Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Jimbo la Mikumi lina Kata 15 na katika Kata hizo zinapata taabu sana ya kutokuwa na Mahakama na zile zenye Mahakama zinachangamoto zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama nyingi hazijapimwa au kurasimishwa na kusababisha wananchi kuingilia na kufanya shughuli mbalimbali za kibinadamu kwenye maeneo ya Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uchakavu mkubwa wa majengo ya Mahakama za Jimbo la Mikumi. Mahakama nyingi zimechakaa sana na hazina umeme wala vyoo kitu kinacholeta usumbufu kwa watumiaji wa Mahakama zetu na watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni ofisi kutokuwa na nembo ya Taifa na Bendera. Mahakama zetu za Jimbo la Mikumi, mfano Kata ya Mikumi na Kata ya Malolo hazina nembo ya Taifa na kupunguza heshima ya Mahakama zetu. Mahakama zetu hazina samani za ofisi, mfano computer, mashine za kurudufu hukumu, makabati ya kuhifadhia nyaraka mbalimbali muhimu. Hii inasababisha malalamiko makubwa kutoka kwa wananchi maana wanakosa haki yao ya kupata hukumu ya kesi na kuambiwa waje siku nyingine hata kama hukumu imeshatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, linginei ni mahabusu. Mahakama nyingi ziko mbali na vituo vya Polisi au Magereza na kusababisha Mahakama kupata shida ya kuwahifadhi watuhumiwa, mfano Mahakama ya Kata ya Malolo ipo zaidi ya kilomita 200 kutoka Kituo cha Polisi na kusababisha usumbufu mkubwa wa kusafirisha wafungwa. Inabidi mtuhumiwa atoe shilingi 60,000/= kwa nauli wakati ni wajibu wa Serikali na ikishindwa inabidi hakimu alipe hela yake ya mfukoni inakuwa ngumu sana. Tunaomba Polisi waje kuwachukua wafungwa ili kupunguza mzigo kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nichangie kuhusu upungufu wa watumishi wa Mahakama. Kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mishahara ya Mahakimu na watumishi wa Mahakama ni midogo. Vile vile posho za nyumba; Mahakimu ni watu muhimu sana kutokana na aina ya kazi zai wanazofanya wanastahili sana kupata posho za nyumba kama wanayopata waendesha mashtaka, maana mahakimu wengi wanaishi mbali sana na maeneo ya Mahakama ambapo hawajapewa na Serikali nyumba za kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokakana na kazi yao ya kutoa haki sawa na kuhukumu, Mahakimu wanastahili sana wapewe ulinzi wa kutosha maana kutokana na kazi yao watuhumiwa wengi wanaokutwa na hatia wanawatisha sana Mahakimu wetu na kutishia usalama wao hasa kwa kuzingatia Mahakimu wengi wanaishi mitaani bila ulinzi wa uhakika na usalama wao na kuhatarisha maisha yao. Ahsante sana.