ndani mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila jambo Ulyankulu inatengwa. Sijui na kwenye maji mtasema wakimbizi. Jamani hebu kuweni na huruma wakati mwingine. Hatupendi kusema Mheshimiwa Profesa, hebu tupeni maji muone, tutatulia. Maji yanawezekana, kilometa hizo nimesema lakini kama nilivyosema, mtu anasimama kwa Makamu wa Rais unadanganya yaani ili kuhakikisha tu watu wa Ulyankulu hatupati maji. Mheshimiwa Profesa na Naibu wako fanyeni mnaloweza tupate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tutatengwa kwa kila jambo? Tuna mradi wa bwawa pale Kijiji cha Ichemba, wameshakuja wametembeatembea sijui ndiyo upembuzi, lakini wamekwenda moja kwa moja hatujui itakuwaje, wananchi bado wana taharuki kwa sababu hawajajua mradi ule utapita kwenye mashamba gani ya watu. Kwa hiyo, hatuna shida nyingine zaidi, kama kila huduma ya Serikali hailetwi Ulyankulu mimi siwezi kujua, sijui tatizo ni Kadutu, sijui kama kweli ni wakimbizi au ni nini, hata maji? Hivi mtu anaweza kuja nyumbani kwako akakuomba maji kikombe kimoja, utamnyima? Huwezi kumnyima, tupeni basi maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hamtaki kutupa tawala za mikoa tupeni maji tu tutaishi. Kama hamtupi maji hatuwezi kuishi. Maana ninyi mna mawasiliano na Mwenyezi Mungu, tutaona sasa nani mwenye mawasiliano na Mwenyezi Mungu na lango halitafunguliwa, hatutakufa sisi, tutakuwepo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nilisema last week na kama alivyosema Mheshimiwa Ndassa, tunakuwa na hoja mahsusi moja, tusipende kuchanganya na mimi sijapenda kuchanganya. Bahati nzuri wataalam wako hapa nyuma yangu, wajue tu tutaleta vagi hata wenyewe hawatakanyaga huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa John Kadutu, tunaendelea na Mheshimiwa Lucia Mlowe.

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)