Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Machano Othman Said

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. MACHANO OTHMAN SAID: Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Pili nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uhai na uzima na kuweza kufika leo katika Bunge letu Tukufu. Pia napenda kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa uchapakazi wao, wamefanya kazi nzuri katika kulitumikia Taifa kwa kipindi chote tangu Mheshimiwa Waziri ameteuliwa.

Mheshimiwa Spika, nitazungumzia maeneo matatu ambayo ni Polisi, Uhamiaji na NIDA. Kwanza nianze na Jeshi la Polisi na kwa upande huu pia niwapongeze sana polisi na zaidi kwa upande wa Zanzibar Kamishna wa Polisi kwa kazi nzuri ambayo wameifanya. Kwa miaka karibu mitatu sasa hali ya utulivu katika Mji wa Zanzibar na maeneo mengine ni nzuri. Maeneo ya ujambazi yamepungua sana na vitendo vya uhalifu pia vimepungua, tatizo ambalo bado lipo kwa polisi na kwa upande wa Zanzibar ni mapambano dhidi ya madawa ya kulevya, tunamuomba Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Maafisa wao waendelee kupambana na suala hili ambalo ni janga la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwa upande wa polisi yapo matatizo ambayo tunaomba wayatatuwe na moja ya tatizo kubwa la polisi ni makazi miundombinu ya makazi kwa polisi kwa upande wa Zanzibar bado ni madogo sana. Katika maeneo mengi ya vituo vya polisi, askari polisi hawana makazi, wanakaa katika hali ngumu, lakini hata vituo vyenyewe vya polisi vimechakaa sana. Mfano, kwa Mkoa wa Mjini Magharibi ambao wananchi wa Zanzibar karibu nusu wanaishi Mjini Magharibi, hali ya vituo ni vichache na vichakavu sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tulifurahi sana Mheshimiwa Waziri alipofanya ziara Zanzibar na kuzungumza na Maafisa wa Polisi na tunaomba Mheshimiwa Waziri afanye tena ziara kutembelea baadhi ya maeneo ya vituo vya polisi ili ajionee hali halisi ya uwepo wa vituo hivyo katika hali mbaya. Tunashukuru kwamba wameanza kujenga nyumba za askari katika Kituo cha Polisi cha Fuoni, lakini waangalie na maeneo mengine zaidi ya Mkoa wa Mjini Magharibi ambapo hali ya uchakavu ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kwa polisi Zanzibar ni ukosefu wa vitendea kazi kama magari na uniform ambazo zinawakabili kwa muda mrefu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri, jambo hili nalo alifikirie sana na aweze kulipatia ufumbuzi zaidi magari katika maeneo ya vituo vya polisi.

Mheshimiwa Spika, nikitoka hapo, naomba nizungumzie Uhamiaji; namshukuru na kumpongeza Kamishna uhamiaji Zanzibar Ndugu Sururu kwa kufanya kazi vizuri sana, lakini naomba hapa nimshukuru Waziri wa Utawala Bora kwa tamko lake ambalo amelitoa hivi punde kuhusu kupandishwa vyeo kwa madaraja. Maafisa wengi wa Uhamiaji Zanzibar walikuwa wanalalamika kwamba wameshakwenda kozi kwa muda mrefu, lakini bado kwa miaka mitano hawajapandishwa vyeo. Nafikiri hili tangazo la Mheshimiwa Waziri leo litawapa nafuu na mategemeo kwamba hali hii itamalizika na wataweza kupandishwa vyeo kama ilivyo kawaida.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupandishwa vyeo na kuisifu Uhamiaji, ukizungumzia kwa ujumla Uhamiaji Tanzania tatizo ambalo naliona ni biashara ya binadamu. Biashara ya binadamu kila siku tunaisikia na tunaomba Serikali ijitahidi sana kukabiliana na changamoto ya biashara ya binadamu. Pia kuna uhaba wa wafanyakazi wa Idara ya Uhamiaji ambao hawajaajiriwa kwa kipindi cha miaka mitatu, minne hivi. Sasa baadhi ya Taasisi za kiaskari kama Polisi, Jeshi na wengine wamepata fursa za ajira, lakini wa Uhamiaji bado hawajapata nafasi za ajira, kwa hiyo, naomba nalo hili liangaliwe sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea naomba nizungumzie NIDA; Taasisi hii ina umuhimu mkubwa katika maisha ya wananchi wa Tanzania, kwa sababu ndiyo inashughulika na kutoa vitambulisho vya Mtanzania, vitambulisho vya Taifa lakini naomba sana Mheshimiwa Waziri na watendaji wako, hii NIDA naiomba sana ishirikiane na Wakala wa Usajili wa Zanzibar ambao nao wanatoa vitambulisho vya Mzanzibari, vitambulisho hivi vina umuhimu sana kwa watu wa Zanzibar na Watanzania kwa ujumla. Jambo ambalo lipo hivi sasa ni kwamba kama vile vitambulisho vya Mzanzibari havitambuliki, tukienda kwenye passport havitambuliki, katika usajili wa simu havitambuliki, kwa hiyo tunaomba NIDA wafanye mashirikiano ya karibu na Mamlaka ya Usajili wa Mzanzibari.

Mheshimiwa Spika, nataka kuzungumzia NIDA ni deni la JKU, Zanzibar Mamlaka hii ya NIDA inadaiwa karibu milioni 489 na JKU Zanzibar kutokana na ulinzi wa ofisi zao mbalimbali. Kule Pemba sehemu ya Micheweni wanadaiwa milioni 82, lakini ukija Ofisi Kuu ya Idara wanadaiwa milioni 222, Mwanakwerekwe wanadaiwa milioni karibu 110 na Gamba hivyo hivyo. Madeni haya yamemalizika tangu Julai, 2018, kwa hiyo tunamwomba Mheshimiwa Waziri akija hapa aje atueleze kuna mpango gani wa kulipa madeni haya ya JKU kwa upande wa NIDA.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja hii. (Makofi)