Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nami fursa ya kuweza kuchangia kwenye wizara zetu mbili hizi, Wizara ya TAMISEMI pamoja na Utumishi na Utawala Bora. Kwanza kabisa ningependa nianze kwa kutoa shukrani nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Tano kwa juhudi kubwa ambazo inafanya katika kujaribu kutatua matatizo, kero na changamoto walizonazo wananchi wa Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini naishukuru Serikali kwa kutupatia fedha kwenye sekta ya afya ambapo tumepata jumla ya shilingi bilioni mbili na milioni 600 kwenye ujenzi wa hospitali ya wilaya pamoja na vituo viwili vya afya. Vile vile kwenye sekta ya elimu tumepata jumla ya shilingi bilioni moja milioni tisa na laki sita. Hizi zote zimekwenda kutatua changamoto mbalimbali kwenye jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru pia Serikali tulipata fedha za Mfuko wa Jimbo shilingi milioni hamsini na tisa na laki moja ambazo kwa kweli zimekwenda kwa kiasi kikubwa kuchangia changamoto za ujenzi kwenye kata zetu zote 21. Kwa hiyo naishukuru sana Serikali kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi kubwa ambazo Serikali yetu imefanya, ziko changamoto mbalimbali ambazo ningependa nijaribu kuzisemea hasa nikianza na sekta ya elimu. Kwenye sekta ya elimu Mkoa wetu wa Singida bado haufanyi vizuri sana katika masuala ya matokeo, lakini ziko changamoto kadhaa ambazo zinachangia kutokufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto hizo ni miundombinu. Kazi kubwa ya Serikali imefanyika na hasa kwenye jimbo langu nami nilipata pia shilingi milioni 300 kwenye kujenga maboma 24. Naipongeza sana Serikali kwa hilo. Kwa shule za msingi peke yake yako maboma 68 ambayo wananchi wamekwishayaanzisha kwa muda mrefu na bado hayajakamilika mpaka leo. Ukienda kwenye shule za sekondari, uangalie kwenye shule za sekondari kwenye Jimbo langu pale maboma zaidi ya 69 ya maabara peke yake hapo hujagusa nyumba za Walimu, mabweni, matundu ya vyoo na vitu kama hivyo. Kwa hiyo bado tunayo changamoto kubwa kwa kweli kwenye kuwekeza, Serikali kuwekeza ili kuweza kusaidia juhudi hizi za wananchi. Maboma haya yameanzishwa mengine yana muda mrefu

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya afya, ninayo maboma kwa mfano kwenye Kata ya Ngimu liko jengo ambalo lilianzishwa na wananchi kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita na mpaka leo halijaweza kukamilishwa. Ukienda pale Kata ya Makuro vile vile na sasa hivi wananchi wengi wameanza sasa kwenye kata nyingine vile vile, Kata ya Msisi wameanzisha ujenzi wa jengo la kituo cha afya, ukienda Kinyajigi pale wameanzisha. Juhudi hizi za wananchi zinahitaji kuungwa mkono na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ombi langu kwa Serikali ni kwa Serikali kuongeza bajeti hii ya kukamilisha maboma ambayo tayari wananchi wamekwishayaanzisha kwa nyakati tofauti na wamefanya kazi kubwa ili tusiwakatishe tama. Tukumbuke kwamba uwezo wa kuyamaliza majengo yale haupo kwa wananchi kwa sasa kwa sababu miradi mingi ya Serikali ambayo inakwenda iwe ni hospitali za wilaya, vituo vya afya, majengo ya shule wananchi wanatakiwa kuchangia asilimia 20 ya maeneo hayo. Kwa hiyo niombe sana Serikali tuongeze bajeti ya maendeleo katika kukamilisha maboma haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kubwa ambalo linatoa duni kwa kweli kwenye sekta ya elimu lakini vile vile na huduma za afya ni watumishi tulionao kwenye sekta zetu. Nitatolea mfano wa Jimbo langu la Singida Kaskazini, kwenye sekta ya shule ya msingi peke yake tunahitaji waalimu zaidi ya 1,733 hivi tunavyozungumza tuna waalimu 860 sawa sawa na asilimia 49.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye sekta nyingine ukienda kilimo unakuta watumishi wako 16, kwenye vijiji 84 na kata 21, ukienda kwenye shule za msingi upungufu wa Walimu na maeneo mengine. Ni kweli Serikali kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri Serikali ilitoa ajira na kwa mwaka uliopita ajira 4,811 za Walimu. Idadi hii ya ajira iliyotoka kwenye sekta ya elimu peke yake ni ndogo sana. Ukijaribu kuangalia kwenye takwimu ambazo zipo za usajili wa wanafunzi kwa mwaka wa jana, mwaka huu ambao ndiyo tunaendelea nao peke yake wamesajiliwa wanafunzi wa elimu ya awali na shule za msingi kwa zaidi ya wanafunzi 2,900,000 ambao peke yake kwa idadi hiyo ilitakiwa wapatikane Walimu ambao watahudumia wanafunzi hao Walimu zaidi ya 65,550.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona karibu asilimia 36 ya Walimu wote waliojiriwa mwaka jana wanakwenda kufanya kazi tu ya kuelimisha wale wa darasa la awali na darasa la kwanza. Kwa hiyo bado tunalo tatizo kubwa, niombe sana Wizara ya Utumishi pamoja na TAMISEMI ambazo zote bahati nzuri ziko chini ya Ofisi ya Mheshimiwa Rais, waangalie namna ya kuweza kuongeza ajira kwa watumishi hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo twende pamoja na maslahi ya watumishi ambao kama tulivyosema kwa zaidi ya miaka mitatu sasa bado watumishi hawajaongezewa mishahara. Idadi ya Walimu tulionao tukumbuke hawa ni wale ambao tunao kwenye takwimu, wengine wako masomoni, wengine wana mashauri mbalimbali, ninayo, naweza nikatolea mfano wa Shule moja ya Msingi Mwasauya ambayo ina Walimu saba, watatu hawapo, wako masomoni, mmoja tayari ana mashauri, wanaoingia darasani ni Walimu watatu kwa shule nzima yenye wanafunzi zaidi ya 400.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hali hii hatutegemei kuwa na miujiza sana ya kufanya vizuri. Kwa hiyo, niombe sana hasa kwa mikoa hii ambayo haifanyi vizuri kama Mkoa wa Singida tupewe kipaumbele cha kupewa watumishi wa kutosha na kuwapunguzia matatizo Walimu hawa ambao wanafanya kazi katika mazingira magumu. Madarasa bado hayatoshi na wengi uwiano kule kwetu unafika mpaka kwa Mwalimu mmoja wanafunzi mpaka zaidi ya 100. Kwa hiyo, naomba sana Wizara iangalie suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la TARURA tunawapongeza sana. Tumeunda Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini lakini nami pia nilikuwa najaribu kuangalia katika mgawanyo wa fedha za TARURA ambao wamekwenda kwenye bajeti ya mwaka huu, yako maeneo mengi ambayo kwa kweli tumepata fedha kidogo. Mkoa wa Singida peke yake tumepata bilioni nne na milioni mia tano, lakini ziko halmashauri hasa kwenye majiji, manispaa moja inapata zaidi ya bilioni saba, zaidi ya bilioni sita wakati Mkoa mzima wa Singida ni bilioni nne na milioni mia tano peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana ndugu Mheshimiwa Jafo, mjaribu kuangalia, tunayo matatizo makubwa sana kwenye barabara zetu kule vijijini na tukiendelea kutoa fedha kiasi kidogo kiasi hiki kwa kweli wananchi wetu watapata matatizo sana. Mimi kwenye jimbo langu yako maeneo mengi, iko barabara ambayo tuliiomba kwa Mheshimiwa Rais kutoka Kinyeto – Kinyagigi – Meria inakwenda mpaka Sagara kule lakini naona haijatengewa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hatujatengewa fedha kwenye baadhi ya madaraja na maeneo mengine, kwa mfano tunalo Daraja la Songa, Kinyeto - Ilongero pale Ntambuko lakini tuna eneo la Mgori – Kikio, haya ni maeneo sugu ambayo tunayo lakini ukienda kwenye fedha ambazo sisi tumetengewa kwenye maeneo hayo ambayo ni ya matengenezo ya dharura sisi maeneo korofi hatujatengewa fedha hata senti moja lakini ukienda pia kwenye marekebisho pale hatujatengewa hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana muende mkafanye review ili pia Halmashauri ya Singida DC waweze pia na wao kupata fedha zitakazoweza kutosheleza. Barabara hizi tunazozungumzia ni muhimu sana kwa uchumi wa Jimbo la Singida Kaskazini.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Monko.

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)