Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza wa hoja hii ya Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa siku hii ya leo.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabla sijaanza kutoa mchango wangu, naomba nitumie fursa hii kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa usikivu wake wa kujali mahitaji ya wananchi wanapomlilia katika shida zao.

Mheshimiwa Spika, ni wiki moja tu imepita tulipotoa kilio kwamba hali ya chakula ni tete katika Kanda ya Kaskazini na wananchi waliouza mifugo yao hata hawana pa kununulia chakula maana bei ya mahindi ilipanda mpaka shilingi 20,000/= kwa debe, lakini Mheshimiwa Rais alitoa tamko kwamba kwa kuwa tuna maghala ya Serikali yanayoweka chakula, wananchi waliouza mifugo yao, wapelekewe chakula kwa bei ya Serikali na chakula hicho kimefika. Naomba niishukuru Serikali, nimshukuru Waziri wa Kilimo na timu yake yote kwa ushirikiano waliotoa. Wanalongido wamefurahi, chakula kimewafikia, na hata wale walanguzi sasa wameshusha bei baada ya kuona kwamba Serikali sikivu imewaletea wananchi wake chakula. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa pongezi na shukrani hizo, nitasema mambo machache sana kuhusiana na hotuba ya Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa sababu mengi yameshasemwa na sipendi kurudia yaliyosemwa, lakini nina machache ya kusema kuhusu Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza na Jeshi la Zimamoto.

Mheshimiwa Spika, kwa Jeshi la Polisi, naungana na wenzangu waliotangulia kusema kwamba mazingira yao ya kuishi na kufanyia kazi ni duni. Serikali iwaangalie kwa jicho la karibu. Ukija kwa mfano katika Jimbo langu la Longido ukaenda katika Kituo cha Polisi kilichopo Kamwanga, wale Polisi wanaishi katika shacks; shacks ni kama banda la kuku. Kwa kweli sisi kama wananchi wa Longido pia tunajali hivyo vyombo vya usalama na hata tulijitolea kabisa tukajenga na Kituo cha Polisi ambacho kinakaribia kumalizika, lakini Polisi wetu hawana makazi.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri; na nilishaongea naye kwamba atuunge mkono kumalizia kile Kituo cha Polisi kipya kilichojengwa kupisha barabara ya lami inayounganisha Wilaya za Rombo na Siha na baadaye Longido.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Jeshi la Magereza, napongeza sana kazi wanayoifanya na uzaishaji ambao wameonesha. Pia nategemea kwamba baada ya kuanzishwa kwa Mobile Courts msongamano wa wafungwa utapungua. Pia nitoe rai kwamba kama zilivyoundwa na Serikali yetu sikivu, tume mbalimbali za kuhakiki masuala ambayo yalikuwa hayaendi sawa katika nchi hii, kwa mfano uhakiki wa watumishi hewa, wale wenye vyeti feki na watu wengi wakabainishwa, naomba pia tume iundwe na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuhakiki wafungwa waliosahauliwa ndani ya Magereza.

Mheshimiwa Spika, wako wafungwa ambao wametuhumiwa tu, ni mahabusu. Wamekamatwa kwa tuhuma za kuhujumu uchumi. Kwa mfano, katika Jimbo langu la Longido, kuna waliotuhumiwa tu kwamba wanajihusisha na biashara ya ujangili kwa sababu sisi ni Wilaya ya Wanyamapori na wanatupwa kule Gerezani, wengine wana mpaka miaka miwili; wanaitwa tu Mahakamani wanarudishwa, wanasema uchunguzi bado unaendelea.

Mheshimiwa Spika, naamini kwamba suala hili litapewa kipaumbele baada ya Mahakama kuongezewa wigo wa kuwa na Mobile Courts na Vyombo vya Usalama vifanye uhakiki wa uhalifu wao kwa haraka, wasikae Gerezani pasipo sababu kama mahabusu ambao hata hawajahukumiwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Jeshi la Zimamoto; ni ukweli usiopingika kwamba bado tuko nyuma sana katika kuendeleza Sekta ya Zimamoto na kunusuru maisha na mali za Watanzania wanaoweza kuathirika kwa majanga ya moto; na wilaya nyingi nchi hii ambazo nimeshazipita hazina miundombinu kabisa ya uzimaji moto; na katika Wilaya yangu ya Longido pia hatuna hata gari la Zimamoto.

Mheshimiwa Spika, naomba katika bajeti hii iongezwe fedha ya kuhakikisha kwamba kila Wilaya angalau inapata gani moja la Zimamoto maana tunapata majanga ya moto kila wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, sisi katika Shule yetu ya Sekondari ya Longido karibu kila baada ya mwaka mmoja au miwili tunapata janga la moto. Hata Kituo cha Polisi Longido mwaka 2018 nyumba ya Askari iliungua moto tukishuhudia; tunazima kwa mchanga na udongo, hatuna chombo chochote cha kuzimia moto. Naomba hilo liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, pia nikienda katika huduma za uhamiaji, napongeza Serikali kwa sababu ya huduma ya kielektroniki na kwa kutengeneza passports zilizokidhi hadhi ya Kimataifa na kuwa moja ya passports bora duniani; lakini niombe kutoa rai kwamba hizi paspoti za kielektroniki zitengenezewe mazingira ya kuwa rafiki kwa waombaji na Watanzania wote wenye haja ya kupata passport.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kwa sababu Watanzania wengi uwezo wao wa kutumia mitandao bado uko chini, hizi passports za muda mrefu ambazo mtu ukitaka kupata, mpaka ujaze fomu iende kanda, iende Makao Makuu; nasi watu tunaoishi mipakani tumekuwa tunategemea zaidi hizi hati za dharura tu. Unaona katika taarifa na hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameonesha kwamba idadi ya wasafiri wa dharura ni kubwa mno ukilinganisha na wasafari wa aina nyingine. Siyo kwamba kuna dharura ni kwamba ndiyo hati ya pekee ambayo ni rahisi kuipata mtu unapotaka kusafiri nchi ya jirani.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa sababu sasa hivi adha wanayopata wananchi wanaotaka kusafiri nchi ya jirani kwa biashara au kwa shughuli za kifamilia au kwa matibabu ni kubwa, maana kila akienda akirudi ile passport inayoitwa hati ya dharura ina-expire; akitaka kuomba nyingine labda ameambiwa arudi ndani ya wiki hiyo hiyo, mpaka apeleke tena zile nyaraka zote; apeleke birth certificate, apeleke sijui barua ya mtendaji na akirudi tena wiki ijayo anaitishwa tena back up ya zile documents zote.

Mheshimiwa Spika, nia ya Serikali najua kwamba ni njema, Waziri wa Mambo ya Ndani alishakuja akatoa elimu katika Jimbo langu, lakini naomba passport za muda mrefu, angalau zile za East African Community zirahisishwe wananchi waweze kupata katika ngazi ya Wilaya. Mtu akija, ajaze fomu, atoe vielelezo vyake, apewe passport ya muda mrefu kwa sababu naamini haki ya kuwa na passport ni haki ya kila Mtanzania mwenye kuwa na haja nayo.

Mheshimiwa Spika, pia naomba niongelee kidogo suala Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, vitambulisho hivi kasi yake ya kutoa ni ndogo mno, wananchi wangu wa Longido kuna waliopigwa picha za kupewa hivyo vitambulisho tangu mwezi wa Kumi mwaka jana lakini mpaka leo hawajapata.

Mheshimiwa Spika, pia niunganishe hapa kwa sababu ya ufinyu wa muda suala zima la kupatiwa hivi vitambulisho ili mtu aweze kuhakikiwa na line yake ya simu. Naomba kuuliza na Waziri anijibu baadaye atakavyohitimisha hoja, Mheshimiwa Waziri atusaidie kwa wale raia ambao siyo raia wa Tanzania lakini wapo nchini kihalali aidha kwa work permint au huku kwa sababu ni dependants, wao ni vitambulisho gani watahitajika kuonyesha ili line zao za simu zisifungiwe itakapofika wakati wa kuzifunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, niipongeze Wizara, Waziri wenyewe ambao ni mmoja ya Mawaziri wasikivu sana ambao mimi nimewafahamu katika Bunge hili, yupo tayari usiku na mchana kukuhudumia ukimpigia simu, nimpongeze yeye na timu yake yote kwa kazi nzuri waliyoifanya katika kuandaa hotuba ya bajeti na pia katika utendaji wao tunaouona katika vyombo vya kitendaji wanavyovitumia. Kazi yao ni nzuri, Mheshimiwa Waziri aendelee hivyo hivyo, tupo nyuma yake kum-support kwa sababu kazi anayofanya inawasaidia Watanzania kubaki salama, lakini tuendelee kuongeza bidii katika kupunguza urasimu na hasa rushwa katika Jeshi letu la Polisi.

Mheshimiwa Spika, polisi bado wanakula rushwa, naomba hata kwa sababu tumekuwa electrified hizo electronic agency zitumike tu kumsoma mtu anayefanya uhalifu kwa mfano barabarani akakutane na faini yake mbele ya safari na sio polisi kuanza ku-negotiate naye. Teknolojia imeendelea, kuna nchi ukienda unapigwa picha tu barabarani unatumiwa kwenye barua kwa sababu gari yako inajulikana, ni ya nani, unatumiwa barua ya madai na usipopeleka gari yako inataifishwa. Kwa hiyo, naomba pia sera hiyo ya kufanya Electronic Traffic Monitoring System iweze kuboreshwa zaidi, maaskari waondokane na hadha ya kusamisha wasafiri barabarani na kuanza kuwahoji na kupatana na hatimaye kudaiwa rushwa ndipo mtu aweze kwenda au vinginevyo atapigwa faini kubwa.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kiruswa.

MHE. DKT. STEPHEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kusema naunga mkono hoja na ahsante kwa kunipa nafasi. (Makofi)