Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ili nami niweze kuchangia. Nianze kwa kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayofanya, tunajuwa wanafanya kazi kubwa lakini vilevile wanafanya kazi hiyo katika mazingira magumu, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitazungumzia mambo mawili, kwanza nizungumzie hali ya uraia kule Mkinga. Wilaya ya Mkinga ni wilaya inayopakana na nchi jirani ya Kenya na kwa muda mrefu sasa tumekuwa na tatizo ambalo limekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wangu, kero ya uraia. Bahati nzuri jambo hili unalifahamu lilifika Mezani kwako ukataka nikupe ufafanuzi tukafanya hivyo lakini jambo hili mpaka leo bado halijapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, ipo changamoto kubwa sana kwa wananchi wangu wa makabila ya Wataita, Wakamba, Waduruma, ambayo haya ni makabila ambayo unayapata vilevile upande wa pili wa nchi jirani ya Kenya. Hili jambo la kuwa na makabila ambayo unayakuta kwenye nchi mbili tofauti si jambo geni. Kwenye maeneo yetu ya mipakani hili ni jambo la kawaida lakini wananchi wangu kule Mwakijembe wanapata usumbufu mkubwa sana kwa kuambiwa siyo raia kwa sababu tu wanaasili ya makabila ya Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili siyo sawa kwa sababu wananchi hawa wamekuwepo kwenye maeneo yetu kabla ya Uhuru. Wamekuwa wakitambulika kama raia wa Tanzania lakini imeingia sasa kadhia tulipoanza kuandikisha raia wetu, wale wananchi wote wanaoonekana wanamajina ya makabila haya moja kwa moja wanaambiwa siyo raia, hii siyo sawa.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri jambo hili nimeshawasiliana na Waziri tangu mwaka jana, nikamuomba ikiwezekana afanye ziara aje aone kadhia hii. Naamini muda bado upo na Waziri atajipanga ili tuje tutatue tatizo hili lakini kwa kweli ni jambo linalowaumiza sana wananchi wangu kwa sababu wananyimwa haki yao ya msingi ya kuchagua na kuchaguliwa kama viongozi lakini vilevile wananyimwa haki ya kushiriki kwenye shughuli nyingine za kimaendeleo kama wananchi halali wa Tanzania. Naiomba Serikali yangu ilifanyie jambo hili uharaka ili wananchi hawa wasione wananyanyasika katika nchi yao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni vitendea kazi. Wilaya yetu ya Mkinga baada ya kuanzishwa, pale Makao Makuu ya Wilaya hatuna kituo cha polisi. Kituo tunachokitumia kama kituo cha polisi kiko takriban kilomita 40 kutoka makao makuu ya wilaya, hili si jambo zuri. Naiomba Serikali ione umuhimu wa kujenga kituo cha polisi kama Makao Makuu yetu ya Polisi katika Wilaya ya Mkinga pale kwenye mji wetu mkuu wa wilaya pale Kasera.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa upande wa Tarafa ya Maramba ambayo hii inajumuisha kata 10 tuna jengo la kituo ambalo limechoka, jengo hili ni condemned lakini ndipo kilipo kituo chetu. Wananchi wamejitahidi kwa nguvu zao kujenga jengo la kisasa. Tunachohitaji ni msaada wa Serikali tuweze kumalizia jengo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali ifahamu kwamba tuna askari wale wanaohudumu katika kata 10 hawana makazi, hii haiwezi kuwa sana. Naiomba Serikali yangu iliangalie jambo hili na iangalie jambo hili ikijua kwamba maeneo haya ni ya mpakani. Sasa unapokuwa na kituo cha polisi kwenye kata kinachohudumia kata 10 lakini kiko kwenye jengo ambalo ni condemned, Mheshimiwa Waziri wewe unajua mambo ya kiusalama silaha na kadhalika, unajua nisiendelee kwa details hapa, lakini tuna changamoto kubwa tunaomba msaada huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vipo vitendea kazi vingine ni changamoto kubwa kwa askari wetu kule Mkinga ambao wanafanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha hali ya ulinzi na usalama katika maeneo ya mpakani inakuwa shwari. Tunawaomba sana muwaangalie kwa jicho la pekee. Gari moja kwa eneo lile halitoshi, lile gari lililoko kwenye Kata ya Maramba ni bovu. Tunaomba msaada wetu tuweze kupata gari ambalo litasaidia kulinda usalama kwenye maeneo yetu ya mipakani.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nawashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)