Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hotuba hii ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nianze kwa kuwapongeza kwa kazi nzuri sana ambayo Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji Wizarani wanafanya. Tunawaona wanajitahidi, wanakimbia, wanafanya kazi, wanabeba maji vichwani, wanafanya kazi nzuri, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuongelea eneo la uboreshaji wa Mamlaka mbalimbali za Usimamizi wa Maji. Imefanyika kazi kubwa sana na mfano mzuri ni pale Dar es Salaam (DAWASCO), nadhani kuna maboresho na uimarishaji mkubwa wa Mamlaka ile kiasi kwamba kelele ambazo tulikuwa tukizisikia sana Dar es Salaam zimepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni vizuri tupongeze na kutambua kazi ya Bodi inayoongozwa na Gen. Mwamnyange pia na Mtendaji Mkuu wa Mamlaka hii Ndugu Luhemeja. Nadhani wanafanya kazi nzuri sana. Kwa muda sasa zile kelele ambazo tulikuwa tukizisikia zimepungua, wanajituma, tunawaona mtaani wanafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya maboresho na marekebisho yaliyofanyika kwa Mamlaka ya Dar es Salaam yafanyike na mikoani na kasi iende hiyohiyo kwa Mamlaka zingine. Nadhani itatusaidia sana kwa sababu moja ya eneo kubwa lenye changamoto ni usimamizi. Kwa hiyo, Mamlaka hizi zikiboreshwa wakaiga mfano wa hii Bodi ya Gen. Mwamnyange na mwenzake Ndugu Luhemeja nadhani watakuwa wamefanya kazi nzuri na tutayaona mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli napongeza kazi nzuri iliyofanyika Dar es Salaam na sasa ihamishiwe mikoani. Nadhani ni vizuri uimarishaji huu ukaenda pia kwenye Mamlaka zile ndogo za kule chini kabisa na zile Jumuiya za Usimamizi tusiwaachie wananchi peke yake. Usimamizi uwe wa wananchi lakini pengine tupeleke utaalam fulani pale ili kusaidia usimamizi uwe bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka ni Mfuko wa Maji. Mwaka 2018/2019 takwimu za upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maji kutoka kwenye Mfuko wa Maji zimepelekwa asilimia 67, napongeza, lakini kutoka kwenye vyanzo vya ndani vingine tumepeleka asilimia 17. Maana yake nini? Maana yake ni kwamba kama isingekuwa Mfuko Wizara hii mngekuwa hamjafanya chochote kwa sababu ingekuwa asilimia 17 peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mitatu mfululizo hoja ya kuongeza fedha ili zikaongezeke kwenye Mfuko huu zimekuwa zikija hapa Bungeni. Hoja yangu hapa nachoshangaa huku kutoona kwa Serikali kunakuja kwa sababu gani? Ni kwamba ninyi mkishawaza ndiyo final, hapa tunakuja kufanya nini kama kwa miaka mitatu tunasema hela iongezwe na haiongezwi na Serikali inaendelea na msimamo wake? Tunaletwa kufanya nini hapa, shilingi 50 tu inashindakana kuongezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwetu sisi umeme ni bora kuliko maji kwa sababu REA tunapeleka shilingi 100 na mambo yanakwenda vizuri na tunaipongeza sana Serikali lakini kwenye jambo ambalo linagusa maisha ya kila mtu hata maskini wa mwisho, hivi tunachoogopa ni nini? Tunachong’ang’ana nacho ni nini? Kwa nini tunataka tulifanye Bunge lionekane halina maana kwa miaka mitatu mfululizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani safari hii Waheshimiwa Wabunge tusikubali. Tumesema na tumebembeleza vya kutosha, safari hii tuweke mguu chini fedha iongezwe, si sawa hivi tunavyoenda. Mimi nimeona hapa tunabembelezana inakuja tunajibishana ooh sijui inflation sijui nini si sawa. Kwa sababu tatizo hili ni kubwa na takwimu zimeonesha bila huu Mfuko miradi yote ingesimama, sasa tusiendelee na kiburi hiki maana kinaumiza wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona humu kuna miradi kwa mfano kuna fedha zile wa Wahindi dola milioni 500, hizi fedha zina miradi specific sisi wananchi wa vijijini hizi fedha hazitafika kwa baadhi ya maeneo yetu. Ukombozi wetu peke yake ni huu Mfuko wa Maji.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu kwa Serikali na kwa Bunge…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nape, tusikilize taarifa kidogo.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokisema kaka yangu Mheshimiwa Nape Nnauye naungana naye kwa silimia 100 siyo tu lazima tupate fedha kutoka kwenye chanzo anachokisema cha mafuta lakini ku- compliment anachokisema Mheshimiwa kaka Nape tunaweza tukapata fedha za kuwasaidia Watanzania hata kutoka kwenye mawasiliano ya simu. Mheshimiwa kaka Nape unachokisema nina ku-compliment safari hii bila kuongeza fedha Wabunge hatutokubali kwa lengo la kuwasaidia watu wetu kwenye sekta ya maji. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nape.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake na namshukuru kwa kuniunga mkono. Ni kweli Serikali tukibaki na kisingizo kwamba kwenye mafuta kutaleta inflation hivi chanzo ni mafuta peke yake, je, kwenye simu au data? Hoja yetu hapa ni kwamba huu Mfuko uongezewe chanzo cha fedha, basi. Mnatoa wapi msiende kujificha kwenye mafuta peke yake, Serikali inaweza kufikiria nje ya boksi tukaenda kwenye vyanzo vingine. (Makofi)

Hoja yetu ni kwamba bajeti ya maji safari hii tunaipitisha hapa kama mnakuja na mpango wa kuongeza fedha vinginevyo mtatuona Waheshimiwa Wabunge wabaya. Kwa hiyo, zile siku za mashauriano zikatumike vizuri na Serikali wekeni commitment hapa kwamba mnakwenda kushauriana, nendeni mkabane kwenye vyanzo vingine huu Mfuko tuuongezee fedha tuone maji yanatiririka vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, tatizo kubwa hili la maji linahitaji mikono ya wadau wengi tulete nguvu ya pamoja. Tulitunga sheria hapa ya Kudhibiti Rasilimali ya Maji ya mwaka 2009. Sheria hii ilianzisha pia mabonde, yako mabonde ya usimamizi wa maji ni kama tisa (9) kama sikosei. Huku kuna kanuni zimetungwa za kusimamia, lengo ni jema lakini zimeweka tozo mbalimbali za watumiaji wa maji haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanatumia maji kwa domestic use, mtu anachimba kisima nyumbani kwake kwanza anatakiwa apewe kibali na anatakiwa akilipie halafu kila mwaka anatakiwa alipe tozo kwa ajili ya kutumia kile kisima. Mimi nasema tukiwatoza watumiaji wa maji ambao wanakwenda kutumia kibiashara sina matatizo nalo lakini hawa ambao ni mtu binafsi ameamua kusaidia watu kwenye eneo lake amechimba kisima kwa fedha zake, ameweka infrastructure kwa fedha zake halafu bado tunaenda kumtoza, actually, nilidhani Serikali badala ya kumtoza ilitakiwa kumlipa kwa sababu anaisadia kusambaza huduma ya maji kwenye eneo lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana mnasimamia na kutekeleza kwa sababu ni suala la kisheria. Ushauri wangu kama ni sheria leteni hapa tufute kwa sababu ni sheria ambayo haina maana badala ya ku-encourage watu wachimbe visima zaidi, kwangu pale Mtama Makao Makuu ya Jimbo kuna watu zaidi ya 50 wamechimba visima halafu unajua kilichotokea nyuma pale walikuwa wanafumbia macho kidogo hivi kwa hiyo watu wanachimba wanaendelea, sasa hivi kwa sababu ya hii dhana ya kukusanya zaidi wameenda kukusanya mpaka madeni ya nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unamkuta mtu ana kisima anaambiwa alipe Sh.700,000 leo, mwanakijiji wa kawaida amechimba kisima kwa hela zake, unachofanya ni kumwambia huyu afunge na akifunga hasara ya nani? Kwa sababu maji yakikosekana hapa mwisho wa siku Serikali itabidi mpeleke fedha za kutibu watu waliougua kwa sababu ya kupata maji machafu, sasa mnachokipata ni kipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu Serikali kwanza wekeni commitment halafu jipangeni leteni kama ni sheria hiyo tubadilishe, kama ni kanuni nendeni mkakae mzibadilishe. Mimi nashauri wale wanaofanya biashara tena siyo ile biashara ya kuuziana mtaani pale, mtu amechimba kisima anawauzia wenzake pale shilingi tano na yeye mnafanya ni mfanyabiashara, huyu ni mtoa huduma tu. Kuna watu wanafanya biashara, wanaotaka kuzalisha umeme tozeni kodi mnayotaka, wanaozalisha maji yale ya kuuza ya chupa tozeni kodi mnayotaka, wale wanaofanya umwagiliaji mkubwa tozeni lakini watumiaji wa kawaida, nimechimba kisima nyumbani kwangu nataka nijihudumie mwenyewe na majirani zangu, nadhani tukiendelea kutoza si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mapendekezo yangu Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana, Mheshimiwa malizia.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja nikiamini kwamba Serikali itakuja na commitment ya kutosha juu ya hoja nilizoziweka hapa. (Makofi)