Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, baba yangu na kwa kweli nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa wanazozifanya. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuridhia kuanzisha zile taasisi mbili zinazojitegemea, moja Kurugenzi ya Mashtaka na Ofisi ya Solicitor General. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa sababu sasa tunaamini mambo ya haki yatafanyika vizuri zaidi kuliko ilivyokuwa katika mfumo wa zamani. Nimeona bajeti imeongezeka kwa sababu tumeanzisha taasisi tofauti na bajeti yake sasa hivi imekuwa kubwa na mnakumbuka kipindi cha nyuma aliyekuwa Mwanasheria Mkuu alikuwa analalamika sana kuhusu bajeti, lakini nina uhakika sasa huyu Mwanasheria Mkuu wa sasa amepata bahati kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni dakika tano tu, naomba niongelee kitu kimoja tu kidogo cha kuhusiana na matumizi ya Mfuko wa Mahakama. Nimwombe sana Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, Waziri wa Katiba na Sheria atusaidie sisi Wananamtumbo, tuna idara ya mahakama pale ngazi ya wilaya inafanya kazi vizuri sana, lakini mazingira waliyonayo sio mazuri. Wamekaa katika majengo ambayo ni ya kuazima na kwa bahati mbaya sasa hivi wamezungukwa na Kituo cha Afya cha Namtumbo. Nimwombe aingize katika bajeti ya mwaka huu Wilaya ya Namtumbo kujengewa Mahakama ya Wilaya ili pale walipo sasa waweze kupisha shughuli za Kituo cha Afya kipya kabisa cha Namtumbo kiweze kufanya kazi vizuri zaidi kuliko kuchanganya haya mambo mawili katika eneo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa fursa, nilitaka niliongelee hilo jambo moja, dakika tano sio muda mrefu, ni kwa sababu tu unapoanza kuongea moja kwa moja unaanza kwenye hoja, lakini ukianza kuogelea maeneo mengine unajikuta muda umeisha, hoja uliyotaka kuongea unaikosa na ni kitu ambacho wenzetu inabidi wajifunze ili tuweze kwenda vizuri katika kuwatumikia wananchi wetu majimboni kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kauli hiyo, naomba nisisitize Mahakama ya Wilaya ya Namtumbo ipate fursa ya kujengwa... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Engineer Ngonyani.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)