Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

kunipa nafasi hii na ni mara yangu ya kwanza kwenye bajeti hii ukiacha maoni ya Kamati niliyoyatoa hapo mbele kuchangia kwenye bajeti ya mwaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana na kumpongeza sana Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa hotuba nzuri iliyojaa takwimu ambazo tunazihitaji, na mimi sihitaji kurudia takwimu hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna Taifa lililoendelea bila viwanda. Viwanda kwanza vinatumia teknolojia, lakini viwanda vinazalisha teknolojia kwa ajili ya sekta nyingine. Kama viwanda ndiyo vinavyozalisha teknolojia ya kuboresha sekta nyingine, itakuwaje nchi hii iondokane na umaskini bila ya kuwa na msingi wa viwanda? Kwa hiyo, naishukuru Serikali kupitia Mpango wa miaka mitano kufanya msingi wa maendeleo uwe ni viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na umuhimu wa viwanda, mimi nilisomea uchumi wa viwanda, maisha yangu mengi sana nilifanya kazi viwandani kama Ofisa mdogo mpaka nikawa Meneja Mkuu. Siwezi hata siku moja nikaongelea maendeleo bila viwanda. Napenda kusema kwamba uendelevu wa viwanda unategemea sana sekta ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimondiyo inayotoa chakula kwa wale watakaofanya kazi viwandani. Sekta ya kilimo ikiongeza tija ndiyo itakayoleta ajira kwenda viwandani, ikisaidiana na sekta ya elimu. Kwa hiyo, ndugu zangu, hatuwezi tukaongelea maendeleo ya viwanda na msingi wa uchumi wetu na maendeleo yetu kama hatutatilia nguvu sana sekta ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo ili iweze kutekeleza wajibu wake katika kuendeleza viwanda, ni lazima iwe ni kilimo cha kisasa. Tutumie zana bora na kisasa, tutumie mbolea na mbegu za kisasa; tutumie viwatilifu, lakini hatimaye ni viwanda ambavyo vitaongeza maisha ya malighafi na chakula kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri, ninampongeza sana.
Kwa hiyo, sisi wote ili tuweze kui-support Serikali au kuipa msukumo kwa msingi huu wa viwanda ili tufikie uchumi wa kati na wa viwanda, tukubaliane kwamba bila ya kuongeza bajeti kwenye kilimo, tusahau maendeleo ya viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusema kwamba wakati wa ukoloni mnyororo wa thamani wa mazao ya kilimo ulivunjika nchi hii. Tulikuwa tunakula tusichozalisha na kutumia tusivyozalisha na tunapeleka nje vitu ambavyo tungepaswa vitumike kwenye viwanda vyetu. Sasa ni lazima turudishe mnyororo wa thamani ya mazao ya kilimo. Namna moja ya kurudisha mnyororo huu ni kupitia viwanda, kwasababu baada ya kufanya kazi mashambani, lazima mazao yale yatakayozalishwa na wakulima yasipopata masoko viwandani ni sawa na kutupa shilingi chooni. (Makofi)
Kwa hiyo ndugu zangu, wakati tunakazania sana kilimo, namna moja ni kukazania viwanda ambavyo vitachakata au vitasindika mazao ya kilimo. Na mimi naomba Bunge hili liazimie kwamba viwanda ambavyo tutaanza navyo ni hivi ambavyo vitakuwa na uhusiano wa karibu na kilimo ambavyo vitaipa kilimo malighafi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hivyo waliotangulia kutoa mchango kwa viwanda wamesema miundombinu ni jambo muhimu, na mimi naungana nao kwamba bila miundombinu viwanda haviwezi vikaendelea. Ndiyo maana hapa katikati kutokana na ukosefu wa umeme hatukuweza kuanzisha na kuendeleza viwanda vingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Muhongo aangalie sana mgao wa umeme kuelekea kwenye viwanda kama tunataka kuwa na viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niongelee jambo moja; ndugu zangu, kuna viwanda mama, kuna viwanda vya kati na kuna viwanda vya kuchakata. Bila viwanda mama hatuwezi kuwa na viwanda vingine. Kwa hiyo, napenda kwa muda uliobaki niongelee umuhimu wa Liganga na Mchuchuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Liganga na Mchuchuma ni viwanda mama. Mchuchuma itatoa makaa kwenda kwenye mradi wa chuma. Kwa hiyo ndugu zangu, tuna jambo moja ambalo Wabunge wengi hawalifahamu kuhusu chuma cha Liganga. Chuma cha Liganga siyo kama maeneo mengine ya migodi ya chuma ina kitu kinaitwa mchanginyiko wa madini mengine ambayo kama huna teknolojia sahihi huwezi ukapata chuma safi kutoka Liganga. Kwa hiyo, siyo rahisi kupata wawekezaji ambao wana ujuzi huo, naomba mjue hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana tutoe msukumo kuanza utekelezaji wa mradi huo. Ilituchukua muda mrefu kupata mwekezaji wa Liganga; na naomba niseme kwamba nilishawahi kuwa Waziri wa Viwanda ili mjue kwamba ninaposema hivyo, nasema mambo ambayo nafahamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipotangaza tender ya Mchuchuma, ilituchukua muda mrefu kupata teknolojia sahihi. Teknolojia hiyo watu wengi wanaipiga vita ili sisi tuendelee kutokuwa na chuma tuagize nje. Mjue kwamba kuagiza chuma nje itakuwa ni ghali kwa viwanda vyetu kwa sababu mazao ya chuma ni mazito na kwa hiyo ni lazima zitakuwa na gharama ya kuleta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna nchi yenye bahati kama Tanzania, Liganga na Mchuchuma ni mwendo mfupi tu! Kwa hiyo, tutakapotengeneza chuma, makaa ya mawe tunayoyahitaji yatakuwa pale karibu. Naomba sana tupiganie mradi wa Liganga uanze mapema inavyowezekana kama kweli tunataka kuwa na viwanda Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka tuwe na viwanda na kilimo bora, tukazanie viwanda vya mbolea vile vile. Tuna gesi lakini wale wanaoleta mbolea kutoka nje, hawataki tuwe na viwanda vya mbolea. Ninawaombeni sana hilo mlijue. Mtwara ina gesi na mambo yanayowezekana tuyafanye sasa, tuanzishe viwanda na hivi ndivyo vinaitwa viwanda mama. Kiwanda cha Chuma, Kiwanda cha Mbolea na mashamba ya mbegu ndiyo yatakuwa ni msingi wa uchumi wa kati wa viwanda. Tukifanya hivyo, tutafanikiwa na mpango huu wa miaka mitano au utabaki kwenye vitabu kama ilivyokuwa muda uliopita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoka mbali, sasa hivi nimetoka Hanang, naomba niwakumbuke watu wa Hanang tena kuendelea kuwashukuru sana kwa ajili ya kunipa kura na nitaendelea kuwajibika kwao. Naomba ushirikiano wa dhati na ninaomba ushirikiano wa Wizara ya Viwanda na Bunge hili ili kweli nchi hii iwe nchi ya viwanda na uchumi wa kati kupitia kilimo cha kisasa na haiwezi kuwa kilimo cha jembe. Ahsanteni sana na Mungu awabariki.