Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Zainabu Mussa Bakar

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZAINAB M. BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunitunuku zawadi ya kusimama hapa. Pili, naunga mkono maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaelezea suala la bajeti kushuka. Bajeti ya Wizara ya Elimu imeshuka sana wakati tunaiangalia Wizara hii kama ni Wizara mama na dira ya Wizara zote. Nasema hivyo kwa sababu Wizara hii ndiyo inayozalisha madaktari, mameneja, wahandisi na viongozi leo tunaipunguzia bajeti. Mwaka jana tulitenga 1.4 mara hii tumeshuka mpaka 1.3. Hivi kweli tupo tayari kuisaidia Wizara hii ambayo ndiyo kioo cha nchi hii ama tunaibeza tu? Kwa sababu mfumo wowote mzuri ndiyo utatufanya tupate matokeo mazuri na wanafunzi na viongozi bora lakini tukiendelea hivi tutaendelea kuwatumbua viongozi kutokana na kwamba hatujaweka ufanisi mzuri katika suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna vitendea kazi kutokana bajeti yetu tumeiweka katika upungufu huu. Tutaendelea kukosa madawati, maabara na vyumba vya kusomea wanafunzi kutokana na kushuka kwa bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu ndiyo tegemeo la nchi hii lakini leo tunawazalilisha au wako chini kabisa. Tunashindwa kuwaongezea mishahara ambayo itawakidhi kwa mahitaji yao ya kila siku. Mwalimu huyo huyo asomeshe mtoto wake na anahitaji pesa za matumizi mengine mwisho wa siku anakuwa na msongo wa mawazo na ndiyo maana anafanya mambo mengine ambayo hayaeleweki. Kwa hivyo, tunakuomba Mheshimiwa Prof. Ndalichako uwaangalie kwa jicho la huruma walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea na suala la uhamisho. Uhamisho wa ualimu imekuwa ni kilio. Tunawatenga walimu na wenza wao kwa kipindi cha muda mrefu, waonane likizo hadi likizo, hiyo siyo sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwalimu yupo Kigoma mwenza wake anafanya kazi Dar es Salam, hatuoni kwamba tunawazalilisha na kwamba Serikali au Wizara hii inavuruga ndoa za walimu wetu? Kwa nini tusiwape uhamisho wakawa karibu na wenza wao? Hivi ni Serikali ya Mapinduzi ndiyo mkakati wake kuona ndoa za watu zinavurugika? Nataka unipe majibu kuhusu uhamisho wa walimu ambao wenza wao wako mbali kama watapewa uhamisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuja kwenye suala la kubadilishwa kubadilishwa kwa mitaala hili limekuwa ni suala la kawaida na kwamba hakufanywi tafiti za kina na wala walimu hawashirikishwi katika masuala haya ya kubadilisha mitaala, jambo ambalo linapelekea wanafunzi wetu kufeli sana. Kwa mfano mzuri nikija kule kwetu Zanzibar sidhani kama walimu wa Zanzibar wana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)