Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi na kabla sijaanza kuchangia hoja hii, naomba nichukue nafasi kwa niaba ya Kambi Rasmi ya Upinzani niweze kutoa salamu za rambirambi kwa familia ya Marehemu Reginald Abraham Mengi, Wafanyakazi wote wa Makampuni ya IPP, Wanahabari wote Nchini na Afrika Mashairiki, Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Tanzania, Watanzania wote na wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro kwa kifo hiki cha ghafla cha ndugu Mengi ambaye alikuwa mtu mkarimu, alisaidia Watanzania wengi, aliajiri wengi, alikuwa Baba mwenye huruma kwa watu wote hasa walemavu na aliwasaidia Watanzania kuwajengea ari ya kujitegemea. Tutakumbuka kitabu chake kile cha “I can, I will, I must” kimewasaidia Watanzania wengi sana kuwa na courage na moyo wa kufanya biashara. Kwa hiyo huu ni msiba mkubwa unatusikitisha wote, naomba Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema peponi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo, niseme tu kwamba Wizara hii ni Wizara nyeti, ni Wizara ambayo inategemewa na Watanzania lakini inategemewa na sekta zote hapa nchini; inategemewa na Kilimo, Afya, Viwanda na kila kitu. Kwa hiyo ni Wizara ambayo inahitaji ushauri mzuri na inahitaji msaada wa kutosha kwa kweli badala ya kulaumu tu. Kabla sijatoa ushauri, niseme tu kwamba Jimbo langu ya Rombo lina shida kubwa sana ya maji na utashangaa Rombo ndiko ambako Mlima Kilimanjaro upo. Zamani kulikuwa na mito mingi ikitoka pale mlimani na kugawa maji katika maeneo mengi ya Mkoa wa Kilimanjaro, lakini sasa nadhani Rombo ni Wilaya inayoongoza kwa uhaba wa maji pale mkoani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niseme tu kwamba naishukuru Wizara, tuna mradi pale katika Vijiji vya Shimbi Mashariki, Ngareni na Ngoyoni ambavyo kwa jumla tulikuwa tunahitaji bilioni 1.33 ili kukamilisha ile miradi lakini Wizara imeshatupatia shilingi milioni 717.7 na sasa hivi tunaomba Wizara itukamilishie shilingi milioni 617 ili miradi hii ambayo ni ya siku nyingi ianze kufanya kazi. Ni matumaini yangu kwamba Wizara itatekeleza kwa sababu niliongea na Naibu Waziri, nimeongea na Katibu Mkuu kwa kweli ni watu ambao ni wasikivu, wanapenda kushirikiana, kwa hiyo nadhani kwamba hili lilatekelezwa, naomba sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ni vyema Serikali pamoja hata na wananchi wangu wa Rombo kufahamu kwamba changamoto ya maji Rombo ukubwa wake unatokana na kwamba hakujawahi kuwa na uwekezaji mkubwa wa maji katika Wilaya ya Rombo kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita. Kwa hivyo miundombinu na vyanzo vya maji vilivyopo kwa miaka 20 iliyopita havijawahi kuboreshwa. Hata hivyo, kwa sasa ninayo furaha kwamba Serikali imeridhia kuboresha huduma hiyo ya maji kwa vijiji 41 vya ukanda wa chini ambavyo ndiyo nina shida kubwa sana ya maji. Kuna usanifu umeshafanyika kutoka chanzo cha maji cha Ziwa Chala ambacho chanzo kile kilikuwa kidogo Wakenya wanasumbuasumbua lakini sasa hivi wameshakubali na Serikali imeshaanza usanifu, kwa hiyo nawaomba Warombo wenzangu wawe watulivu, kazi hiyo inafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna chanzo kingine cha Mto Njoro kule Tarakea vilevile Wizara kwa kutumia wataalam wake na wataalam wa kule Halmashauri wameshaanza uwezekano wa kupata maji katika chanzo kile na chanzo kingine cha Kinyasini, Mto Uwashi na Mbushi vyote hivyo katika Mwaka huu wa Fedha huenda kazi ikafanyika na nimeongea na Katibu Mkuu kwamba tayari fedha ambazo zimeshatengwa bilioni 10 huenda zikapatikana kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri, tulishasema mara nyingi hapa Bungeni kwamba tunayo shida kubwa sana na Jumuiya ya maji inayosambaza maji kule Rombo. Hii Jumuiya inaitwa Kiliwater. Utashangaa mwezi uliopita, mimi binafsi nimepokea bili ya maji Sh.58,000 na kule nyumbani nimeacha watu wawili tu ndiyo wanaotumia maji, lakini imeingia bili ya Sh.58,000. Nimejaribu kulalamika wakaniambia iko sawasawa, haya ndiyo malalamiko ya wananchi kwamba hata maji kidogo yaliyopo yanagawanywa vibaya na wale wanaotaka wafungiwe maji, hawafungiwi kwa sababu ambazo wala hazieleweki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya mwanzo wakati Mzee Lwenge akiwa Waziri tulilalamika na tukaomba kwa sababu Halmashauri iliweka azimio kwamba tuombe tuanzishiwe Mamlaka ya Maji katika Halmashauri ya Rombo baada ya kuindoa hii Halmashauri na ombi hili lilikubalika sasa kama litatekelezwa au kama tutaanzisha ile Mamlaka ya Maji ile ya Kitaifa ambayo itasimamia maji kwa ujumla, lakini kwa wakati huu wa mpito ile Jumuiya inayogawa maji pale, ifanywe mikakati ya kuiangalia ili isiendelee kuumiza wananchi, wakifanya hivyo watakuwa wamewasaidia sana watu wa Rombo .

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo lingine ambalo nataka kusema, suala la maji ni kubwa na kama tusipokuwa makini suala hili linaweza likaja kusababisha hata vita ya tatu ya dunia kwa sababu vyanzo vingi vya maji vinakauka nchini na hata duniani kwa ujumla. Kwa hiyo, ningeishauri Serikali; kwanza tufanye mkakati wa kuanzisha mabwawa maalum ya kuhifadhi haya maji ya mvua ambayo yanapotea hovyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukivuna haya maji ya mvua yanaweza kutusaidia. Nilisema tena katika mchango wangu mwaka uliopita; ukiangalia hapa Kongwa mpaka Kibaigwa maji mengi yanamwagika hovyo kutoka Kiteto huko na nchi kama zile za Senegal, Siera Leone huko walianzisha kitu kinaitwa “man-made lakes”, wakachimba, wakakinga yale maji na sasa hivi wanayatumia, hiyo itatusaidia. Vilevile tuanze utaratibu wa kugawana pia hata maji haya tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, tuanzishe utaratibu wa makusudi kwa baadhi ya maeneo hata mjini kufanya recycling ya maji haya tunayotumia tunasema machafu, tunayatupa, kwa sababu haya maji yanaweza yakatusaidia kwa matumizi mbalimbali; kwa matumizi ya wanyama, yanaweza yakatusaidia kwa matumizi ya umwagiliaji na matumizi mengine hata matumizi ya majumbani ukiondoa matumizi ya chakula na kadhalika. Kwa hiyo, ninachokisema ni kwamba, inawezekana tumerdhika kwamba maji tunayo, mito ipo na kadhalika, lakini tunakokwenda maji yanapungua Kitaifa na Kimataifa, kwa hiyo Wizara ifanye mikakati ya namna ya kuhifadhi haya maji yaliyopo ili yaweze kutumika sawasawa. Pia watunze na haya mabwawa kwa sababu kuna mabwawa mengine yanapotea. Angalia kwa mfano, Ziwa hili la Babati; Ziwa la Babati sasa hivi linajifukia kwa sababu ya uchafu. Angalia Ziwa Jipe; na lenyewe linajifukia kwa sababu ya uchafu kwa sababu tusipofanya bidii wenyewe kile alichotupa Mwenyezi Mungu kinapotea

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni huizi certificates; ni kweli zinachelewa na zikichelewa zinapandisha gharama kwenye ile miradi na ni kweli vilevile kuna ufisadi kwenye hii miradi na ni ukweli vilevile kwamba baadhi ya Watumishi katika mamlaka zetu na kadhalika bado hawajaenda na kasi ambayo inazungumzwa. Sasa nifikie mahali niseme, kwa nini tuna mamlaka halafu tunalalamika? Yaani kwa nini tunalalamika kuhusu Watumishi wa Halmashauri sisi Bunge? Yaani tunakaa hapa Bungeni tunamjadili Injinia wa Maji wa Halmashauri fulani, hivi hii inawezekana kweli? Kwa hiyo, niseme kwamba labda pengine sisi tumekosea mahali fulani. Niishauri Wizara hao wanaolalamikiwa wachukue hatua ili Wizara iendelee na kazi yake nzuri ambayo inafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)