Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kupata nafasi ya kuchangia kwenye bajeti muhimu ya Wizara ya Maji. Awali ya yote, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa ambazo inazifanya hasa kwenye miradi ya maji. Jimboni kwangu ipo miradi ya maji ambayo ilishaanza kutekelezwa; nina mradi wa Kijiji cha Kabungu ambao una thamani ya shilingi milioni 600, mradi wa Kijiji cha Kamjela wenye thamani ya shilingi milioni 800 na mradi wa Kata ya Mwese wenye vijiji vitatu ambao una thamani ya shilingi bilioni moja na milioni mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ikikamilika itawasaidia sana wananchi wa maeneo husika ambao wanategemea kutatua kero ya maji. Niiombe sana Serikali iharakishe kupeleka fedha kwa ajili ya kumalizia hii miradi. Fedha zitakapokuwa zimeenda, tunategemea kero ya maji ambayo ipo kwenye hivi vijiji itakuwa imetoweka na kuwafanya wananchi waweze kuzalisha na kufanya shughuli zao za maendeleo bila kuwa na wasiwasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vijiji 18 ambavyo vilichimbiwa visima. Vijiji hivi vinategemea mradi huo ambao ulikuwa na thamani ya shilingi milioni 400 uweze kutatua tatizo kubwa kwenye maeneo husika ya hivyo vijiji, mpaka sasa bado vijiji hivyo havijakamilishiwa hiyo miradi ya visima. Niombe sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana akisaidiwa na Naibu wake watoe msukumo mkubwa ili hivyo vijiji viweze kukamilika, miradi hii itawasaidia sana wananchi. Akinamama wengi kipindi cha kiangazi hawafanyi kazi nyingine, kazi kubwa ni ya kwenda kutafuta maji yalipo. Kwa hiyo, naomba Wizara iangalie uwezekano wa kusaidia kwenye maeneo haya ili vijiji hivi viweze kukamilisha na kazi ilishafanyika, wametumia fedha nyingi lakini bado kile kilichokuwa kimekusudiwa hakijatekelezwa ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo Mmradi wa Kijiji cha Ngomalusambo. Mradi huu fedha zilizopelekwa zimeliwa, mradi ulikamilika lakini haujatoa hata tone la maji. Niombe sana Mheshimiwa Waziri afike kwenye eneo hili akajionee, aangalie tatizo lililopo kwenye eneo la Kijiji hiki cha Ngomalusambo. Mradi ulipokamilika wananchi walifurahi wakitegemea watapata maji ya kutosha, lakini toka ulipokuwa umekabidhiwa kwenye kijiji husika, mradi huu umebaki kuwa pambo, haujaonesha matunda yake. Naamini watendaji waliosimamia ule mradi hawakuutendea haki na ni vyema wakawafuatilia ili waangalie zile fedha zilizotumika zaidi ya milioni 200 hazikufanya kazi ya aina yoyote na tija haipo. Naomba hili Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo Mradi wa Kijiji cha Karema; Mradi wa Maji wa Karema ni mradi ambao tulitegemea kwamba ungekuwa umetatua kero ya wananchi kwenye eneo la Kata ya Karema. Kwa bahati mbaya sana mradi huu toka umekamilika umekuwa na shida kubwa sana ya kutoa huduma ya maji. Niombe sana Serikali iende ikachunguze ule mradi ili tuangalie ni kitu gani kinachosababisha mradi usitoe maji kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama chanzo cha maji kinaonekana hakifai, Mji wa Karema upo jirani sana na Ziwa Tanganyika; tutaona kitu cha ajabu sana kama maji hayatapatikana kwenye maeneo hayo. Niombe Mheshimiwa Waziri najua anaufahamu mradi huu, waufanyie uhakiki na watume wataalam waende wakafanye kazi ili tutoe tatizo lile la maji ambalo lipo kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu utakapokuwa umefanyiwa ukarabati na ukakamilika, utakuwa umetatua kero kubwa sana. Wananchi wengi wa ukanda wa ziwa huwa wanapata mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu kwa sababu ya kutumia maji ya ziwani. Kwa hiyo, tunaomba muufuatilie huu mradi ili uweze kutoa suluhisho la kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi mkubwa wa maji unaotarajiwa kufanywa na Serikali wa kutoa maji Ziwa Tanganyika kuyapeleka Makao Makuu ya Mkoa wa Katavi, Mpanda Mjini. Mradi huu ni muhimu sana kwa wakazi wa Mkoa wa Katavi na utasaidia karibu maeneo yote. Nauzungumzia mimi kwa sababu mradi huu upo Jimboni kwangu na utakapokuwa umekamilika, utawanufaisha wananchi wa vijiji takribani 10 ambao watapitiwa na ule mradi. Niombe sana Wizara iharakishe mchakato wa mpango wa kupeleka maji kwenye Mkoa wa Katavi, ule utakaotoa maji kutoka Ziwa Tanganyika ili uende kutatua kero ya Manispaa ya Mpanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Mpanda una matatizo makubwa sana ya maji, mji umekua lakini bado unahitaji sana huduma ya maji. Chanzo pekee cha maji kilichopo hakitoshelezi kupeleka maji kwenye maeneo husika. Kwa hiyo, tunaomba mradi huu ujengwe haraka na unapojengwa upewe kipaumbele kwenye maeneo ambayo yatapita kwenye mradi, Kijiji cha Kapalamsenga tunategemea kabisa nacho kitapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Itetemya, Kijiji cha Kasekese, Kijiji cha Kaseganyama, Kijiji cha Sibwesa, Kijiji cha Mkungwi, Kijiji cha Ikata, Kijiji cha Kabungu na vinginevyo ambavyo vitapitiwa kwenye Jimbo la Mheshimiwa Kapufi, Mpanda Mjini viweze kunufaika na mradi huu. Ni vyema Serikali ikausukuma huu mradi ili uweze kufanya kazi kwa wakati na tuna mategemeo sana na Waziri husika na msaidizi wake kwamba wataufanyia kazi wakishirikiana na timu yao ya wataalam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo Vijiji 16 kwenye Jimbo langu; Vijiji vya eneo la Mishamu. Vijiji hivi vilikuwa na visima vya maji, ni eneo lililokuwa la wakimbizi na UN ilichimba visima vingi kwenye maeneo hayo. Bahati mbaya, miradi hii ni ya muda mrefu na nimekuwa nikiiomba Wizara kila siku iweze kuwasaidia wananchi wa maeneo yale kuvifanyia ukarabati vile visima ili viweze kutoa huduma ya maji. Ni mategemeo yangu kwamba Wizara ni sikivu, mtaenda kuangalia changamoto zilizopo kwenye vijiji hivi vya Mishamo vipo 16 ili waweze kuwasaidia na waweze kutoa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, tunaipongeza Serikali kwa jitihada ambazo wamezifanya na zaidi tunawapongeza Mawaziri kwa kazi kubwa sana wanayoifanya. Naamini Waziri husika amefika kwenye miradi ambayo nimeitaja, tunaomba akaifanyie kazi, awape fedha wakandarasi waweze kukamilisha ile miradi ili iweze kutoa huduma husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)