Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia. La kwanza, nitumie fursa hii kuwapa pole sana wananchi wangu wa Kata Tulya ambao wamepatwa na matatizo ya shule ya msingi kuharibiwa na mvua pamoja na zahanati yao. Niwaambie wawe watulivu, nami nitapata fursa weekend kwenda kuungana nao katika shida hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya yeye pamoja na wasaidizi wake kwenye Wizara hizi ambazo leo hii tuna mjadala mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, kwa sababu leo ni weekend na nchi yetu itakuwa na jambo kubwa upande wa michezo, nawatakia kila la heri vijana wetu wa umri wa chini ya miaka 17 na wapeperushe vizuri bendera yetu ya Taifa. Nawatakia kila heri pia club ya Simba ambao na wenyewe watakuwa wanapeperusha bendera ya nchi yetu kwa upande wa vilabu bingwa barani Afrika watakapopambana na wenzetu wa kule Kongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimeyasema hayo, niende moja kwa moja kwenye maombi. Jambo la kwanza ambalo ningependa kulileta mezani kwa Mheshimiwa Waziri ni hili ambalo moja kwa moja lina muunganiko na dhahama iliyowapata ndugu zetu wa Kata ya Tulya, kwamba kwa kuwa zahanati ile imeharibiwa na kwa kuwa ndugu yetu Mheshimiwa Jafo amekuwa mstari wa mbele sana katika kusaidia upande wa Sekta ya Afya, naomba apatapo nafasi tena ya kutupatia vituo vya afya, basi Kata ya Tulya ambayo zahanati yake imeharibika katika Kijiji cha Doromoni, iweze kupewa kipaumbele. Sambamba na hiyo, aikumbuke pia Kata ya Mtoa ambayo ni Kata ya Mbugani ambako upatikanaji wa huduma za afya umekuwa wa shida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimeyasema hayo, naomba niende kuweka ushauri kwenye mambo mawili makubwa. Jambo la kwanza, nimefuatilia mijadala tangu Waziri alipotoa hoja hii. Ni vizuri sana niwashauri Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania, kuna mambo ambayo tunatakiwa tuwe tunayabeba kwa umakini mkubwa sana, hasa katika kipindi hiki ambacho Mheshimiwa Rais wetu ametangaza vita ya kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wakati wa kubigania uhuru walikuwa na stahili zao za kupambana na walikuwa na namna ambazo wanakumbana nazo. Sasa hivi ambapo pana vita ya kiuchumi, hao watu tunaopambana nao kwenye vita za kiuchumi ni watu wenye akili, ni watu wenye fedha, na ni watu watu wenye uwezo wa kijasusi. Kwa maana hiyo, kila jambo linapotokea kwenye nchi yetu ni vyema sana tukawa tunalitafakari kwa uzito mkubwa badala ya kwenda kwenye uzito mwepesi kama sisi tunavyofanya mambo yanapotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tumeshuhudia katika nchi yetu yakitokea matukio ya kiuhalifu mengi mengi hivi, ambayo kwa bahati nzuri sana Serikali iliyadhibiti yote; moja ya matukio mabaya ni kama yale ya Kibiti; matukio mengine kama yale ya utekwaji wa watoto kule Arusha; matukio mengine ni kama yale ya utekwaji watoto kule Njombe; na mengine ya kiuhalifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio ya aina hii yote yamedhibitiwa na Serikali kupitia vyombo vya dola hivi hivi. Ni jambo la ajabu sana linapotokea tukio mojawapo la kiuharifu, badala ya watu kuona kwamba nchi yetu imekuwa na matukio ya kiuhalifu ambayo yanashughulikiwa na Serikali, kwa sababu za kisiasa na kutengeneza taswira chafu kwa Serikali, watu wanakimbilia kwenda kuhisi kwamba huenda matukio yanafanywa na vyombo vya dola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilimsikiliza mchangiaji mmoja, Mheshimiwa Mbunge wa kutoka Dar es Salaam akisema matukio ya aina hii kwa nini yasichukuliwe kwamba yamefanywa na Serikali au kupitia vyombo vyake? Akatolea mfano tukio la kutekwa kwa Mo. Hata mwizi tu ambaye ajaenda shule; mwizi wa mifugo aliyeko kijijini, hawezi kuiba mfugo, akaenda kuchinjia ng’ombe wake wa wizi mlangoni kwa nyumba yake. Sijui nimeongea Kiswahili cha Kikenya! Yaani mwizi hawezi kwenda kuiba ng’ombe, akamchukua ngo’ombe wa wizi akaenda kuchinjia nyumbani kwake ama mlangoni kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukianza kuwaza kwamba vyombo vya dola vinaweza vikawa vimeshiriki kwenye utekaji, halafu yule mtu akaokotwe, halafu vyombo hivi vikampeleke pale; ni kitu ambacho ni kuwaza kwa haraka haraka na kwa kutafuta kuaminisha watu jambo ambalo silo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa watu wanaofikiria, unaweza ukaona na ni muunganiko mkubwa kwamba hawa ni watu wanaotengeneza chuki dhidi ya Serikali na mambo mengine yanaweza yakawa yanafanyika ya muundo huu.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo niliona pia ni vyema nikalishauri, hiki ni chombo cha uongozi. Bunge ni chombo cha uongozi, ni chombo cha uamuzi, ni chombo cha sera. Kwa kuwa ni chombo cha viongozi, tunapokuwa tunajadili hapa, ingefaa miaka kadhaa itakayokuja watu wakipitia Hansard zeweze kuwapa dira kwamba katika kipindi hiki Taifa lilikuwa linatekeleza mambo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sote tunajua kwamba tunatekeleza miradi mikubwa itakayoiwezesha nchi kwenda uchumi wa kati. Kwa maana hiyo, kwa kila tunachokusanya kama Taifa na kwa kila Mtanzania siyo viongozi tu; kila mtanzania anatoa mchango wake katika kutekeleza masuala haya; ni vyema sisi tulio viongozi tukaweka kipaumbele kuwaelezea Watanzania kwamba kila jambo linalotokea halitokei kwa bahati mbaya, bali linatokea kwa mpangilio kwamba tuna ajenda tunayoitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, siyo halali kwa viongozi ambao wanajua kinachofanyika kuwa wa kwanza kulalamika kwamba hatuzioni fedha za matumizi mengineyo. Tunatekeleza miradi ambayo itafanya siku zijazo tupate fedha za matumizi mengineyo nyingi kuliko za sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, tunajenga vituo vya afya ambavyo havikujengwa kwa muda mrefu; siyo kwamba havijawahi kujengwa, vilishajengwa, lakini sasa hivi pia kuna vituo vituo vinajengwa maeneo ambayo hajawahi kuwa na kituo. Mfano kama Kinampanda pale hatukuwahi kuwa na kituo lakini kimejengwa. Sasa tunapokuwa tunatekeleza miradi ya aina hiyo tunatumia fedha hizo hizo ambazo tunajibana Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, inapotokea kwamba tunajibana ili tutekeleze miradi ya maendeleo, wengine wasitumie kama fursa ya kutengeneza chuki dhidi ya kundi mojawapo kwamba halijatendewa haki. Mifano inayotolewa ya watumishi wa Umma; na wenyewe ni sehemu ya mpango mkakati huu tunaotekeleza wa kuweza kuhakikisha kwamba tutakapokuwa tumeshatengeneza miradi itakayotengeneza fedha nyingi, tutaweza kujipandishia mishahara tunavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuwapandishia watumishi wa umma…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwigulu.

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)