Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Mboni Mohamed Mhita

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba awali ya yote nitumie fursa hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu pamoja na watendaji wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niendelee kutoa kilio cha wananchi wa Wilaya ya Handeni, niendelee kutoa kilio cha wananchi akina mama wa Handeni Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya maji Handeni imegeuka kuwa janga la kiwilaya. Nasema janga kwa sababu ukosefu wa maji katika Wilaya ya Handeni pamoja na Jimbo la Handeni Vijijini umezuka sasa na kusababisha changamoto mbalimbali ambazo sasa zimeanza kuingia katika sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosefu wa maji Handeni umechangia kwa kiasi kikubwa kusababisha milipuko ya magonjwa. Historia ya kupatikana Ugonjwa wa Kipindipindu Handeni ni kwa sababu ya ukosefu wa maji katika Wilaya ya Handeni ambayo sasa hiyo imeingia kwenye Sekta ya Afya. Lakini wakati huohuo, ndoa za akina mama Wilaya ya Handeni zinalegalega, akina mama wanaamka alfajiri saa kumi kwenda kutafuta maji, na haina guarantee kwamba wakirudi wanarudi na maji. Wakati mwingine wanatoka saa kumi wakirejea ni saa saba au saa nane za mchana na wakati huo hawajarudi na maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe utajionea, uaminifu kwenye zile ndoa unapungua, ndoa nyingine zinalegalega, na akina mama wengine wamekosa ndoa zao kwa sababu ya changamoto ya maji. Hilo ni tatizo la kijamii sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtagundua kwamba watoto wa kike Mkoa wa Tanga tumekuwa tukishika mkia kwenye ufaulu, sasa hapo tumeingia kwenye elimu. Kwa sababu mabinti hao badala ya kutumia muda huo kwenda kujisomea wanautumia kwenda kusaka maji. Wakati wenzao wa wilaya na mikoa mingine wakitumia muda huo kujisomea, sisi mabinti wa Handeni Vijijini tunatumia muda huo kwenda kusaka maji, hali kadhalika mtajionea kwamba comparison ya ufaulu utatofautiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati huohuo, muda ambao akina mama wanaamka kwenda kusaka maji ndiyo muda ambao na wanyama wakali pia wanatoka kwenda kusaka maji. Sasa hebu tuangalie mwanamama in a very vulnerable situation anakutana na mnyama mkali, wengine wamedhurika na wengine wamepoteza maisha kabisa, hilo ni tatizo la kiusalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo kubwa kabisa ni kurudi nyuma kiuchumi. Wakati ambao wenzetu wa wilaya na mikoa mingine wanajijenga kuanzisha miradi ya akina mama na kutumia mikopo mbalimbali sisi akina mama wa Wilaya ya Handeni na Jimbo la Handeni Vijijini tunatumia kwenda kusaka maji. Ni ukweli usiofichika kwamba hata ukituangalia hatuwezi kulinga na akina mama wa mikoa mingine, hatuwezi kulingana na akina mama wa wilaya nyingine kiuchumi kwa sababu muda ambao wenzetu wanatumia fursa za Serikali za kutengeneza vikundi, za kuanzisha miradi, sisi tumejitwika ndoo tunasaka maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nini kifanyike? Naomba nitoe maoni yangu; kwanza niishukuru sana Serikali ilitupatia bilioni mbili ili kuweza kukarabati Mradi wa HTM ambao kwa kirefu ni Handeni Trunk Main. Lakini mradi huu ulianza mwaka 1974 ukiwa na lifespan au uhai wa miundombinu wa miaka 20, nikiwa na maana kwamba mwaka 1994 ile miundombinu itakuwa imechoka. Sasa wenyewe tufanye hesabu kuanzia mwaka 1994 mpaka 2004 mpaka 2014 mpaka 2019, miaka mingi imekwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashukuru Mungu Serikali imetuweka kwenye mpango lakini naomba sasa pendekezo langu liwe Serikali iharakishe ukarabati wa miundombinu ya HTM ili akina mama wa Handeni ambao wamekuwa sasa wamezoea kuisikia hii ahadi, imekuwa kama ni ahadi sugu, angalau waone utekelezaji wa kuonekana. Naamini kwamba Serikali ina mipango mizuri lakini bado iko kwenye paperwork Wizarani, hatujaanza kuona implementation katika Wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo langu la pili, naomba Serikali iridhie sasa Mji wa Mkata ambao ndiyo Makao Makuu ya Halmashauri ya Handeni Vijijini, itegemee vyanzo tofauti vya maji. Pale kunategemewa HTM, kunategemewa visima, lakini tunategemea CHALIWASA ambao ni mradi wa Chalinze, ambao tunashukuru Mungu mpaka sasa hivi ile miundombinu imefika Manga, na Manga ni kijiji ambacho kiko ndani ya Kata ya Mkata. Kwa lugha nyingine ni kwamba Serikali ikiridhia basi miundombinu ile inaweza ikasogea mpaka Mkata Mjini na kata ile ikawa ina sources mbalimbali za kuweza kujipatia maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa lakini si kwa umuhimu ni Serikali ifuatilie ubadhirifu mkubwa ambao umefanyika kwenye mabwawa ya Manga, Mkata na Kwandugwa, pamepotea zaidi ya bilioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru Mungu kwamba Waziri alifika, Naibu Waziri amefika na amejionea. Tulifanya ziara na Mheshimiwa Waziri, na tukafanya ziara na Mheshimiwa Naibu Waziri, kaka yangu, Mheshimiwa Aweso alifika mpaka eneo na alijionea na siku hiyo baadhi ya wakandarasi pale walishikiliwa. Lakini kushikiliwa kwa wale bado hakujaokoa hali ya changamoto ya pale Handeni, Handeni Vijijini na Kata nzima ya Mkata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisitumie muda naona kengele ya pili imelia, kwa hiyo naomba Serikali ichukue hatua kali. Baba yangu, Mheshimiwa Keissy alisema fedha zile zitapikwe, bilioni moja ni nyingi sana kupotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja. Nashukuru sana, ahsante sana kwa kunisikiliza.