Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kwa kunipa nafasi kuzungumza machache kuhusu Wizara hii ya Habari, Utamaduni na Michezo. Kwanza, nitazungumzia kuhusu utamaduni. Watanzania tuna tamaduni zetu za asili, tamaduni ambazo zilikuwa zinatuonesha kama kweli sisi Watanzania, lakini sasa hivi hizi tamaduni zinapotoshwa sana kwa kuiga mambo ya kimagharibi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, pale Tanga kuna makabila katika Mkoa wa Tanga; kuna Wabondei, Wasambaa, Wazigua, Wadigo, tuseme ndio wenyeji wa Mkoa wa Tanga na wana ngoma zao nzuri tu; wanacheza ngoma zao vizuri, lakini utakuta ngoma hizi sasa hivi zinapotoshwa katika ile michezo yake ya kiasili.

Kwa mfano, katika Jiji la Tanga kuna ngoma inaitwa Baikoko. Yaani ukitaja ngoma ya asili ya Tanga ni Baikoko. Nataka kuwaambia ngoma ya Tanga ya asili siyo Baikoko, ile Baikoko ni ngoma ambayo inapotosha sana watoto na kizazi hiki tulichonacho kwa sababu ile ngoma ni matusi matupu mwanzo mwisho. Matusi na watu kukatika katika, yaani mtu kukatakata mauno ambayo hayana maana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi mtu ukimwambia utamaduni anaona labda kusimama na kukatikakatika inakuwa ndiyo utamaduni. Kumbe akiimba ule wimbo ukiwa una ujumbe fulani utawafikia watu, watu wakauelewa ule ujumbe, ndio utamaduni wetu.

Mheshimiwa Spika, pia mfano mwingine kuna ngoma ile ya Hiyari ya Moyo, nilipokuwa mdogo, tulikuwa tunakwenda Tanga kuangalia ile ngoma. Mimi nilikuwa naona ngoma ya Hiyari ya Moyo wanacheza tu wanatingisha mabega, lakini sasa hivi mpaka mtu anakatika kabisa mpaka…

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, kama mtu anaangalia yaani ile ngoma…

SPIKA: Mheshimiwa Nuru pokea taarifa.

MHE. ALLY K. MOHAMED: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa mzungumzaji, huu ni utamaduni wa kukatika viuno, sasa nashangaa anasema wanakatika viuno. Hivi tuulizane humu ndani ya Bunge, kuna watu wasiokatika viuno?

SPIKA: Mheshimiwa Nuru vipi, mimi sijamwelewa lakini labda umemwelewa.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Aaa.

SPIKA: Haya endelea Mheshimiwa Nuru labda mwenzangu umemwelewa, pokea taarifa.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, taarifa siipokei kwa sababu Mheshimiwa Keissy naye anapenda kujipitisha pitisha, samahani kama panya, panya akitaka kutajwa ajipitisha kwa watu.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee na mchango wangu. Kwa hiyo, mimi ninachosema, hebu tujaribu turudi kwenye tamaduni zetu…

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Turudi kwenye tamaduni zetu za kizamani, tufanye…

SPIKA: Samahani Mheshimiwa Nuru, taarifa nyingine unapata. Mheshimiwa Waziri Dkt. Kigwangalla tafadhali.

T A A R I F A

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge anayesema hapa Bungeni kwamba utamaduni sio kitu static, utamaduni ni dynamic unabadilika kutokana na nyakati. Kwa hivyo, utamaduni wa watu wa Tanga hata mimi bibi yangu anatokea Tanga, Machui, umeendelea kubadilika zama na zama ndio maana leo hii hata muziki upo unaoitwa muziki wa kizazi kipya ambao wanaimba akina Sugu na Profesa Jay.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, utamaduni unabadilika, hata lugha ya Kiswahili ukitaka kutafuta lugha ya Kiswahili ni nini imetoka wapi, ni lugha imeibuka zama hizi za miaka hii ya 1900, lakini haikuwepo, sio lugha ya asili. Kulikuwa na makabila zaidi ya 128, lakini yanaunganishwa na utamaduni mmoja wa lugha ya Kiswahili. Kwa hivyo, napenda afahamu kwamba utamaduni sio static ni kitu dynamic.

SPIKA: Endelea Mheshimiwa, anakwambia tu mambo yanabadilika, hayo unayoyaona leo ndio yenyewe.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, asante na ndio kanipeleka mbele ngoja niende mbele halafu nitarudi nyuma, ndio hayo nilikuwa mengine nataka kuchangia. Sasa hivi Watanzania tunachanganya lugha ya Kiingereza na Kiswahili, tunatakiwa tukinyooka kwenye Kiswahili twende kwenye Kiswahili tu tusichanganye lugha Kiswahili na Kiingereza hapana, tunapoteza uzalendo wetu na Utanzania wetu. Tuzungumze lugha moja tu, sisi tunasema tunazungumza Kiswahili ni lugha yetu ya Taifa, tusichanganye maneno.

SPIKA: Anasema tusichanganye changanye maneno Waheshimiwa, unazungumza, mara mother tongue sasa inakuwa tabu. (Kicheko)

Mheshimiwa Nuru endelea.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Vile vile nikizungumzia kuhusu muziki wa kizazi kipya, kweli tunaupenda muziki wa kizazi kipya, lakini na huo muziki wa kizazi kipya tuuangalie je, ukoje? Je, Wizara kama Wizara au BASATA je, inazihakiki zile nyimbo? Mfano tukiimba sijui nyege nyege Nyegezi kwetu Mwanza Nyegenzi, wimbo kama huu…

SPIKA: Mheshimiwa Nuru unavunja Kanuni. (Kicheko)

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, samahani.

SPIKA: Endelea Mheshimiwa.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Kwa hiyo, tunatakiwa tulete nyimbo ambazo zina mantiki, zinapendeza mpaka anayezisikia pia pale alipo hata kama alikuwa anaandika atachezesha hata mkono kuona kuwa ule wimbo umemwingia. Kwa hiyo, nyimbo tunazoziimba tunataka nyimbo za kizazi kipya lakini nyimbo ziwe nyimbo zenye mafundisho mazuri sio nyimbo ambazo zinaleta maana mbaya mpaka watoto wanaozisikiliza haziwasaidii chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zamani kulikuwa na nyimbo zenye mafunzo, tulikuwa na akina Mwinamila walikuwa wakiimba mpango wa pili wa maendeleo, unasema, kuleni kuku, mayai, mboga, samaki, maziwa; kuleni chakula bora cha kujenga mwili na kulala kwenye nyumba bora, si ndio? Tulikuwa tunafundishwa kuwa tunatakiwa tule chakula na wakati huo huo tulale kwenye nyumba ambazo ni bora, lakini leo nani kamwaga pombe yangu, nauliza. Sasa hiyo jamani kweli tutakuwa, kwa hiyo tutakuwa hapo hatufanyi… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Sugu uende ukawaeleze wenzako, huu ndio ujumbe, ukaeleze kundi lako huko. (Kicheko)

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, Ninachoomba twendeni turudi kwenye tamaduni zetu za asili japokuwa kuna nyimbo za kizazi kipya, lakini zile nyimbo za kizazi kipya ziwe na nyimbo ambazo maudhui yake yanalenga kuwajenga wale wanaozisikiliza.

Mheshimiwa Spika, pia napenda kuzungumzia kuhusu Serikali kuona umuhimu tuwe na shule zetu maalum za wanafunzi wenye vipaji maalum yaani tuwe na shule ambazo tutawapeleka kweli wanasoma masomo mengine lakini wakati huo huo anaendelezwa kimichezo kama ni bondia, mchezaji mpira, labda ni muigizaji, vyovyote inavyokuwa vile.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunawajengea ile shule na wanakwenda pale, kwa hiyo wakimaliza pale, tunapata wanafunzi ambao ni cream kwa kuwapeleka mahali na kuwa wanashiriki katika kuliinua Taifa letu kwa sababu michezo ni afya na vilevile michezo ni ajira.

Kwa hiyo, tukipata watu namna ile tunaweza tukaendelea, kama wenzetu Nigeria walivyowekeza, akina Kanu wale walikuwa wapo kwenye shule za vipaji maalum mpaka leo tumeweza kupata wachezaji wazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini sio kwa umuhimu wake, Mheshimiwa Naibu Waziri alikwenda Tanga kuweka jiwe la msingi katika eneo ambalo litajengwa kiwanja kikubwa sana cha michezo. Ninachoomba sasa hivi Serikali angalau ijaribu kujenga uzio kwa sababu wananchi wanajaribu kusogea na mwisho ule uwanja utamezwa, utakuja kukuta wengine watakwambia wanadai fidia walipwe ili waweze kupisha ujenzi wa kiwanja. Kiwanja kile kama kitajengwa kitakuwa kizuri na kitapendeza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Nuru.

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)