Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uzima na hatimaye kusimama mbele yako kuweza kuchangia bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru sana Rais wetu kwa kazi kubwa anayoifanya. Vilevile nawashukuru sana Makamu wa Rais, Waziri wetu Mkuu ambaye amekuwa ni kiongozi wetu na mshauri wetu kwa kazi kubwa anayofanya na katika kumshauri pia Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Mawaziri, nampongeza sana Mheshimiwa Mkuchika na siku zote wanasema penye wazee hapaharibiki neno; amedhihirisha yeye ni baba, amedhihirisha pamoja na yote hayo na kama wanavyosema Waswahili kwamba, mkubwa akivuliwa nguo basi anachutama. Yeye ni jalala, lakini tunaona, tunamkubali na tunaona yale yote anayoyafanya. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Mary Mwanjelwa, Naibu Waziri kwa ushauri mzuri na kazi nzuri anayomsaidia Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Jafo. Ameonesha umahiri mkubwa sana hasa katika kutatua changamoto nyingi zinazowakabili wanawake. Ameweza kumsaidia na kumshauri Rais na hatimaye sasa tunaona matunda mazuri yanayofanyika, nampongeza sana na namwombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumtia nguvu, kumpa ujasiri na afya aendelee kuwatumikia Watanzania. Waheshimiwa Manaibu Waziri pia na wao tuwapongeze sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kuchangia kuhusiana na asilimia mbili ambayo katika Bunge la Bajeti mwaka jana tuliipitisha. Asilimia hii mbili tumeona ni kwa jinsi gani ambavyo imekuwa na mafanikio katika kusaidia makundi maalum na hasa kundi la watu wenye ulemavu. Niombe tu kwamba, kuna baadhi ya Halmashauri ambazo bado hazijatimiza matakwa ya Sheria hii ya Fedha (Finance Act); naomba sana azisimamie ili basi ziweze kutoa hiyo asilimia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, nishauri kwamba, kumekuwepo na changamoto baadhi ya watu wenye ulemavu ambao wako maeneo tofautitofauti, naomba kwamba, busara itumike tuangalie ni kwa jinsi gani ikibidi basi kama ni mmoja mmoja basi tuwakopeshe kwa sababu, wapo ambao tumeona wamefanya vizuri sana. Kwa hiyo, kusiwe na kigezo kwamba, lazima wajiunge kwenye vikundi naomba sana ofisi iweze kuangalia hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayoifanya hasa katika kutoa elimu bure. Nami nimekuwa siku zote nikithibitisha kwamba, elimu hii bure imesaidia baadhi ya watoto wenye ulemavu kupelekwa shule ambao walifichwa majumbani, lakini kwa sababu elimu ni bure wametolewa na sasa hivi wako kule. Changamoto iliyopo ni miundombinu, bado ni tatizo. Naiomba sana Serikali kuona ni kwa jinsi gani watasaidia katika kutatua changamoto hii ya miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika shule zote za sekondari tumeona na nashukuru sana wananchi kwa ujumla wamejitoa sana, Wabunge wamejitoa sana katika kuiunga mkono Serikali. Naomba kuona kwamba, ni kwa jinsi gani sasa katika shule hizi za sekondari, zile shule ambazo zina mabweni basi watoto wenye ulemavu waweze kupelekwa kule ili wasipate shida wakasome.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo pia watoto wenye ulemavu ambao wanakwenda katika shule ambazo ni maalum na Serikali ilikuwa na utaratibu wa kuhakikisha kwamba, inatoa fedha wakati shule zinapofungwa, lakini hivi sasa watoto wale imekuwa ni shida kwa sababu wengine wanalazimika kukaa muda wote shule mpaka inapofika Disemba. Namshauri Mheshimiwa Jafo, ameonesha umahiri mkubwa, naomba awaangalie watoto hawa kwa jicho la pekee, wapewe nauli ili unapofika wakati wa kurudi nyumbani basi waweze kurudi nyumbani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hostel zitasaidia sana kwa sababu, kwa mfano kule kwetu jamii ya Wamasai, kama mnavyofahamu, mtoto wa kike akiwepo nyumbani ni rahisi sana kuolewa. Naomba sana hostel kwa ajili ya shule ambazo zipo kwa mfano Shule ya Sekondari ya Oldonyowasi ambayo ni mpya imejengwa hivi karibuni na ndio wameanza kidato cha kwanza. Naomba ujenzi wa hostel katika Shule hii ya Oldonyowasi, ili basi waweze wanafunzi wale ambao wengi wao ni kutoka katika jamii yetu hii ya wafugaji waweze basi kukaa hostel.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naenda haraka haraka, vilevile naomba nizungumzie suala la Walimu; Walimu kwa kweli, kukopa kunasaidia na asiyekopa hafahamu nini maana ya kukopa, lakini baadhi ya taasisi za kifedha zinawaumiza Walimu na baadhi ya Walimu wamekwishaacha shule. Naomba niitaje Baypot imekuwa ni kikwazo kikubwa kwa Walimu ambao kwa kweli, wengine wamelazimika kuacha shule na kukimbia ili kukwepa hiyo mikopo ambayo imekuwa ni kero kubwa kwao. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha uko hapa, alitazame hili ili kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana TARURA na kipekee kabisa kwa sababu, natoka Mkoa wa Arusha, nampongeza Meneja wa TARURA Mkoa wa Arusha, nampongeza Meneja wa TARURA katika Halmashauri ya Arusha DC. Niombe tu sasa kwamba, kweli wanahitaji kuangaliwa ni kwa jinsi gani tunawaongezea bajeti ili waweze kutimiza yale malengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo ambalo kwa kweli ni la kutolewa mfano. Ni jambo ambalo kwa kweli, la kushukuru Serikali kwa jinsi ambavyo imeweza kujenga vituo vya afya na vituo hivi vya afya vinakwenda kutatua changamoto ya vifo vya wanawake na watoto. Haijawahi kutokea, tuna kila sababu ya kujivunia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli ambaye, tumeona fedha zinazopatikana zinatumika katika kuhakikisha kwamba, zinafanya yale ambayo yamekusudiwa. Vituo hivi pamoja na hospitali za wilaya zinazokwenda kujengwa haya ni mapinduzi makubwa ya maendeleo, naipongeza sana Serikali yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hilo tu pia tumeona ni kwa jinsi gani Rais wetu kutokana na utawala bora amedhihirisha miradi hii mikubwa kama kusingekuwa na utawala bora, basi isingewezekana; leo hii kuna Stieglers Gorge, tunaona kwamba, nikwa jinsi gani tatizo changamoto ya umeme itakwenda kutatuliwa. Tumeona Mradi wa REA, lakini sio hilo tu, ujenzi wa reli ya kisasa, vyote hivi ni maendeleo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuangalie pia katika Jiji la Dar es Salaam, tuangalie Ji la Dodoma jinsi ambavyo unapendeza na majengo yale ya Serikali. Hii yote ni kutokana na utawala bora na matumizi sahihi kabisa ya fedha katika kuhakikisha kwamba tunasimamia na kuleta maendeleo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamesemwa, mimi naipongeza sana Serikali na Mawaziri kwa vifua walivyonavyo vya kuweza kuhimili yote hayo na msivunjike moyo. Kama ndani ya miaka mitatu ambapo sasa hivi tupo mwaka wa nne, Rais Magufuli ameweza kufanya yote hayo, wapo wengine ambao ndani ya miongo zaidi ya miwili mpaka leo hii hawana hata ofisi ya chama, kwa nini tusimpongeze Rais wetu Magufuli kwa kazi kubwa aliyofanya. Nampongeza sana, tunamtia moyo Rais wetu ili kuhakikisha kwamba anazidi kuwaletea Watanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba Watanzania wanaona na 2020 siyo mbali mwakani tutaona Watanzania watakachoenda kufanya na nina uhakika kwamba CCM itaendelea kutawala. Upinzani bado upo nyuma sana kwa hiyo sisi tutaendelea kutawala kwa sababu ya sera nzuri na utawala bora tulionao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Waheshimiwa Mawaziri hongereni sana, msivunjike moyo tuendelee kufanya kazi na sisi Wabunge kumbukeni ni askari miamvuli wenu humu ndani kwa hiyo kabla hamjafikiwa nyie sisi tutakuwa wa kwanza. Alluta continua, mapambano yanaendelea CCM iendelee kutawala. (Makofi)