Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hotuba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Tunduru Kusini kuna Tarafa tatu, Kata 15, vituo vya Polisi vinavyofanya kazi ni viwili tu. Kwa kuzingatia kuwa Tunduru Kusini inapakana na Mto Ruvuma katika mpaka wa Msumbiji. Hivyo, tunaomba Kituo cha Polisi katika Kata ya Lukumbule, katika eneo la Lukumbule pamoja na Kituo cha Uhamiaji ili kudhibiti watu wa Msumbiji wanaoingia Tanzania bila kufuata utaratibu na sheria za nchi. Vilevile tunaomba Kituo cha Polisi katika Kata ya Misechela, Kijiji cha Misechela na katika Kata ya Namasakata katika Kijiji cha Namasakata ili kuwarahisishia katika Kata ya Mchateka ambayo ina idadi kubwa ya wakazi. Tunaomba kituo cha Polisi katika Kijiji cha Mchateka Kati ili kuhudumia wananchi wa Kata hiyo. Lengo la kuomba Vituo hivi vya Polisi ni kupunguza kero kubwa kwa wananchi kutembea mwendo mrefu kufuata huduma ya Kipolisi.

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Namasakata hamna hata kituo kimoja cha Polisi. Tarafa hiyo ina Kata tano yaani Ligoma, Misechela, Tuwemacho, Mchuruka na Namasakata na hamna kituo cha Polisi hata kimoja. Huduma ya Kipolisi wataipata Makao Makuu ya Wilaya ya Tunduru Mjini.

Mheshimiwa Spika, sambamba na vituo vya Polisi, tunaomba vituo vya Uhamiaji ili kupata huduma za visa kwani maeneo niliyotaja yamepakana na Msumbiji hivyo kuna mwingiliano wa wananchi wa Msumbiji na Tanzania, lakini wananchi wa Tanzania wakienda Msumbiji wanapata shida sana kwa vile Askari wa Msumbiji wananyanyasa sana Watanzania kwa kuwapiga hatimaye kuwafunga na kuwanyang’anya mali zao wakati wao wakija Tanzania hawanyanyaswi hivyo. Kwa hiyo, tunaomba vituo vya Uhamiaji ili wananchi wa Tanzania wapate visa za kwenda Msumbiji kwa ukaribu zaidi badala ya kufuata Tunduru Mjini ambapo ni zaidi ya kilometa 80 kutoka mpakani.

Mheshimiwa Spika, pamoja na vituo vya Polisi, tunaomba Serikali kuangalia uwezekano wa kujenga nyumba za Askari katika Kituo cha Polisi Walasi na Kituo cha Polisi Masuguru ambao karibu wote wanakaa uraiani na hata Askari waliopo Makao Makuu ya Polisi Wilaya hawana makazi ya kudumu. Kuna nyumba 300 za Polisi ziliungua moto miaka mitano iliyopita lakini hadi hivi leo nyumba hizo hazijajengwa. Tunaomba nyumba zile zijengwe ili kupunguza adha ya makazi kwa Askari wetu wanaofanya kazi katika mazingira magumu sana ya makazi kwa kuchanganyika na wananchi ambapo ni hatari kwa maisha yao.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, Serikali iongeze bajeti ya fedha kwa ajili ya kununua mafuta kwa ajili ya magari ya Polisi. Ni aibu kubwa sana kwa Jeshi la Polisi na Uhamiaji kuwa ombaomba wa mafuta kwa ajili ya kuendesha shughuli zao za kila siku na ndiyo maana Polisi wakiitwa mahali kuna uhalifu hawafiki kwa wakati kwa sababu ya kukosa mafuta ya kufika eneo la tukio. Wakati mwingine wanalazimika kuomba mafuta kutoka kwa mtoa taarifa ili waweze kufika eneo la tukio.