Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza mchango wangu kwa kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Makatibu wote wanaohudumu kwenye Wizara hii kwa kazi nzuri na kubwa ya kusimamia elimu nchini, hasa Sera hii ya Elimu Bure. Sera hii imewezesha watoto wengi kupata elimu ambayo ni haki yao ya msingi.

Mheshimwia Mwenyekiti, pia napenda kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kufanya maamuzi muhimu ya kutekeleza Sera hii ya Elimu Bure ambayo ni hitaji la nchi yetu kwa muda mrefu. Kwa hili Mheshimiwa Rais amethubutu na amefanikiwa kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sasa Taifa letu linaelekea kwenye uchumi wa viwanda, ipo haja kubwa sana ya kuimarisha vyuo vya ufundi kuanzia vile vya VETA hadi vya mafundi mchundo (FTC). Katika kuimarisha vyuo hivi ni bora vyuo vya ufundi visichanganywe na kozi nyingine kama vile kozi ya urembo na ulimbwende. Jambo hili limekuwa likivunja hadhi ya vyuo vyetu. Vilevile, Vyuo vya VETA visiwe kimbilio la wale waliofeli Form Four na Darasa la Saba, ifike wakati hata wale waliofanya vizuri kwenye masomo ya Sayansi wapelekwe VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Liwale ndiyo wilaya iliyo mbali sana na Makao Makuu ya Mkoa wa Lindi ambako kuna Vyuo vya VETA, Ualimu na Afya. Hivyo, vijana wengi wanashindwa kumudu kupata elimu ya vyuo hivyo. Hivyo Serikali ione umuhimu wa kutujengea Chuo cha Ufundi, VETA. Halmashauri imeshaanza kujenga maboma mawili ya madarasa, hivyo naiomba Serikali kuokoa nguvu za wananchi kwa kuwapatia Chuo cha VETA. Vijana wengi wanaoshindwa kuendelea na masomo ya juu kwa kukosa nafasi wangeweza kupata elimu hiyo ya VETA kwa karibu badala ya kwenda Lindi ambako ni mbali na gharama ni kubwa. Liwale tuna uhitaji mkubwa wa Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi wa vyuo vya ufundi ni muhimu sana kuhudhuria mafunzo kwa vitendo, lakini wanafunzi wengi wanashindwa kuhudhuria kikamilifu kutokana na changamoto mbalimbali, kama vile nauli za kwenda na kurudi makazini na chakula cha mchana wanapofanya kazi viwandani. Naomba Serikali ifikirie kuwapatia posho za mafunzo viwandani wanafunzi wanaohudhuria mafunzo kwa vitendo. Hakuna maana ya kuwapeleka watoto katika shule/chuo cha ufundi kama elimu hiyo haitaambatana na elimu kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie uhaba wa walimu, hasa walimu wa Sayansi. Hapa napenda nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kuanza kuajiri walimu. Nishukuru kwa Halmashauri yangu ya Liwale kuwa miongoni mwa Halmashauri zilizopata mgao wa walimu hao japo limekuwa kama tone la damu baharini, kwani uhaba wa walimu ni mkubwa sana Wilayani Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule zetu nyingi zina walimu watatu tu. Shule zenye walimu wengi ni zile zenye walimu wanne. Hata pale RAS anapotaka kufanya mgawazo wa watumishi mkoani anakosa rasilimali fedha ukizingatia katazo linalomkataza RAS kuhamisha mtumishi bila ya kuwa na fedha. Hivyo, naishauri Serikali kutenga fedha mara kwa mara kwa ajili ya kufanya mgawazo kwa walimu hata pale panapokuwa na umuhimu wa kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kitengo cha Udhibiti Ubora wa Elimu ni kitengo muhimu sana. Ili kuwe na elimu bora, naishauri Serikali kuongeza uwekezaji katika kitengo hiki kuanzia ikama ya watumishi hadi vitendea kazi ikiwa ni pamoja na magari. Mfano, katika Halmashauri yangu ya Liwale, kitengo hiki hakijawahi kuwa na gari japokuwa mtawanyiko wa kata na shule zetu ni mkubwa sana. Zipo shule hazijawahi kuona Wakaguzi kwa zaidi ya miaka mitano. Ukiuliza watasema hawana usafiri hata wa pikipiki. Hivyo, naiomba sana Serikali kutupatia gari litakalowawezesha wakaguzi na idara ya elimu kwa ujumla. Hadi sasa Idara ya Elimu Msingi na Sekondari wote hawana magari, hali ni mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ikaitazame Liwale kwenye Idara ya Elimu ili tutoke kwenye kuburuza mkia kwa Mkoa wa Lindi na Taifa kwa ujumla.