Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niseme machache katika Wizara hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na TAMISEMI na suala nzima la posho za Wenyeviti wa Vijiji na Vitongozi. Hawa ni viongozi ambao wanachaguliwa kama ambavyo Madiwani, Wabunge na Rais wanavyochaguliwa, lakini hatujaweka utaratibu wa kuangalia haki zao na hasa kuhakikisha kwamba wanapata posho. Napendekeza kwamba kama Serikali Kuu haina uwezo wa kuwawezesha viongozi hawa kupata posho, basi itoe maelekezo maalum katika makusanyo ya ndani ya vijiji husika, viongozi hawa walipwe kutokana makusanyo hayo. Hiyo itawasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala la vitambulisho vya wajasiliamali, zoezi ili limeanza ghafla ghafla na limeleta taharuki kubwa huko kwa wananchi na hasa pale Serikali inaposhindwa kubainisha ni yupi mjasiliamali ambaye anatakiwa apewe kitambulisho? Kumekuwa na sintofahamu, mama mwenye mafungu matatu ya mboga anatakiwa alipe shilingi 20,000/=, mama huyo huyo akiwa na mikungu mitano ya ndizi, anatakiwa alipe shilingi 20,000/= na sehemu nyingine kama kule kwangu mtu mmoja analazimishwa kulipia hata mara tatu kwa sababu ana biashara tatu tofauti. Hiyo ni sintofahamu kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, vitambulisho hivi vinaenda kubana kabisa mapato ya vijiji na mapato ya Halmashauri. Halmashauri hizi zitastawi vipi kama mapato yake kwa namna tofauti tofauti yanaendelea kuchukuliwa na Serikali Kuu? Naiomba Serikali hilo waliangalie, kwa sababu wananchi sasa wananituma, Mheshimiwa Mbunge, hebu tuulizie, hivi ile kodi ya kichwa imerudi? Maanda sasa kila tukizunguka ni vitambulisho, vitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haipo familia ambayo hahijihusishi na ujasiliamali sasa. Kila familia lazima ifanye ujasiliamali, vinginevyo maisha ni magumu. Sasa kama unafanya ujasiliamali ni shilingi 20,000/=. Maisha kule ni magumu sana, naomba hilo liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusiana na ujenzi wa zahanati kama sera inavyozungumza. Kwa bahati mbaya kabisa, mimi katika Jimbo langu kuna Kata moja aina zahanati hata moja za Serikali. Ile kata inaitwa Kata ya Namayuni. Ile kata ina vijiji sita, kuna kijiji kimoja kinaitwa Kijiji cha Naama, chenyewe wamejitahidi, wamejenga angalau kufikia boma. Naomba Wizara iwasaidie wale wananchi wapate ile zahanati iishe ili basi kata ile nzima iweze kupata huduma kwa sababu wananchi wanatembea kilometa zaidi ya 20 mpaka 50 kufuata huduma za matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, bado kuna tatizo la miundombinu iliyokamilika kuendelea kutotumika. Katika Kata ya Mingumbi katika Kijiji cha Lyomanga, Mfuko wa TASAF ulitoa fedha na kujenga zahanati toka mwaka 2009. Mpaka hivi tunavyozungumza, zahanati ile haijatumika na sasa inaelekea kubomoka. Naiomba Serikali ifuatilie hiyo zahanati na ione namna gani pesa za Serikali zinapotea bila kuwa na sababu ili basi ikiwezekana wafanye marekibisho na wananchi wapate huduma ya matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la korosho. Nachukuwa fursa hii kuipongeza Serikali na hasa ile kauli iliyotolewa na Mheshimiwa Rais kuhusiana na kwamba itawalipa sasa wakulima wa korosho pamoja na wale kangomba. Nikiri kabisa, sasa angalau tunaishi kwa matumaini, kwa sababu hali mwanzoni ilikuwa ni ngumu sana. Ingawa malipo yenyewe bado hayajafanyika, lakini tunayo imani kwamba siku moja tutalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili niseme, Serikali iache tabia ya kuingilia michakato iliyopangwa kwa mujibu wa sheria. Suala la korosho na utata uliotokeza ni kwa sababu tu Bodi ya Mazao Mchanganyiko haina uzoefu wa kusimamia zao la korosho. Katika namna ambayo hatufahamu, ni kwa namna gani Bodi ya Korosho ambayo inatambulika kwa mujibu wa sheria ikawekwa pembeni na badala yake ikachukuliwa Bodi ya Mazao Mchanganyiko ambapo mzigo umewalemea mpaka sasa wanashindwa kufanya malipo kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inajinasibu kwamba imetoa pesa, lakini bodi ile inashindwa kwa sababu haina uzoefu. Kwa hiyo, naomba hili liangaliwe sana. Kwa sababu maamuzi hayo yamepelekea hasara, athari za kisaikolojia, na kudumaza maendeleo, naitaka Serikali iwaombe radhi wakulima wa korosho kwa kitu kilichotokea. Kwa sababu kuna watu wamepoteza maisha, Serikali iwaombe radhi wakulima wa korosho kwa sababu lile lililofanyika, limefanywa kwa makusudi. Kwa hiyo, naomba hilo lifuatiliwe mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo napenda niseme ni suala zima la TARURA. TARURA wanafanya kazi vizuri lakini bajeti yao haitoshi. Wanajitahidi, lakini bajeti yao haitoshi. Naitaka Serikali iongeze bajeti TARURA. Nami katika Jimbo langu, naomba TARURA ishughilikie barabara ya kutoka Mbombwe – Anga - Nakindu mpaka Miangalaya; lakini pia ishungulikie barabara ya kutoka Mkarango - Mitole na kutoka Chumo mpaka Mkoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nikumbushe ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne. Hii nalizungumza kwa mara ya tatu nikiwa humu Bungeni. Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Kikwete akiwa katika Sherehe za Kumbukumbu za Vita ya Maji Maji pale Nandete, aliahidi kwamba atajenga barabara kutoka Nandete mpaka Nyamwagi, ile ahadi mpaka sasa haijafanyiwa chochote. Naitaka Serikali ifuatilie utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la ufuta. Jimbo la Kilwa Kaskazini na Kilwa ujumla, sisi ni wakulima wazuri wa ufuta. Mwaka 2018 kulitokea na tatizo kwamba ufuta ambao hauna bodi ulilazimika kusimamiwa na Ofisi ya Mkoa na siyo Halmashauri, matokeo yake yalipelekea mapato ya Halmashauri kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018 tulikwenda TAMISEMI, tulifuatilia sana. Tunaomba zao la ufuta lisimamiwe na Halmashauri na siyo Mkoa kwa sababu zao hili halina bodi na Halmashauri ina uwezo wa kufanya hivyo. Kwa kufanya hivyo, kung’ang’ania kusimamiwa na mkoa, mapato ya Halmashauri yanapungua. Tunaomba sana zao hili lisimamiwe na Halmashauri na siyo vinginevyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nizungumzie kuhusu upandishwaji wa madaraja. Tunaomba Serikali ijitahidi sasa kuona madaraja na mishahara ya watumishi inapandishwa. Watumishi hawa wanafanya kazi kwa kujitolea, wanafanya kazi kwa nguvu kubwa lakini wanakosa motisha kiasi kwamba ufanisi wa kazi unapungua. Kwa hiyo, Walimu, Watumishi wa Afya wote wale wapandishwe madaraja na mishahara iongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nizungumzie kuhusiana na fedha za Mfuko wa Wanawake Vijana na Watu Wenye Ulemavu. Hili limezungumzwa sana na Wajumbe wa Kamati yangu, lakini pia nami niongezee. Tumefanya ziara sehemu mbalimbali, Halmashauri ya Wilaya ya Kahama imefanya vizuri sana na imefanya vizuri katika eneo hilo kwa sababu imefanya maamuzi ya kuchukuwa hizi pesa badala ya kumpa mtu mmoja mmoja ikaandaa utaratibu ambao utaenda kuwasaidia kundi hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie ile model ya Halmashauri ya Kahama, ikiwezekana ifanyike sehemu nyingine. Kwa sababu sasa mianya imefungwa. Mwanya peke yake ambao kama hatutakuwa makini, Watendaji wa Halmashauri wanaweza kutumia kupiga sana pesa, ni katika pesa hizi za asilimia kumi. Kwa hiyo, tuwe makini sana, hizi pesa ikiwezekana tuzielekeze katika namna ambayo tunaweza kufuatilia na walengwa wakapata mahitaji yao stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukukumbuke pia katika eneo la walemavu bado walemavu wanashindwa kupata yale mahitaji yao kulingana na aina ya ulemavu waliokuwanao. Tuangalie uwezekano wa kuwasaidia walemavu wasioona wapate fimbo, walemavu viziwi wapate shimesikio, walemavu wa viongo wapate viungo bandia, wapate baiskeli na wale walemavu albino wapate mafuta kwa ajili ya kujinusuru na adhari za miale ya mwanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukijielekeza huko tutakuwa tumewasaidia sana, vinginevyo hii mikopo tunaweza tukaipeleka na isiwe na marejesho. Ni heri tupeleke kwa kuwasaidia Walemavu kwa ulemavu walionao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Vedasto.

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana. (Makofi)