Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Eng. Christopher Kajoro Chizza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buyungu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ENG. CHRISTOPHER K. CHIZA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote kwa kuleta hotuba nzuri Bungeni.

Mheshimiwa Spika, Kampeni ya Uzalendo yenye kaulimbiu “Kiswahili Utashi Wetu, Uhai Wetu” imenigusa sana. Umuhimju wa lugha unaonekana siku zote katika kufikisha taarifa sahihi kwa walengwa. Lugha isipoeleweka, hata ujumbe unaotumwa haufiki vizuri na wakati mwingine inawezekana kusababisha madhara.

Mheshimiwa Spika, watoto wadogo ni wepesi kujifunza lugha, wakifundishwa lugha vizuri wanadaka mafundisho haraka na kutumia mafundisho hayo katika maisha yao ya kawaida. Ili kuwajengea uwezo watoto wetu ni lazima lugha fasaha ya Kiswahili itumike katika mafundisho, mihadhara, makongamano na kadhalika. Kuna neno kama “NANILII” ambapo vijana wengi hata wa shule za sekondari na vyuo vikuu wanalitumia sana, mimi silipendi. Katika kuhamasisha uzalendo wetu, ni muhimu sana kutumia lugha fasaha ya Kiswahili kutoa mafunzo kwa vijana wetu katika shule, vyuo na wahariri wa magazeti na kadhalika ili kupeleka ujumbe sahihi kwa umma.

Mheshimiwa Spika, Muungano wetu. Bunge hili kupita mjadala wake katika bajeti ya Makamu wa Rais limedhihirisha kwamba kuna haja ya kutoa elimu ya Muungano kwa watu wote (elimu kwa wanafunzi wadogo na watu wazima) ili dhana ya Muungano ieleweke vizuri kwa watu wote. Nashauri Wizara hii ishirikiane na Wizara inayoshughulikia Muungano ili kuratibu mafunzo ya uzalendo, ukiwemo Muungano wetu kwa watu wote. Katika hili, lugha fasaha ya Kiswahili ni lazima itumike vizuri, vyombo vyote vya habari vitakavyoshiriki vielekezwe kutumia Kiswahili fasaha katika kufikisha ujumbe kwa walengwa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.