Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. LOLESIA J. M. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kushukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye hotuba hii. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kazi nzuri. Nimpongeze Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watumishi wote wa Wizara. Hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeelezea kwa undani utekelezaji wa miradi mbalimbali kitaifa iliyofanyika katika mwaka wa fedha 2018/2019. Nimpongeze sana kwa utekelezaji mzuri uliofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Wizara ni juu ya uimarishaji wa elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi. Serikali ianzishe vyuo vya ufundi vyenye ubora ili watoto wakihitimu wawe na uwezo wa kujiajiri moja kwa moja. Kwa kuwa Sera ya Taifa inazungumzia juu ya kuwa na Chuo cha VETA kila Wilaya, nashauri sana sera hii itekelezeke kwa vitendo nikimaanisha kila wilaya ipate Chuo cha VETA chenye ubora. Hii itasaidia sana wahitimu wa darasa la saba na wahitimu wa kidato cha nne wapate ujuzi ili hatimaye wajiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali irudishe mfumo wa zamani ambapo katika shule za msingi na shule za sekondari kulikuwa na elimu ya kujitegemea na shule zilikuwa na michepuo mbalimbali mfano kulikuwa na shule za sekondari zenye mchepuo wa biashara, zingine mchepuo wa kilimo, elimu hii ilikuwa inawajengea uwezo mkubwa wanafunzi kujitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naipongeza Serikali kwa ujenzi wa Chuo cha VETA katika Mkoa wa Geita. Kwa kuwa uhitaji wa elimu ya ufundi ni mkubwa sana, Serikali ione umuhimu wa kukamilisha mapema iwezekanavyo kwani katika Mkoa wa Geita na Wilaya zake hatuna Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukamilika mapema kwa VETA Mkoa itasaidia kupunguza changamoto katika mkoa wetu. Ujuzi wa ufundi stadi unahitajika sana katika kufikia azma ya Serikali ya Viwanda vilevile katika kuongeza kipato na kupunguza umaskini kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.