Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa hii nafasi ili nami niweze kuchangia bajeti ya Wizara hizi muhimu, bajeti ya TAMISEMI na bajeti ya Utumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kuwapongeza Mawaziri wote wawili pamoja na team zote mbili, kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana. Wanafanya kazi nzuri na kwa ushahidi kabisa, kwenye Jimbo langu TAMISEMI wamefanya kazi nzuri sana katika eneo la TARURA, eneo la Afya na eneo la Elimu. Kwa kweli nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile kumpongeza Mheshimiwa Rais naye kwa kazi nzuri iliyotukuka. Amefanya mageuzi makubwa ya nchi hii, amefanya makubwa mno. Ushahidi ni mkubwa pamoja na miradi ya kimkakati kwenye Jimbo langu, ni mambo mengi ambayo ameyafanya na haijawahi kutokea toka enzi za ukoloni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa suala la TARURA. TARURA chombo chenyewe ni kizuri sana, lakini kuna tatizo kubwa kwamba TARURA haina pesa kabisa. Kwenye Jimbo langu nina mtandao wa barabara usiopungua 1,000. Bajeti tumepewa shilingi bilioni 1.5 ambazo ni kilometa 35 kama sikosei. Kuna madaraja chungu nzima, hayapungui 200. Utamaliza miaka mingapi kukamilisha hiyo kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri tungeenda kiuchumi zaidi, tuangalie ni namna gani haya maeneo ambayo ni muhimu yapewe kipaumbele. Unapozungumzia Mbeya Vijijini, unazungumzia kilimo cha nchi hii. Mazao yanatoka kwenye mashamba, lakini hatuna barabara kabisa. Mazao hayawezi kutoka shambani kuja sokoni na vile vile hatuwezi kupeleka pembejeo kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza hivi leo, barabara ya kuanzia Songwe Viwandani kwenda Jojo haipitiki kwa vile daraja lilikuwa limeshabomoka. Daraja hilo moja linahitaji zaidi ya shilingi milioni 250. Leo ni mwaka wa tatu wananchi wanasumbuka daraja halijajengwa. Pamoja na maombi maalum, inavyoelekea, tatizo katika bajeti, tuangalie ni namna gani TARURA waongezewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara nyingine ya kuanzia Kawetere kwenda Ikukwa, barabara ya Irambo kuja Ihango mpaka Nsonyanga, barabara za Mbonile mpaka Nyarwerwa. Tuna barabara nyingi mno ambazo ni muhimu na za kiuchumi lakini hazimo kabisa hata kwenye mpango wa bajeti. Kama nilivyosema, kwa bajeti ya shilingi bilioni 1.5 utafanya nini kwenye mtandao kilometa 1,000?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ijaribu kuangalia ni namna gani itatunusuru kwenye barabara? Bila barabara hakuna kilimo, bila barabara hakuna elimu, bila barabara hakuna hata shughuli za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kuchangia kidogo katika Wizara hizi mbili ni suala la afya. Napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Rais na Waziri Mheshimiwa Jafo, wamefanya kazi kubwa mno. Halmashauri ya Mbeya tulikuwa hatuna Hospitali ya Wilaya, tulikuwa hatuna vituo vya afya vya kutosha, lakini wametupatia vituo vya afya vitatu; Kituo cha Afya cha Ikukwa, Kituo cha Afya cha Ilembo na Kituo cha Afya cha Santiria. Vituo hivi vimebadilisha kabisa muundo na huduma za afya katika Halmashauri yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunahitaji mahitaji makubwa zaidi. Wananchi wamejenga zahanati, maboma hayapungui 70 ambayo yanahitaji msukumo na bajeti ya Serikali. Pia kuna vituo vya afya vilivyojengwa kwa nguvu za wananchi; kuna Kituo cha Afya cha Ifupa, wananchi wameshajenga, wametumia karibu shilingi milioni 200. Kwa hiyo, tunaomba tu kama shilingi milioni 200 tuweze kumalizia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Kituo cha Afya cha Isuto, nacho kimefikia hatua nzuri, tuna Kituo cha Afya cha Ihoho, Kituo cha Afya cha Maendeleo na Kata ya Tembela. Hivi viko katika hatua nzuri. Kama ikiwezekana, tunaiomba tena TAMISEMI waangalie ni namna gani kwa upendeleo kabisa hivi vituo vipate bajeti ya ku tosha ili tuweze kuvikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la elimu, napo napenda kupongeza tu kwa vile tumefanya vizuri, Serikali kwa kweli imefanya jitihada na wananchi wenyewe nao wamefanya jitihada kiasi cha Halmashauri yangu ya Mbeya kiufaulu tumefanya vizuri sana. Shule zimefanya vizuri na wananchi wameweza kufungua shule tatu ikiwemo moja ya high school na shule moja ya wasichana ambayo ni ya bweni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ni mengi. Sasa ukiangalia tuna wanafunzi karibu 70,000, walimu tulionao ni 1,035, angalia gap hiyo. Pamoja na jitihada za wazazi, bado tunahitaji walimu ili waweze kuinua uchumi wa vijana wetu. Kuna shule ambayo ina mwalimu mmoja, inaitwa Ilindi. Hii shule ina wanafunzi karibu 300, mwalimu mmoja. Kimaajabu ile shule imefaulisha watoto na ikapata nafasi nzuri. Kwa mshangao wa kila mtu akauliza, itakuwaje shule ya mwalimu mmoja, madarasa saba ikafaulisha kuliko shule zenye walimu wengi? Tukagundua kumbe hata wazazi nao wanashiriki kwenda darasani kufundisha watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hali kama hii nafikiri siyo nzuri sana. Ili tuweze kushindana na wenzetu, inabidi elimu yetu nayo iwe nzuri, tufanye vizuri katika elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda nichangie kidogo, ni suala la uendelezaji wa miji na mipango miji. Kwa sisi ambao tunazunguka majiji, majiji sasa hivi yamejaa na watu wengi ujenzi unakuja kwenye vijiji vyetu ambavyo havijapimwa. Kwa hiyo, tunaongeza squatters zile ambazo tulizikuta. Sasa hivi squatters zinahamia kwenye Halmashauri ambazo zinaizunguka Jiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ijaribu kuangalia iwe na mkakati wa kuhakikisha kuwa vijiji vyote ambavyo vinazunguka majiji, vipimwe, viwe katika mpangilio mzuri na yale maeneo ambayo yapo mijini kama maeneo ya Tanganyika Parkers, haya yagawiwe kwa wananchi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Njeza.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)