Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa dakika hizo tano. Kwanza kabisa, naanza kwa kuunga mkono hoja hii ya Wizara ya Muungano. Nitumie fursa hii kumuunga mkono sana na kuwapongeza Waziri wa Muungano, Mheshimiwa January Makamba na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Mussa, kwa kazi nzuri wanayofanya lazima niwapongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia natumia fursa kwa kipekee kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo ameondoa changamoto iliyokuwa inatukabili muda mrefu ya deni la ZECO. Hilo lazima tushukuru sana na kupongeza na hii inathibitisha kwamba Mheshimiwa Rais ni muumini wa kweli wa Muungano wetu. Hilo lazima tulioneshe na Watanzania lazima waelewe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo mazuri yanayofanywa na Mheshimiwa Janauary na timu nzima, napenda kusema kwamba sote tunaupenda Muungano, mimi ndiyo muumini wa kwanza wa Muungano. Katika kuupenda Muungano tunaomba hayo ambayo mmeyakusudia na kuyaendeleza muyafanyie kazi inavyostahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nisisitize maeneo matatu kwa haraka haraka. Fursa za kiuchumi Zanzibar ni jambo linalopigiwa makelele siku zote. Miaka ya 1985 mpaka tunakwenda 2000 wenzetu wa Tanzania Bara walikuwa wanakuja kufanya biashara Zanzibar, wanabeba mali kule na wanatunufaisha Wazanzibari. Sijui kimetokea nini hapa katikati, ndugu zetu wa Tanzania Bara mnahamia Rwanda, Burundi, Kenya na Uganda mnatuacha jirani zenu, hebu angalieni hapo tunakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni kwenye masuala ambayo tunaungana, nakwenda kwenye Balaza la Mitihani la Taifa, hapo bado hapajakaa vizuri. Kuna communication, coordination na cooperation ndogo, tuweke sawa hapo. Balaza la Mitihani lile na chombo maalum kinachotambulika kisheria ili ku-coordinate, cooperate na ku-communicate baina ya Wizara zetu mbili, tutakwenda vizuri, tunaupenda Muungano. Pia NACTE kwenye elimu ya juu, tuangalie kinachotambulika Tanzania Bara na Zanzibar kitambulike. Tunaomba tufanye hayo kwani tutakwenda vizuri na Muungano wetu Mheshimiwa January na timu yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine zuri kabisa, naomba niliseme kwa Watanzania wote kuhusu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejenga misingi imara ambayo inaweza kulidumisha Taifa letu miaka mia ijayo. Kwa hiyo, yale marekebisho madogo madogo ambayo tunaomba yanaendelea kufanyika siku zote isiwe ni neno la kuleta mjadala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaendelea na marekebisho madogo madogo, Katiba yetu iko vizuri na tutakwenda nayo vizuri hata miaka mia ijayo kwa sababu kila kilicho ndani ya Katiba ile kinatafsirika vizuri. Hiyo implementation ni jambo lingine wala siingilii lakini Katiba yenyewe kama Katiba inatufaa na ndiyo maana ikatufikisha miaka 55 hii na tukiwa tunasifiwa na mataifa yote ulimwenguni kwa Muungano ambao tunao, kwa nini tusiringe? Lazima turinge na Taifa letu kwa sababu Muungano wetu ni mzuri, uko very unique, inatakiwa na mataifa yote waige kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tuweze kuendeleza haya, hizo changamoto tuzimalize kwa muda unastahiki ili tuweze kujivunia zaidi Muungano wetu na kuupenda zaidi Muungano wetu. Mimi naipenda Zanzibar, naipenda Tanzania Bara lakini nakupenda Muungano zaidi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)