Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie kwenye hotuba ya Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa pamoja na Waziri wa Nchi anayeshughulikia mambo ya Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya. Nimemshangaa sana ndugu ya Mheshimiwa Ngombale pale alipotamka kwamba anaitaka Serikali iwaombe radhi wakulima wa korosho. Mimi nasema Serikali haiwezi kuomba radhi ila inapaswa kupongezwa kwa hatua iliyoichukua kwa kuwanusuru wakulima wa korosho. Mheshimiwa Ngombale yeye analima ufuta, nimeshangaa sana anaposema habari ya korosho na Wilaya Masasi ambayo natoka mimi ndiyo Wilaya ya pili kwa uzalishaji nchini baada ya Tandahimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa wa Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi alivyolishughulikia suala la korosho na kuwasamehe wale ambao walinunua kinyume na utaratibu almaarufu kama ‘kangomba’. Tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tunashuhudia jinsi wananchi wanavyojitokeza kwa wingi, nimeona mkutano wa pale Mufindi, Iringa, Mtwara, Namtumbo, kwa kweli Watanzania wana imani kubwa na Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. Nadhani vyama vya upinzani mwakani itabidi wajitafakari kuona kama kuna sababu ya kumweka mgombe Urais kwa sababu kwa hali ile navyoiona sidhani kama kutakuwa na mgombea yeyote atakayeweza kushindana na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli.

WABUNGE FULANI: Aaaaaa.

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana jirani yangu Waziri Jafo na wasaidizi wake ndugu yangu Mheshimwa Kandege na Mheshimiwa Waitara kwa kazi kubwa mnayoifanya TAMISEMI, hongereni sana. Mheshimiwa Jafo namfahamu siku nyingi sana na wengi tunamfahamu pale alipokuwa Plan International aliwahi kuwa mfanyakazi bora lakini Bunge lililopita tulimchagua Mheshimiwa Jafo kutuwakilisha kwenye Bunge la SADC. Mheshimiwa Anne Makinda aliwahi kusimama hapa akasema anatuwakilisha vyema baada ya kupewa Kamati kule kwenye SADC, tunakupongeza sana. Kwa hiyo, haya unayofanya TAMISEMI ni mtiririko wa utendaji kazi wako uliotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Waziri, Kapteni Mstaafu George Huruma Mkuchika na Mheshimiwa Dkt. Mwanjelwa, msaidizi wake katika Wizara hii. Tunapongeza tuna maana, Mheshimiwa George Huruma Mkuchika, yeye ni kati ya wachache ambao wapo madarakani waliowahi kuteuliwa kwa nafasi mbalimbali kuanzia DC, RC hadi Waziri katika vipindi vyote vya Marais watano walioongoza nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Baba wa Taifa alimteua kuwa DC na Mheshimiwa Rais Mwinyi akamteua kuwa DC baadaye Mzee Mkapa akamteua kuwa RC. Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete na Mhehimiwa Dkt. Magufuli wote wammeteua Mzee huu kuwa Waziri katika awamu zao. Kwa hiyo, kwa kweli tunampongeza kwa utendaji wake mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la TAMISEMI, hii ni Wizara ngumu sana. Bahati nzuri nimekulia TAMISEMI, nimekuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa, Diwani kwa miaka 10, Meya na sasa Mbunge, naifahamu TAMISEMI ni ngumu sana. Kwa mfumo Mheshimiwa Jafo, Manaibu, Katibu Mkuu na watu wa TAMISEMI kwa ujumla sasa haitembei bali inakimbia kwa utendaji wenu wa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye afya elimu wengi wamezungumza sitaki kurudia sana lakini nikuombe Mheshimiwa Jafo pamoja na juhudi ambazo zimeendelea kufanywa hasa katika Jimbo la Lulindi kama nilivyokuwa nikieleza mara kwa mara kwamba sasa hivi kituo kinachofanya kazi ni kimoja tu cha Nagani. Namshukuru Mheshimiwa Rais nilipomuomba suala la gari amenikubalia na wananchi wa Lulindi wanashukuru sana kwa jinsi ambavyo amesikiliza kilio kile. Bado nikombe Mheshimiwa Jafo na Naibu Katibu Mkuu Afya na timu nzima ya Naibu Mawaziri, Mungu akiwajalia mkapata fedha za kuongeza vituo vya afya tunahitaji kituo muhimu sana cha afya cha Mnavila kilichopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naomba kituo hiki kwa haraka sana? Tunalo tatizo kubwa sana la wananchi wetu kupoteza maisha na viungo kutokana na wimbi kubwa la kuzaana kwa mamba katika Mto huu wa Ruvuma. Tatizo lililopo ni kwamba hatuna kituo cha afya karibu, hivyo, kukitokea majanga ya namna hiyo wananchi wetu wanapata tatizo la kupoteza maisha ama kupata ulemavu kwa sababu hakuna huduma ya haraka katika eneo hilo. Kutoka pale Mnavila kwenda kwenye kituo cha afya ni zaidi ya kilomita 50. Kwa hiyo, nikuombe sana kwa huruma yako kwa kweli kituo hiki ni muhimu sana kipatikane ili tuweze kuwanusuru wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili hili la ujenzi wa hospitali, nishukuru kwa kunipatia Hospitali ya Wilaya ambayo inajengwa hivi sasa pamoja na kituo pale Chingutwa. Nashauri kitengo kile kinachohusika na gharama za majengo haya wawe waangalifu katika kutoa fedha aidha shilingi milioni 400 au 500 kwa sababu kuna baadhi ya maeneo ambapo upatikanaji wa vifaa ni mgumu inapelekwa shilingi milioni 400 lakini eneo ambalo halina tatizo inapelekwa shilingi milioni 500. Kwa hiyo, nadhani hili ni suala tu la marekebisho la kuangalia eneo ambalo lina changamoto nyingi basi ndiyo lipelekewe fedha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nishukuru kwa jinsi unavyoiongoza TARURA lakini bado Mheshimiwa Waziri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana kwa mchango wako.

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)