Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017- Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami naomba nichangie hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda kwa kuanza kwa pongezi kwake kwa maandalizi mazuri ya hotuba iliyosheheni mpangilio mzuri unaoonesha azma ya Serikali kutupeleka katika uchumi wa viwanda. Nimefurahishwa na suala zima la kuangalia umuhimu wa kuzingatia miundombinu muhimu, wezeshi kwa ajili ya kuanzisha viwanda au kuviendeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka na mimi niongezee hapo kuwa kwa sasa hivi kwa uzoefu tuliokuanao huko nyuma, kila Wizara inafanya kazi peke yake. Napenda kuona atakaporudi kuja kuwasilisha maadhimisho ya hotuba yake, atufahamishe juhudi ambazo anazifanya kushirikiana na Wizara nyingine ambazo moja kwa moja zinahusiana na masuala ya maendeleo ya viwanda kama nishati, maji, miundombinu, elimu, kazi ili kuhakikisha kuwa mipango yake itaweza kutekelezwa na masuala yote muhimu yatakuwa yamezingatiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna viwanda ambavyo tayari vinaendeshwa, vingine vipya, vingine vya zamani, lakini kwa bahati mbaya bado kuna matatizo ya kimsingi ya miundombinu muhimu, wezeshi kwa viwanda hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua mipango iliyopo kwa viwanda vilivyopo kwanza kwa sasa hivi, ya kuhakikisha kuwa vinapata umeme wa kutosha, vinapata allocation ya gas kwa ajili ya kuzalisha umeme wa kuendesha shughuli zao, vinapata maji ya kutosha na zaidi ya yote miundombinu bora itakayowezesha mazao kwenda na kuondolewa kwenye viwanda hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna matatizo ya kimsingi ambayo lazima tuyatatue sasa kabla hata hatujafikiria kuanzisha viwanda vingine. Hii itakuwa ndiyo njia peke yake ya kuwavutia wawekezaji wa ndani na wa nje kuja kuwekeza katika viwanda nchi hii, baada ya kuona mifano mizuri ya viwanda ambavyo tayari viko nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile kutoa rai kwa Serikali kuwa hadi sasa tunavyozungumza, naamini kutokana na hilo kuwa kila Wizara inajiendesha yenyewe bila kuangalia mahusiano ya karibu yaliyo katika Wizara hizo, tunakuwa na migongano ya sera na sheria, hata taratibu za kiuendeshaji zinazosababisha kuwe na kukinzana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo, ukizungumzia viwanda vinataka kuwekeza, lakini unakuta labda viwanda vinapotaka kuwekezwa sehemu fulani, mweka umeme yeye ile sehemu siyo kipaumbele kwake. Kwa hiyo, moja kwa moja kunakuwa kuna kukinzana. Kiwanda kinaweza kuanzishwa, soko linaweza kuanzishwa, lakini linachelewa kuanza kazi kwa sababu halijapata miundombinu muhimu ya umeme, maji na hata barabara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kuona jinsi gani Serikali imejipanga, Wizara muhimu zikae pamoja kupanga mipango tangu mwanzo wanapotengeneza road map ya viwanda, hadi inapofika utekelezaji kuwa kila kitu kiko in place ili viwanda vikianza vianze kufanya kazi bila kusuasua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuzungumzia suala zima la mambo ya vipimo na viwango. Tuna tatizo kubwa sana hata kwa viwanda vilivyopo katika uzalishaji uliopo wa viwango na vipimo sahihi vinavyoweza kuhakikisha kuwa bidhaa zetu zinapata ushindani unaostahiki. Tuna taasisi ziko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara ambazo kazi yake ni kuhakiki viwango na vipimo. Kwa bahati mbaya, havina uwezo wa kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sasa wakati tunajipanga kwenda kwenye uchumi wa viwanda, kuhakikisha taasisi muhimu kama hizi zinawezeshwa kwa maana ya taaluma, maabara, nyenzo zote zitakazowawezesha wao kuhakikisha kuwa viwango na vipimo viko sahihi ili bidhaa tunazouziwa ziwe zile ambazo zina ubora unaotakiwa au ubora ambao unaweza kushindana na bidhaa zinazotoka nje ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi kuona katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri, ameelezea kuwa kutakuwa na mgawanyo wa viwanda nchi nzima kufuatana na rasilimali zilizopo. Hili ni wazo jema kwa sababu hii itaondoa ule mtindo wa zamani kuwa kila kitu kinalundikwa katika Miji Mikuu na sisi wa pembenzoni tunakuwa kila siku ni wa kuzalisha malighafi na tunashindwa mahali pa kuzipeleka. (Makofi)
Napenda kuona sasa kuona ramani kamili ya viwanda hivi hasa maeneo ya pembezoni au vijijini ambako kilimo kinaendeshwa kwa wingi na jinsi gani viwanda vya aina mbalimbali, vikianzia vile vidogo kabisa, vya kati na hata vikubwa vitakavyokuwa vimeainishwa. Hii itahakikisha Watanzania wengi wanashiriki katika uchumi wa viwanda, wanapata kipato, ajira na vile vile na maisha yao yanainuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia kwa ufupi suala zima la kukuza soko la ndani. Tumekuwa ni watu wa kuagiza bidhaa ambazo hatuzalishi na kuzalisha bidhaa ambazo hatuzitumii. Napenda kuona hili linabadilika kwa sababu bidhaa nyingi tunazoagiza kutoka nje kwa fedha nyingi, kwanza hazina ubora ambao tungeutegemea, lakini vilevile zinaua soko la ndani na vilevile zinaua ajira zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalima mazao mengi sana nchi hii ya kutosha kulisha nchi yetu hata na majirani. Huo ni mwanzo mzuri kwetu kwa ajili ya viwanda. Sasa napenda kupata kutoka kwa Waziri mkakati alionao wa kukuza soko la ndani kwa maana ya kuanza kuwekeza katika viwanda ambavyo vinazingatia mahitaji ya ndani kabla ya kuzungumzia masuala ya ku-export. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kujua, Mheshimiwa Waziri ana mkakati gani wa kupunguza uagizwaji wa bidhaa kutoka nje ambazo kwa kweli hatuzihitaji, ukizingatia kwa sisi wenyewe tunao uwezo wa kuzalisha? Tungependa kuona anaanza kupunguza kidogo kidogo uagizwaji wa bidhaa za nje ambazo haziitajiki na kuongeza uzalishaji wa bidhaa za ndani. Hii itawezekana akishirikiana na Wizara zinazozalisha mazao ya kilimo, ufugaji na uvuvi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la uwezeshaji wa wajasiriamali. Tanzania hii kuna mwenzangu mmoja ni Mheshimiwa Mbunge amesema kuwa kila mahali kuna frame. Mimi lile sioni kama ni jambo baya, ule ni ujasiriamali. Kinachotakiwa sasa ni je, wanawezeshwa vipi hawa wajasiriamali kwa maana ya mafunzo, nyenzo na mitaji? Napenda sana kuona Wizara hii ya Viwanda inaboresha kitengo kinachoshughulika na wajasiriamali ili tuone jinsi gani wamejipanga kuwasaidia wajasiriamali wale wadogo kabisa, wa kati, hata wakubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ndiyo ina taasisi muhimu zinazosaidia kujenga uwezo wa wajasiriamali kwa maana ya tafiti, masoko na uzalishaji, Iakini hatujaona moja kwa moja jinsi ambavyo wajasiriamali wetu wengi wananufaishwa na hizi taasisi. Tungependa sasa kuona ule mpango ambao upo chini ya Wizara wa industrial upgrading unatumika na kufanya kazi vizuri zaidi; kutoa mafunzo kuwatafutia masoko, kuwapa mbinu za uzalishaji na viwango na kuwaanzishia viwanda na kuwasimamia hadi wakomae. Kwa kuanzia na ngozi, nguo, usindikaji chakula, mafuta ya kula na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba sekta ndogo ndogo mbalimbali zichukuliwe na kupewa mafunzo, nyenzo bora za jinsi ya kuzalisha, jinsi ya kuanzisha viwanda na ku-maintain ubora na ku-maintain kufungasha vizuri katika njia ambayo inavutia walaji, lakini vilevile kuuza katika soko la ndani na hata la nje kwa maana ya masoko ya Afrika Mashariki na Afrika kwa ujumla. Wizara hii ni muhimu na ya kimkakati sana katika masuala ya kukuza uchumi na kuondoa umaskini. Hata hivyo, tungependa kuona moja kwa moja mchango wake unavyoonekana kufuatana na mipango yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sikatai sasa hivi ndiyo tumeanza hizi mbio za kwenda kwenye uchumi wa viwanda na kwa mwaka huu tunaweza tusione viwanda moja kwa moja; lakini japo ile mipango ioneshe mwelekeo wa Serikali katika kuhakikisha kweli hivi viwanda tutavifikia. Tuondoe hizi kejeli ambazo tunazisikia hapa kuwa ooh, mnasemasema tu! Oooh, mnapanga panga tu, uwezo wa nchi hii kuwa na uchumi wa viwanda upo, lakini tujipange vizuri, tuwe realistic, tusijiwekee malengo ambayo tutashindwa kuyafikia, lakini tuanze pole pole kwa mwelekeo mzuri utakaotuhakikishia kuwa mwisho wa siku tunaweza kufanya hili jambo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sijawatendea haki akina mama na vijana kama sitazungumzia suala zima la mchango na ushiriki wa wanawake na vijana katika suala zima la viwanda. Wanawake na vijana ni wazalishaji wakubwa na wana jeshi kubwa nyuma yao. Hili ni lazima lichukuliwe maanani wakati wa mipango yote ya viwanda. Viwanda vidogo vidogo, biashara ndogo ndogo nyingi zinaendeshwa na makundi haya makubwa mawili, sasa tunapozungumzia viwanda vilevile lazima na wao tuwabebe, tuhakikishe kuwa akina mama na wao wanawezeshwa katika masuala ya usindikaji, vifungashio na mafunzo muhimu ya jinsi gani ya kuboresha huduma anazozitoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, akina mama wamekuwa ni wafumaji wa nguo; masweta, wengine tunatoka kwenye Mikoa yenye baridi sana, akina mama wangeweza kuwekewa viwanda vya kufuma masweta na soksi na nini, badala ya kuagiza sweta na uniform za watoto kutoka China, eeh wakawekewa mifumo hiyo wakafuma masweta wakawa wanauza katika nchi yetu hata nje ya nchi, hiyo ingekuwa ni ajira tosha na ingeinua kipato na maisha ya akina mama wengi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wengi sana wanamaliza vyuo vikuu na shule mbalimbali katika ngazi mbalimbali, wangetengewa hawa utaratibu kwa kupitia BRELA ambayo ndiyo inaandikisha makampuni wakawekewa namna ya kuandikisha makampuni yao, wakawekewa namna ya kufundishwa jinsi ya kuzalisha na kuanzisha biashara mbalimbali au uzalishaji mbalimbali wakapata ujuzi huo, wakaunganishwa na mitaji kutoka benki, wakaanzisha biashara zao wenyewe bila kungojea kuhangaika kuajiriwa na mtu yeyote. Hiyo ingekuwa ni njia moja ni rahisi sana ya kukuza viwanda nchini kwetu kuanzia vile vidogo vidogo na kadri wanavyoendelea kuwa wakubwa wakakua mpaka wakaja kuwa na viwanda vikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Roma haikujengwa siku moja ndugu zangu, lakini tukianza vizuri tunaweza tukafikia malengo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizugumzie sasa kidogo Mgodi wa Kiwira. Mgodi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira ni mgodi ambao uko Ileje, Jimbo ambalo mimi ndio Mbunge wake. Mgodi huu haujawahi kunufaisha Ileje. Kwanza ulikuwa hautambuliki kama uko Ileje wakati kijiografia na kwa njia nyingine zote uko Ileje. Haya, hayo tuyaache, hiyo ni historia!
Sasa hivi tunaambiwa mgodi ule upo tayari kufufuliwa na ule mgodi ulianzishwa ili makaa ya mawe yale yatumike kwa ajili ya umeme. Ileje ni Wilaya mojawapo ambayo haina umeme, viwanda, barabara, haina kitu chochote ambacho unaweza ukakizungumza kuwa ni cha maendeleo zaidi ya kilimo, lakini rasilimali zimejaa pale, zimetuzunguka. Napenda sasa Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa, uwaeleze wana Ileje mgodi ule utafufuliwa lini?
MHE. JANET Z. MBENE: Naunga mkono hoja.