Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 - Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza mtoa hoja, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kazi nzuri anayoifanya. Pia nitumie nafasi hii kuwapongeza wasaidizi wake, Mheshimiwa Jenista pamoja na Mheshimiwa Angellah Kairuki pamoja na Naibu Mawaziri wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa sisi katika Wizara yetu, tuna mambo mawili, moja ubadhirifu wa fedha za miradi ya maji vijijini. Tukiri kabisa kulikuwa kuna changamoto kubwa sana hasa katika maeneo ya vijijini kuona fedha zinalipwa lakini mradi haujakamilika na hata ukikamilika unatoa maji leo, kesho hautoi. Sisi hiyo kama changamoto tumeiona na baada ya kubadili muundo kwa maana Wahandisi wa Maji wengi walikuwa hawawajibiki kwetu na kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini, tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kupitisha Muswada ule na Mheshimiwa Rais amekwisha usaini, tunaamini uanzishwaji wa Wakala wa Maji Vijijini tunaenda kuwa na muarobaini ambao utaenda kutatua tatizo la maji kabisa vijijini. Tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali kwa Wahandisi wa Maji pamoja na wakandarasi wababaishaji ambao wanatuchelewesha katika utekelezaji wa miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili ni kuhusu suala zima la ulipaji wa madeni ya wakandarasi. Utekelezaji wa miradi ya maji unategemeana na fedha. Tulikuwa na madeni takribani zaidi ya shilingi bilioni 88 tunayodaiwa na wakandarasi, lakini nitumie nafasi hii kuwashukuru sana Wizara ya Fedha kuliona hilo, wametupa takribani zaidi ya shilingi bilioni 44 ndani ya mwezi uliopita na wametupa commitment ndani ya mwezi huu watatupa tena shilingi bilioni 44. Kwa hiyo, tupo vizuri na tumejipanga katika kuhakikisha kwamba tunakamilisha miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Hussein, amezungumzia hoja ya mradi wake wa Nyang’wale, tumelipa zaidi ya Sh.1,705,000,000. Mwambie mkandarasi afanye kazi, hana uwezo, tutamuondoa katika kuhakikisha miradi ya maji inakamilika ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto, yapo mafanikio makubwa sana. Sisi kama Wizara ya Maji ambayo siyo Wizara ya Ukame, ukienda Arusha zaidi ya mradi wa shilingi bilioni 520; mradi wa Same Mwanga zaidi ya Dola milioni 300; ukienda Longido zaidi ya bilioni 16 wananchi wanapata maji; tunatoa maji Zziwa Victoria na kuleta Tabora, Nzega na Igunga na hata Simiyu kwa Mheshimiwa Mbunge wa Bariadi kwako Mwenyekiti tunakupelekea maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumejipanga vizuri katika kuhakikisha kwamba hatutokuwa kikwazo sisi kama Wizara ya Maji kwa wananchi na Waheshimiwa Wabunge ili wananchi wetu waweze kupata maji safi salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)