Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Chief nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, leo nina jambo moja mahususi. Bahati nzuri mapacha wa wakimbizi tupo watatu hapa, mwenzangu amekwishaanza kuligusia. La kwanza nimpongeza rafiki yangu Mheshimiwa Kangi Lugola kwa kuteuliwa kuwa Waziri wa Wizara hii. Ni Wizara kubwa yenye changamoto nyingi, panataka utulize kichwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe darasa kidogo, mwaka 1972 kulitokea vita kwa wenzetu Burundi, enzi za utawala wa Mchombelo, kundi kubwa likakimbilia Tanzania wakati ule Waziri wa Mambo ya Ndani alikuwa mzee Maswanya, wakaangalia maeneo ambayo yana nafasi kwa hiyo wakaamua wakimbizi kundi kubwa liletwe Ulyankulu, Mishamo na Katumba, nasi tukasema njoo tuwasaidie katika hali ya kibinadamu, sasa tumekaa nao miaka 44.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014, Serikali ya Awamu ya Nne ikatoa uraia ikiwa tarehe 14 Oktoba, nami nikiwa Mwenyekiti wa Halmashauri, lakini kwa ahadi, wale waliokuwa wakimbizi wakaahidi kuwa watiifu kwa Serikali mbele ya Mheshimiwa Kikwete, kwa hiyo walipata uraia. Baada ya hapo kumekuwa na mazungumzo je, zifungwe kambi hizi zote tatu au ziendelee kuwepo? Bahati nzuri Kamati ya Ulinzi na Mambo ya Nje imejadili sana jambo hili. Mabunge yaliyopita ilifika hatua, kuna Wabunge humu walikuwa wanasimama humu kukataa watu hawa wasipelekwe katika maeneo yao, kwa sababu mkishawapa uraia ile sio kambi tena ya wakimbizi, ni sehemu halali ya kuishi au kambi ifungwe na watu wahame. Analosema Mheshimiwa Kakoso, wapo watu walikataa Utanzania, walikataa kurudi Burundi, wanataka nchi ya tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya kwa taarifa yenu wakimbizi wa uraia wa Ulyankulu wanazaliana sana kuliko eneo lolote Tanzania. Kwa maana hiyo tunapongea hapa ile idadi ya wakimbizi waliokuwa wamebaki hawana uraia imekwishaongezeka, lakini Serikali yetu inapata kigugumizi kila wakati, ukiwagusa ndugu zangu wa TAMISEMI ndio kabisa hawataki kuleta majibu ya kueleweka, bado unamfuata Kadutu kagombee, utagombeaje kama watu hawahudumii watu wako. Watu wale wananipenda sana, lakini hawajatekelezewa, huduma za Serikali hazifiki kule. Sasa kwa nini Serikali isiwe na kigugumzi juu ya jambo hili, kwani wakisema kambi imefungwa, bahati mbaya kwenye kitabu cha hotuba ya Waziri eneo lile la Idara ya Wakimbizi limeguswa kidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu 70% ndio wapigakura wa Ulyankulu, ndio wapigakura waliomchagua Kadutu na Magufuli, lakini wakakataliwa kuchagua Madiwani, lakini ajabu kwa Kakoso kule na kwa Mbogo wamechagua Madiwani. Hebu waniambie hasira waliyonayo itakuwaje? Hivi viongozi hawalioni hili? Serikali hawaoni? Tunaenda kwenye uchaguzi wa Serikali za mitaa, mle ndani kuna Serikali mbili; kuna mkuu wa makazi ana mamlaka yake, halafu TAMISEMI inaingia kwa kuviziavizia, Serikali yetu halafu tunaingia kwa kuviziavizia, ya wapi hiyo? Kwa nini tusiwe na mamlaka kabisa tunaviziavizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa lakini mle ndani kuna Serikali mbili. Kuna Mkuu wa Makazi ambaye ana mamlaka yake halafu TAMISEMI inaingia kwa kuviziavizia. Serikali yetu tunaingia kwa kuviziavizia, kwa nini tusiwe na mamlaka kabisa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niseme Serikali ifike mahali ieleze, kama tunadhani Mheshimiwa Kikwete alikosea, tu-review uamuzi kwa sababu wapo watu walikuwa tayari kurudi Burundi lakini walipopata fursa ya kuchagua kurudi Burundi au Tanzania wakasema sisi ni Watanzania. Hata hivyo, kuna jambo ninyi hamlijui, hawa wenzetu tayari wamo kwenye Wizara zenu, iwe Wizara ya Fedha, Mambo ya Ndani, TAMISEMI na ninyi mnakaa nao hamjui kumbe huyu Mrundi, huyu hivi, huyu hivi, wamo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu mnasema mna Idara nzuri ya Usalama wa Taifa, Polisi lakini mnakaa nao. Pakitokea jambo Ulyankulu tayari, ndiyo watu wanasema huku bado hapajakaa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimesema nitachangia suala hilo hilo tu, niwasihi sana Serikali, Kamati ya Ulinzi na Mambo ya Nje mbona imesema na imeshauri muda mrefu, kwa nini tusiwe na uamuzi? Tunafunga kambi ili wale ambao wamejidai kutafuta nchi ya tatu waondoke tubaki na wale walio tayari basi! Baada ya hapo tutakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwani ukiwaambia chagueni Diwani kuna tatizo gani? Mbona Kadutu wamemchagua? Mbona Mheshimiwa Rais Magufuli wamemchagua? Kuna shida gani wao wasichaguane? Zamani watu walikuwa wanasema, ooh, misitu, sasa misitu kwenye kura, ni jambo la ajabu hili. Jamani tutafute sababu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)